JIHUDHURISHE, ILI AANZISHE MAZUNGUMZO NA WEWE

by Admin | 5 April 2022 08:46 am04

Nakusalimu katika jina la mwokozi wetus Yesu Kristo, sifa na utukufu vina yeye milele na milele. Amina.

Unafahamu kuwa shetani ambaye ni adui yetu, si kila wakati anafanya mambo yake kwa kutegemea jitihada zake tu, anajua  kabisa mambo mengine huwa hayatoki isipokuwa kwa kufuata kanuni ambazo tayari Mungu alishaziweka.

Na huwa anazitumia hizo kanuni, kutuharibu sana, lakini sisi kama wana wa ufalme, hatuzitumii kumuharibu yeye.

Kwamfano madhara aliyopanga kumletea  Ayubu, alitambua kuwa haiwezekani kwa njia ya kawaida kuyatekeleza ,. Ndipo akatumia njia ya juu Zaidi ya kujishusha, kwa kwenda KUJIHUDHURISHA mbele za Mungu,.

Akashusha kiburi chake hadi chini kabisa, akaungana na Malaika watakatifu wa Mungu, kupanda mbinguni, akaenda mbele ya uwepo wa Mungu, kwa unyenyekevu wote, akitumaini kuwa kwa kutenda kule, ni lazima tu Mungu atamwangalia, kwasababu Mungu ni Mungu wa uumbaji wote.

Na kweli baadaye Mungu alipomwona anatembea tembea mbele ya uwepo wake kwa muda mrefu, akaanzisha mazungumzo naye, Akamuuliza unatoka wapi shetani, akasema duniani, katika mizunguko yangu, ndipo shetani akatumia fursa hiyo ya mazungumzo, kupeleka na mashataka yake yote. Na mwisho wa siku akapatiwa haja yake.

Akashuka chini, akamfanya Ayubu kama alivyoweza kumfanya..

Ayubu 1:6 “Ilikuwa, siku moja ambayo hao wana wa Mungu walikwenda kujihudhurisha mbele za Bwana, Shetani naye akaenda kati yao.

7 Bwana akamwuliza Shetani, Umetoka wapi wewe? Ndipo Shetani akamjibu Bwana, na kusema, Natoka katika kuzunguka-zunguka duniani, na katika kutembea huku na huku humo.

8 Kisha Bwana akamwuliza Shetani, Je! Umemwangalia huyo mtumishi wangu Ayubu? Kwa kuwa hapana mmoja aliye kama yeye duniani, mtu mkamilifu na mwelekevu, mwenye kumcha Mungu na kuepukana na uovu”.

Tunachopaswa tujue ni nini, Ikiwa mungu wa dunia hii, anajua siri ya mafanikio ya uharibifu wake, haitegemei tu nguvu zake mwenyewe, bali pia kwa kujihudhurisha mbele za Mungu ..Unategemea vipi wewe na mimi tusiwe watu wa namna hiyo?

Shetani anatushangaa sana, tunapomkimbia Mungu, anatushangaa sana tunapokwenda mbali na uwepo wa Mungu, kwa visingizio visivyokuwa na maana, hatutaki kwenda kumfanyia Mungu ibada hata mara moja kwa wiki tunasema tumechoka, kwasababu jumatatu tunakwenda kazini hivyo hatuna budi tulale!! Ndugu ukitegemea nguvu zako kuyaongoza haya Maisha jihesabie tu wewe ni MKIA Maisha yako yote. Ndivyo ilivyo..

Hilo shetani alijaribu akaona halifai, na wewe unalijaribu, alijua si kila wakati nitajiamulia tu mimi mwenyewe, kwa nguvu zangu..Lazima niwe na muda wangu wa kwenda kujinyenyekeza, tena kwa muda mrefu mbele za Mungu.

Ikiwa tunaona mikesha ni shida, hata mara moja kwa mwezi, tusahau Mungu kuanzisha mazungumzo yoyote na sisi. Ikiwa hatujizoezi kusali mara kwa mara, na kuutafuta uso wa Mungu hata kwa mifungo wakati mwingine, tujue tu mambo mengi sana tutafeli kuyatimiza maishani mwetu.

Faida za kujihudhurisha mbele za Bwana ni zipi?.

Tunapokuwa uweponi mwa Bwana muda mrefu, Mungu mwenyewe ataanzisha mazungumzo na sisi, atatuuliza, unasumbukia nini, una haja gani, unatafuta nini? Kama tu alivyofanya kwa shetani…Lakini akitutazama hatupo uweponi mwake, Tunazunguka zunguka tu duniani, na masumbufu ya Maisha haya kila wakati, siku saba kwa juma, siku 365 za mwaka, na yeye ataendelea na mambo yake, atatuacha tutaabike wenyewe..

Biblia inasema..

Yakobo 4:8 “Mkaribieni Mungu, naye atawakaribia ninyi..”

Ndugu tujizoezi, kumkaribia Mungu kila siku, ibada inayotoka rohoni iwe ni sehemu ya Maisha yetu, Na bila shaka tutaanza kumuona Mungu akisema na roho zetu.

Kumbuka uanzapo kufanya mambo kama hayo kwa bidii, hutasikia sauti kama sauti ikisema na wewe, bali rohoni Mungu atakuwa anazungumza na Maisha yako. Na mara utaona yote uliyokuwa unamwomba, au unayatamani yatendeke tangu zamani, Mungu anakufanikisha kwa njia ambazo hujazitazamia. Hivyo ndivyo Mungu anavyozungumza na watu.

Tukiijua kanuni hii, shetani atatuchukia sana, kwasababu tutakuwa tumeshajua siri ya mafanikio yetu, kama yalivyokuwa yake katika huu ulimwengu.

Kama wewe ni mtakatifu, anza sasa kumpa Mungu muda wako wa kutosha, huko ndiko kujihudhurisha mbele zake, usiwe na udhuru wa kutokwenda ibadani, usiwe na udhuru wa kutohudhuria mikesha na wenzako, usiwe na udhuru wa kutokufunga na kuomba, na kujifunza Neno kila siku. JIHUDHURISHE kwa kadiri uwezavyo mbele za Mungu.

Ndivyo Mungu atakavyoanzisha mazungumzo na wewe.

Bwana akubariki.

Ikiwa bado upo nje ya Kristo, kumbuka kuwa, hatuna muda mrefu hapa duniani, Unyakuo ni wakati wowote, kulingana na kutimia kwa dalili zote zilizotabiriwa katika maandiko, na kama hilo halitoshi fahamu kuwa mlango wa neema, umeshaanza kufungwa, usipoiamini injili, leo, kesho itakuwa ni ngumu Zaidi, na siku moja hutaiamini kabisa. Kwasababu neema haidumu milele, maandiko yanasema hivyo!.

Hivyo tubu dhambi zako kwa kumaanisha leo, mgeukie Kristo, injili tuliyobakiwa nayo sasa sio ya kubembelezwa, ni wewe mwenyewe uone hali halisi, umgeukie muumba wako.

Maran Atha.

Tafadhali shea na wengine ujumbe huu;

Pia Kwa maombezi/ Ushauri/ Maswali/ Whatsapp:
Tuandikie katika BOXI la Maoni hapo chini au
Piga namba hizi: +255693036618 au +255789001312

Mada Nyinginezo:

TUSIRUHUSU MAMBO YA KUSUBIRISHA, YAVURUGE MUDA WETU NA MUNGU.

Amin, nawaambia, Kizazi hiki hakitapita..

Je! Shetani anao uwezo wa kuumba, kama Mungu?

“Vya Kaisari mpeni kaisari”  ni vipi hivyo tunavyopaswa tumpe?.

Rudi nyumbani

DOWNLOAD PDF
WhatsApp

Source URL: https://wingulamashahidi.org/2022/04/05/jihudhurishe-ili-aanzishe-mazungumzo-na-wewe/