TOFAUTI YA UBATIZO WA YOHANA NA UBATIZO WA BWANA YESU

by Admin | 9 September 2022 08:46 pm09

Jina la Bwana na Mwokozi Yesu libarikiwe. Karibu tujifunze biblia.

Je kuna utofauti wowote ya Ubatizo wa Yohana na ule wa Bwana Yesu?,

Jibu ni kwamba hakuna utofauti wowote, ubatizo ni ule ule mmoja  wa toba, lakini kinachoutofautisha ule wa Yohana na ule wa Bwana Yesu ni “jina” Lakini ubatizo ni ule ule.

Kumbuka kabla ya Bwana Yesu kuja watu walikuwa wanasali, walikuwa wanafanya maombezi, na vitu vingine lakini walikuwa hawalitumii jina lolote, kwasababu hawakupewa maagizo hayo na Mungu. Hali kadhalika na Yohana alipokuja na ufunuo mpya wa ubatizo, alibatiza pasipo kuhusisha jina lolote. Maana yake baada ya watu kutubu kwa kumaanisha kuziacha dhambi zao, ishara ya mwisho ya wao kutakasika ilikuwa ni “kuzamishwa katika maji, na kuibuka juu” pasipo kutaja jina lolote.

Lakini Bwana Yesu alipokuja, mambo yalibadilika.. Kila kitu cha KIMungu ni lazima kifanyike kwa jina lake yeye..

Wakolosai 3:17 “Na kila mfanyalo, KWA NENO AU KWA TENDO, FANYENI YOTE KATIKA JINA LA BWANA YESU, mkimshukuru Mungu Baba kwa yeye”.

Kutokana na maagizo hayo, Mitume na wanafunzi wengine wa Bwana Yesu, walianza kulitumia jina la Yesu katika mambo yote yote ya kiMungu watakayoyafanya kwa NENO na kwa MATENDO.

Mfano wa MANENO ambayo walianza kutamka kwa jina la Yesu ni SALA zote NA MAOMBI  NA MAHUBIRI …ndio maana utaona walipokwenda kutoa pepo, na kuombea watu wenye magonjwa na madhaifu mbali mbali walitumia jina la Yesu,..

Luka 16:17 “Na ishara hizi zitafuatana na hao waaminio; KWA JINA LANGU watatoa pepo; watasema kwa lugha mpya”.

Vile vile utaona walipoenda kuhubiri na kufundisha, walifundisha kwa jina la Yesu..

Luka 24:46 “Akawaambia, Ndivyo ilivyoandikwa, kwamba Kristo atateswa na kufufuka siku ya tatu;

47 na kwamba mataifa yote watahubiriwa KWA JINA LAKE habari ya toba na ondoleo la dhambi, kuanza tangu Yerusalemu”.

Soma pia Matendo 4:18

Mfano wa matendo hayo yalikuwa ni ubatizo!..

Hayo yalikuwa ni Maneno, sasa utauliza vipi kuhusu Matendo..je! kuna matendo yoyote ambayo yalikuwa yanafanywa kwa jina la Yesu?.. Jibu ni ndio!

Kumbuka ubatizo si yohana peke yake aliyekuwa anafanya, bali na wanafunzi wake pia walikuwa wanawabatiza watu..kwasababu Yohana aliwafundisha hivyo, na zaidi sana utaona pia Adrea kabla ya kuwa Mwanafunzi wa Bwana Yesu alikuwa ni mwanafunzi wa Yohana. Hivyo alikuwa anaujua ubatizo vizuri na alikuwa akibatiza, kabla hata ya Bwana Yesu.

Lakini baada ya Bwana YESU kuja, na kufahamu kuwa mambo yote, ni lazima yafanyike kwa jina la Bwana Yesu, ikiwemo ubatizo pia, ndipo wote wakaacha kubatiza kama Yohana, kwa kuzamisha bila kutaja jina lolote, na wakaanza kubatiza kwa jina la Yesu.

Matendo 2:37 “Walipoyasikia haya wakachomwa mioyo yao, wakamwambia Petro na mitume wengine, Tutendeje, ndugu zetu?

38 Petro akawaambia, TUBUNI MKABATIZWE KILA MMOJA KWA JINA LAKE YESU KRISTO, mpate ondoleo la dhambi zenu, nanyi mtapokea kipawa cha Roho Mtakatifu”.

Umeona?.. kumbe hata ubatizo, ni lazima uwe kwa jina la Bwana Yesu ili ulete matokeo.. Ndio maana Mtume Paulo, alipokutana na wale watu kipindi wapo Efeso, aliwaambia wakabatizwe upya kwa jina la Yesu, ijapokuwa tayari walikuwa wameshabatizwa kwa ubatizo wa Yohana.

Matendo 19:1 “Ikawa, Apolo alipokuwa Korintho, Paulo, akiisha kupita kati ya nchi za juu, akafika Efeso; akakutana na wanafunzi kadha wa kadha huko;

2 akawauliza, Je! Mlipokea Roho Mtakatifu mlipoamini? Wakamjibu, La, hata kusikia kwamba kuna Roho Mtakatifu hatukusikia.

3 AKAWAULIZA, BASI MLIBATIZWA KWA UBATIZO GANI? Wakasema, Kwa ubatizo wa Yohana.

4 Paulo akasema, Yohana alibatiza kwa ubatizo wa toba, akiwaambia watu wamwamini yeye atakayekuja nyuma yake, yaani, Yesu

5 WALIPOSIKIA HAYA WAKABATIZWA KWA JINA LA BWANA YESU.

6 Na Paulo, alipokwisha kuweka mikono yake juu yao, Roho Mtakatifu akaja juu yao; wakaanza kunena kwa lugha, na kutabiri.”

Ndugu unayesoma ujumbe huu, fahamu kuwa kama hutabatizwa katika ubatizo sahihi, baada ya kuujua ukweli, utakuwa umemkataa Mungu moja kwa moja!!!.. na kuna madhara makubwa sana ya kutokubatizwa kwa jina la Bwana Yesu, (siku zote usilisahau hilo kichwani mwako).

Ikiwa bado hujampokea Yesu, kumbuka hizi ni siku za Mwisho, Kristo anarudi hivyo ni vizuri ukayatengeneza maisha yako kabla nyakati za hatari hazijafika.

Bwana akubariki.

Tafadhali shea na wengine ujumbe huu;

Pia Kwa maombezi/ Ushauri/ Maswali/ Whatsapp:
Tuandikie katika BOXI la Maoni hapo chini au
Piga namba hizi: +255693036618 au +255789001312

Mada Nyinginezo:

JE! UMEBATIZWA UBATIZO SAHIHI?

MFANO WA MAMBO HAYO NI UBATIZO.

UMUHIMU WA KUBATIZWA.

Je ni viatu gani Musa aliambiwa avivue?  Vya mwilini au vya rohoni? (Kutoka 3:5).

HAKUNA MTU ANIONDOLEAYE, BALI MIMI NAUTOA MWENYEWE

Rudi nyumbani

DOWNLOAD PDF
WhatsApp

Source URL: https://wingulamashahidi.org/2022/09/09/tofauti-ya-ubatizo-wa-yohana-na-ubatizo-wa-bwana-yesu/