Wakaanani walikuwa ni watu gani?

by Admin | 5 April 2022 08:46 am04

Wakaanani walikuwa ni watu wanaoishi katika nchi ya Kaanani. Kumbuka Kaanani alikuwa ni mtu, ambaye tunamsoma katika Mwanzo 9:18, kuwa alikuwa ni mwana wa Hamu, ambaye aliuona utupi wa baba yake.

Mwanzo 9:18 “Wana wa Nuhu waliotoka katika safina, ni Shemu, na Hamu, na Yafethi; na HAMU ndiye BABA WA KANAANI”.

Wakaanani ndio watu waliokuwa wanamiliki sehemu kubwa ya Israeli, kabla wa nawa Israeli hawajaingia nchi hiyo, ndio maana nchi ya Israeli hapo kwanza ilikuwa inaitwa nchi ya Kaanani, kwasababu hao wakaanani, ndio walikuwa wameshikilia sehemu kubwa ya nchi hiyo, Zaidi ya mataifa mengine machache kama Wahiti, Wahivi na Wayebusi.

Wakaanani walitawala ardhi ile kuanzia Kusini mwa nchi ya Lebanoni, mpaka karibia na mipaka ya nchi ya Misri.

Wakaanani walikuwa ni watu waliokuwa wanaabudu miungu, hivyo desturi zao zilifarakana na sheria wa Mungu wa Israeli, kwani walikuwa ni wachawi, watu wanaobashiri, wanaojichora, wanaotazama nyakati za hatari, wanaowapitisha Watoto wao kwenye moto kwaajili ya sadaka kwa miungu yao. N.k.

Kwasababu ya machukizo hayo, ambayo pia yalichangiwa na laana Mungu aliyomlaani Hamu, kwa kosa la kuuona uchi wa Baba yake, ndipo Mungu akawaondoa katika nchi hiyo na kuwapa wana wa Yakobo (yaani wana wa Israeli).

Kumbukumbu 18:9 “Utakapokwisha kuingia katika nchi akupayo Bwana, Mungu wako usijifunze kutenda kwa mfano wa machukizo ya mataifa yale.

10 Asionekane kwako mtu ampitishaye mwanawe au binti yake kati ya moto, wala asionekane mtu atazamaye bao, wala mtu atazamaye nyakati mbaya, wala mwenye kubashiri, wala msihiri,

11 wala mtu alogaye kwa kupiga mafundo, wala mtu apandishaye pepo, wala mchawi, wala mtu awaombaye wafu.

12 Kwa maana mtu atendaye hayo ni chukizo kwa Bwana; kisha ni kwa sababu ya hayo Bwana, Mungu wako, anawafukuza mbele yako.

13 Uwe mkamilifu kwa Bwana, Mungu wako.

14 Maana mataifa haya utakaowamiliki huwasikiliza wanaoshika nyakati mbaya na kutazama bao; bali wewe, Bwana, Mungu wako, hakukupa ruhusa kutenda hayo”.

Mbali na kwamba Wakaanani walikuwa ni watu WASIOFAA, lakini pia biblia inarekodi kuwa walikuwa ni watu Hodari, wakubwa kimwili na walioendelea sana. Ndio maana utaona Musa alipowatuma watu wakaipeleleze ile nchi yao, wale wapelelezi walikuja na ripoti za kuogopesha, kwani walijiona nafsi zao kama mapanzi mbele ya hao Wakaanani.

Hesabu 13:32 “Wakawaletea wana wa Israeli habari mbaya ya ile nchi waliyoipeleleza, wakasema, Ile nchi tuliyopita kati yake ili kuipeleleza, ni nchi inayowala watu wanaoikaa; na watu wote tuliowaona ndani yake ni watu warefu mno.

33 Kisha, huko tuliwaona Wanefili, wana wa Anaki, waliotoka kwa hao Wanefili; tukajiona nafsi zetu kuwa kama mapanzi; nao ndivyo walivyotuona sisi”.

Jamii ya Wakaanani sasahivi haipo tena, imepotea (Bwana ndiye aliyeitowesha).

Ni nini tunachoweza kujifunza kwa Wakaanani?

Kikubwa tunachoweza kujifunza ni kwamba mafanikio ya mtu au Taifa, sio kigezo cha kukubaliwa na Mungu.

Wakaanani walikuwa wameendelea kuliko Israeli, walikuwa na sayansi kubwa kuliko Israeli na mataifa mengi, lakini Mungu aliwaondoa katika ile nchi na kuwatowesha kabisa kwasababu walikuwa wanafanya machukizo.

Hiyo ni kutukumbusha na sisi watu wa siku za mwisho kuwa, Mafanikio ya kimwili sio kigezo cha kukubaliwa na Mungu. Leo hii kipimo cha kwanza cha mtu aliyebarikiwa na Mungu ni kiwango cha mali alicho nacho, na fedha alizonazo.. lakini Si utakatifu tena..

Bwana Yesu alisema..

Marko 8:36 “KWA KUWA ITAMFAIDIA MTU NINI KUUPATA ULIMWENGU WOTE, AKIPATA HASARA YA NAFSI YAKE?

37 Ama mtu atoe nini badala ya nafsi yake?

38 Maana kila mtu atakayenionea haya mimi, na maneno yangu, katika kizazi hiki cha uzinzi na dhambi, Mwana wa Adamu atamwonea haya mtu huyo, atakapokuja katika utukufu wa Baba yake pamoja na malaika watakatifu”.

Na Zaidi sana Neno la Mungu linatuhimiza tuutafute Utakatifu kwa gharama zote, kwasababu pasipo huo hatutamwona Mungu (Waebrania 12:14), Na utakatifu tunaupata kwa kumpokea Roho Mtakatifu ndani yetu.

Maran atha.

Tafadhali shea na wengine ujumbe huu;

Pia Kwa maombezi/ Ushauri/ Maswali/ Whatsapp:
Tuandikie katika BOXI la Maoni hapo chini au
Piga namba hizi: +255693036618 au +255789001312


Mada Nyinginezo:

Wahiti ni watu gani?

Moabu ni nchi gani kwasasa?

Wasamaria walikuwa ni watu gani?

TUMEFANYIKA KUWA WANA WA MUNGU!

Je Adamu na Hawa, walikuwa hawafanyi mema kabla ya kula tunda?

Rudi nyumbani

DOWNLOAD PDF
WhatsApp

Source URL: https://wingulamashahidi.org/2022/04/05/wakaanani-walikuwa-ni-watu-gani/