Uga ni nini? Na kazi yake ni ipi kibiblia?

by Admin | 5 December 2020 08:46 pm12

Uga ni sakafu ya kupuria/kupepetea nafaka iliyotumika zamani.

Ikumbukwe kuwa zamani, hawakuwa na mashine za kupuria kama tulizonazo sasahivi baadhi ya sehemu, ilikuwa nafaka ikishatolea shambani, na majani yake, ilipelekwa moja kwa moja kwenye sakafu hii maalumu iliyonyooka ambayo ilijengwa kwa mawe, au  juu ya ardhi ngumu,..Karibu kila shamba lilikuwa ni lazima liwe na sakafu yake maalumu kama hii, na kama shamba ni dogo, basi waliungana wawili au watatu kushea Uga mmoja.

Tazama picha juu,

Sasa nafaka ilipokuwa ikipelekwa pale, hatua ya kwanza, ilimwagwa kwenye Uga huo, kisha wanyama, kama Ng’ombe, au Punda, au Farasi, walipitishwa juu ya nafaka hiyo kuikanyanga kanyaga..Na lengo la kufanya hivyo  ni kuyalegeza magamba  magumu yaliyoishikilia nafaka.

Sehemu nyingine walitumia fimbo badala ya wanyama, na kuzichapa kama vile wanavyochapa maharage au mbaazi, katika baadhi ya sehemu tunazoishi, vivyo hivyo katika enzi za biblia hususani kipindi kile cha Ruthu.

Sasa baada ya hatua hiyo, kilichofuata, ilikuwa ni kupepeta ili kuondoa hayo makapi yaliyochanganyikana na nafaka.. Hivyo walitumia kifaa maalumu kilichoitwa pepeto.. pepeto lililotumika wakati ule, halikuwa kama hili la kwetu, la chekecheke, hapana, bali lilikuwa ni beleshi fulani ambalo mbeleni lina mdomo kama wa uma, au rato.

pepeto

Hivyo walichokifanya ni kupitisha pepeto hilo katikati ya mchanganyiko huo wa nafaka na makapi, na kurusha juu, waliporusha juu, yale makapi yalichukuliwa na upepo na nafaka kurudi chini, na hivyo, wanairudia hatua hiyo, tena na tena na tena..mpaka nafaka peke yake ibaki chini kwenye ile sakafu. (Uga)

Kisha inaichotwa na kwenda kusagwa ajali ya matumizi ya nyumbani.. Hayo ndiyo yalikuwa matumizi ya Uga.

Unaweza kulisoma neno hilo katika vifungu hivi baadhi;

Ruthu 3:1 “Kisha Naomi akamwambia mkwewe, Je! Mwanangu, si vizuri nikutafutie raha, ili upate mema?

2 Basi na huyu Boazi, je! Siye wa mbari yetu, ambaye ulikuwapo pamoja na wasichana wake? Tazama, usiku wa leo atakuwa akipepeta shayiri pale ugani.

3 Basi wewe oga, ujipake mafuta ujivike mavazi yako, kisha uende kwenye uga; walakini usijionyeshe kwake mtu yule, ila atakapokwisha kula na kunywa”.

Soma pia kwa wakati wako, Ruthu 3:6,14,  1Nyakati 13:9, Yoeli 2:24, 1Samweli 14: 2 , Hosea 13:3, Yeremia 51:33

Je kuna umuhimu wowote wa sisi kufahamu juu ya Uga?

Jibu ni ndio, kwa kujua hilo itatusaidia kufahamu, Yohana alimaanisha nini pale inaposema juu ya habari za Yesu kuwa pepeto lake lipo mkononi mwake, kuusafisha uwanda wake..

Tusome;

Mathayo 3:11 “Kweli mimi nawabatiza kwa maji kwa ajili ya toba; bali yeye ajaye nyuma yangu ana nguvu kuliko mimi, wala sistahili hata kuvichukua viatu vyake; yeye atawabatiza kwa Roho Mtakatifu na kwa moto.

12 Ambaye pepeto lake li mkononi mwake, naye atausafisha sana uwanda wake; na kuikusanya ngano yake ghalani, bali makapi atayateketeza kwa moto usiozimika”.

Anachofanya Kristo leo hii ulimwenguni, ni kuusafisha uwanda wake(sakafu yake ya kupepetea ambalo ndio kanisa lake), na anaisafisha kwa pepeto, (uma) ulio mkononi mwake, Hivyo sote ni kama tunarushwa rushwa juu, na kama wewe utakuwa ngano halisi utashuka chini, lakini ukiwa kapi jepesi, utapeperushwa na upepo. Na baadaye utakusanywa na kwenda kuchomwa moto usiozimika.

Zipo pepo za aina nyingi leo hii ndugu yangu, Upepo wa mafundisho ya uongo, upepo wa unasa, upepo wa uzinzi, upepo wa fedha n.k..vyote hivi vinawapeperusha watu, Hizi ni nyakati za mwisho. Injili tuliyonayo sasa hivi sio injili ya kupembelezwa tena, ni injili ya kujichunguza umesimama wapi.  Na unakwenda wapi. Hakuna mtu ambaye hajawahi kusikia injili, hivyo ni wajibu wako wewe mwenyewe kuhakikisha Kristo yupo ndani yako. Ili uwe mahali salama.

Shalom.

Tazama  maana ya maneno mengine ya biblia chini.

Tafadhali washirikishe na wengine habari hizi njema, na pia kama utapenda tuwe tunakutumia mafundisho ya Neno la Mungu ya mara kwa mara kwa njia ya email yako au Whatsapp basi tutumie ujumbe kwenye namba hii +255693036618 au +255789001312

Mada Nyinginezo:

USIPIGE MATEKE MCHOKOO!

Hisopu/ Hisopo ni nini katika biblia?(Zaburi 51:7)

Bwana Yesu alikufa akiwa na umri gani?

Duara ya Ahazi ni ipi? Na je! Kivuli cha Hezekia kilirudije nyuma?

Mungu anaposema “nitaliweka jina langu” ana maana gani?

Rudi nyumbani

DOWNLOAD PDF
WhatsApp

Source URL: https://wingulamashahidi.org/2020/12/05/uga-ni-nini-na-kazi-yake-ni-ipi-kibiblia/