MAMBO YA KUJIFUNZA KATIKA KITABU CHA TITO.

by Admin | 28 March 2021 08:46 am03

Kitabu cha Tito ni waraka ulioandikwa na Mtume Paulo, kwa mtu anayejulikana kama Tito. Tito alikuwa ni mmoja wa watu waliogeuzwa kumgeukia Kristo, kupitia injili ya Mtume Paulo. Na mtu huyu alikuwa ni mwenyeji wa mji ulioitwa Krete.

Krete ni kisiwa kilichopo kusini mwa nchi ya Ugiriki, zamani kilikuwa kinaitwa Krete na hata leo hii bado kinaitwa hivyo hivyo Krete.

Kwahiyo Mtume Paulo katika ziara zake za kuhubiri, alifika pia katika kisiwa hicho, na hatimaye huyu Tito akawa mmoja wa matunda yake katika Injili. Na kwa kuwa alikuwa na bidii Zaidi  kuliko wengine, akachaguliwa kwa uongozo wa Roho Mtakatifu kuwa mwangalizi wa makanisa ya huo miji.

Na Paulo na wenzake baada ya kuondoka katika huo mji, kwenda kwenye miji mingine kwajili ya kuhubiri injili, ilibidi amwandikie waraka Tito, na kumpa maagizo machache ya namna ya kulijenga kanisa, Na maagizo hayo yalikuwa yamegawanyika katika vipengele viwili. 1) Maagizo jinsi ya kuteua viongozi wa kanisa na 2) Maagizo kwa waumini wote wa kanisa.

 1. MAAGIZO JINSI YA KUTEUA VIONGOZI WA KANISA.

Uteuzi wa viongozi ulitegemea vigezo fulani vya kimaandiko, hivyo ilibidi Paulo amfundishe Tito vigezo vya maaskofu, wachungaji na wazee wa kanisa, wanavyopaswa wawe, ili kanisa lisije likaanguka kwa kukosa uongozi thabiti, kutokana na kuwa viongozi wasio na vigezo. Hivyo Paulo kwa uongozo wa Roho akamwandikia Tito waraka huo na baadhi ya mambo aliyomwambia ni kama yafuatayo..

Tito 1:4 “ Tito, mwanangu hasa katika imani tuishirikiyo. Neema na iwe kwako na amani zitokazo kwa Mungu Baba na kwa Kristo Yesu Mwokozi wetu.

5 Kwa sababu hii nalikuacha Krete, ili uyatengeneze yaliyopunguka, na kuweka wazee katika kila mji kama vile nilivyokuamuru;

6 ikiwa mtu hakushitakiwa neno, naye ni mume wa mke mmoja, ana watoto waaminio, wasioshitakiwa kuwa ni wafisadi wala wasiotii.

7 Maana imempasa askofu awe mtu asiyeshitakiwa neno ,kwa kuwa ni wakili wa MUNGU;asiwe mtu wa kujipendeza nafsi yake,asiwe mwepesi wa hasira, asiwe mlevi wala mgomvi, asiwe mpenda mapato ya aibu.

8 bali awe mkaribishaji, mpenda wema, mwenye kiasi, mwenye haki, mtakatifu, mwenye kudhibiti nafsi yake;

9 akilishika lile neno la imani vile vile kama alivyofundishwa, apate kuweza kuwaonya watu kwa mafundisho yenye uzima, na kuwashinda wenye kupinga.

10 Kwa maana kuna wengi wasiotii, wenye maneno yasiyo na maana, wadanganyaji, na hasa wale wa tohara, ambao yapasa wazibwe vinywa vyao.

11 Hao wanapindua watu wa nyumba nzima, wakifundisha yasiyowapasa kwa ajili ya mapato ya aibu”

 2. MAAGIZO KWA WAUMINI WOTE WA KANISA.

Na pamoja na hayo, Paulo alimpa maagizo ndugu Tito, Na maagizo hayo yalikuwa ni maonyo kwa waumini wote, wazee wakike kwa wa kiume, na vijana wa kike kwa wakiume, na watumwa.

Aliwaonya wazee wanawake wawe katika utakatifu, ili wawe vielelezo kwa wanawake vijana, kadhalika na watumwa wawatii Bwana zao.

Tito 2:1 “Lakini wewe nena mambo yapasayo mafundisho yenye uzima;

2 ya kwamba wazee wawe wenye kiasi, wastahivu, wenye busara, wazima katika imani na katika upendo na katika saburi.

3 Vivyo hivyo na wazee wa kike wawe na mwenendo wa utakatifu; wasiwe wasingiziaji, wasiwe wenye kutumia mvinyo nyingi, bali wafundishao mema;

4 ili wawatie wanawake vijana akili, wawapende waume zao, na kuwapenda watoto wao;

5 na kuwa wenye kiasi, kuwa safi, kufanya kazi nyumbani mwao, kuwa wema, kuwatii waume zao wenyewe; ili neno la Mungu lisitukanwe.

6 Vivyo hivyo na vijana waume uwaonye kuwa na kiasi;

7 katika mambo yote ukijionyesha wewe mwenyewe kuwa kielelezo cha matendo mema, na katika mafundisho yako ukionyesha usahihi na ustahivu,

8 na maneno yenye uzima yasiyoweza kuhukumiwa makosa, ili yule mwenye kupinga atahayarike, kwa kuwa hana neno baya la kunena juu yetu.

9 Watumwa na wawatii bwana zao, wakiwapendeza katika mambo yote; wasiwe wenye kujibu,

10 wasiwe waibaji; bali wauonyeshe uaminifu mwema wote, ili wayapambe mafundisho ya Mwokozi wetu Mungu katika mambo yote.

11 Maana neema ya Mungu iwaokoayo wanadamu wote imefunuliwa”.

Na pia Mtume Paulo, alimpa maagizo Tito, kuwa awakumbushe watu kunyenyekea kwa wenye mamlaka..

Tito 3:1 “Uwakumbushe watu kunyenyekea kwa wenye uwezo na mamlaka, na kutii, na kuwa tayari kwa kila kazi njema;

2 wasimtukane mtu ye yote, wasiwe wagomvi, wawe wema, wakionyesha upole wote kwa watu wote”.

Na mwisho, akamwambia maneno haya..

Tito 2: 15 “Nena maneno hayo, onya na kukaripia kwa mamlaka yote; asikudharau mtu awaye yote”.

Katika waraka huu tunajifunza mambo kadhaa.

 1. Kwanza tunajifunza kanisa la Kristo linaongozwa na maaskofu, wachungaji, walio na vigezo vya kimaandiko, kama tulivyovisoma hapo juu..

2. Na pia kila mshirika wa kanisa, ni lazima ajifunze kuishi maisha ya utakatifu, Kama ni mzee fahamu kuwa kuna vijana chini yako na watoto, ambao wanapaswa kujifunza kutoka kwako, wakikuona wewe mzee una mizaa je watajifunza nini kutoka kwako?..wakikuona wewe mzee unavaa vibaya watajifunza nini kutoka kwako?.

Vivyo hivyo kama wewe ni mtumwa, labda unafanya kazi katika shirika fulani, au na juu yako wapo wakubwa kuliko wewe, halafu wanakuona huna adabu, ni mwizi, na sio mnyenyekevu, je unawatengenezea picha gani kuhusu ukristo?

Na pia kinatufundisha sisi kama washirika wa mwili wa Kristo, kunyenyekea kwa wenye mamlaka. Haijalishi mwenye mamlaka ni nani, biblia imetuonya tuwaheshimu na kuwanyenyekea, unyeyekevu unaozungumziwa hapo sio kuwaabudu au kuwaogopa kiasi kwamba hata wakikuambia usimwabudu Mungu wako uwatii.. Hapana! Bali unyenyekevu unaozungumziwa hapo ni ule wa wewe kufuata na kutii maelekezo yao yote ambayo yanaelekeza kufanya mema, na kuwaheshimu kama unavyowaheshimu watu wengine wote.

Kwamfano mwenye mamlaka katika mji wako amesema  “siku fulani ni ya kufanya usafi” hapo huna budi kutii.

 3. Na jambo la mwisho tunaloweza kujifunza ni kukaripia, na kuonya kwa mamlaka yote watu wote wanaokwenda kinyume na Neno la Mungu ndani ya kanisa. Paulo alimwambia Tito akaripie, hivyo hata leo tuna jukumu hilo hilo, la kukaripia uzinzi na wazinzi waliopo kanisani, kukaripia walevi waliopo kanisani, kukaripia watukanaji na wavaaji vibaya kanisani, tena biblia imesema kwa tufanye hivyo kwa mamlaka yote, bila hofu kwasababu si dhambi. Wengi wanaogopa kukaripia kwasababu wanahisi kwamba watakuwa wanawahukumu watu. Hapana!. Kuambiwa ukweli sio kuhukumiwa bali ni kuonywa. Na biblia na ukristo kwa ujumla, dhima yake kubwa ni maonyo! Hakuna kitu kingine, kama hutaki maonyo, basi ukristo haukufai.

Bwana atubariki.

Kama hujampokea Yesu, kama bado unavaa vimini, kama bado ni mlevi, mshirikina,  mwizi n.k fahamu kuwa ukifa leo unakwenda jehanamu. Hivyo ni bora ukampokea Yesu leo kwa kutubu, na kuacha kufanya dhambi, ili upate wokovu na msamaha wa dhambi.

Yesu Kristo yupo mlangoni kurudi !!!.

Tafadhali washirikishe na wengine habari hizi njema,

Kwa maombezi/Ratiba za ibada/ Ushauri/ Maswali.
Piga namba hizi: +255693036618 au +255789001312

pia kama utapenda uyapate mafundisho haya kwa njia ya Whatsapp au email basi tutumie ujumbe kwenye namba hizo hizo.


Mada Nyinginezo:

MAMBO YA KUJIFUNZA KATIKA KITABU CHA FILEMONI.

KUJIPAMBA NI DHAMBI?

KITABU CHA YUDA: SEHEMU YA 3

JINSI MTUME PAULO ALIVYOUTHAMINI WITO WAKE, JUU YA WENYE VYEO.

UFUNUO Mlango wa 2: Sehemu ya pili.

Rudi nyumbani

DOWNLOAD PDF
WhatsApp

Source URL: https://wingulamashahidi.org/2021/03/28/mambo-ya-kujifunza-katika-kitabu-cha-tito/