HAKUNA MTU ANIONDOLEAYE, BALI MIMI NAUTOA MWENYEWE

HAKUNA MTU ANIONDOLEAYE, BALI MIMI NAUTOA MWENYEWE

Yapo mambo mengi Bwana Yesu aliyoyafanya ambayo katika akili za kawaida, ni ngumu kuaminika. Yapo mengi lakini leo tulitazame moja kuu, ambalo hakuna mwanadamu yeyote wala kiumbe chochote kinachoweza kufanya. Na jambo hilo si linguine zaidi ya  UWEZO WA KUUTOA UHAI WAKE NA KUURUDISHA.

Umewahi kujiuliza mtu anawezaje wezaje kuutoa uhai wake yeye mwenyewe na kujirudishia??..Ni kama vile hilo jambo haliwezekani ee?..Lakini liliwezekana kwa Jemedari, Mkuu wa Uzima, Yesu.. Hebu tusome mistari ifuatayo ili tuelewe vizuri….(Zingatia vipengele vilivyoanishwa kwa herufu kubwa)

Yohana 10:15  “kama vile Baba anijuavyo, nami nimjuavyo Baba. Nami NAUTOA UHAI WANGU KWA AJILI YA KONDOO.

16  Na kondoo wengine ninao, ambao si wa zizi hili; na hao nao imenipasa kuwaleta; na sauti yangu wataisikia; kisha kutakuwako kundi moja na mchungaji mmoja.

17  Ndiposa Baba anipenda, KWA SABABU NAUTOA UHAI WANGU ILI NIUTWAE TENA.

18  HAKUNA MTU ANIONDOLEAYE, BALI MIMI NAUTOA MWENYEWE. NAMI NINAO UWEZA WA KUUTOA, NINAO NA UWEZA WA KUUTWAA TENA. AGIZO HILO NALILIPOKEA KWA BABA YANGU.

19  Kukaingia tena matengano kati ya Wayahudi, kwa ajili ya maneno hayo.

20  Wengi wao wakasema, Ana pepo huyu, tena ana wazimu; mbona mnamsikiliza?.

21  Wengine wakasema, Maneno hayo siyo ya mtu mwenye pepo. Je! Pepo aweza kuwafumbua macho vipofu?”

Hapo Bwana Yesu anasema “Hakuna mtu autoaye uhai wake bali anautoa mwenyewe”.. Utauliza vipi pale msalabani, sio wale watu walimuua??.. Nataka nikuambie kuwa hawakumuua, biblia inasema “yeye mwenyewe aliitoa roho yake (Mathayo 27:50  “Naye Yesu akiisha kupaza sauti tena kwa nguvu, akaitoa roho yake”)

Ndio maana baadaye wale askari  walipotaka kwenda kuivunja miguu yake wakamkuta kashakufa..kwasababu kikawaida adhabu ya kutundikwa msalabani inamchukua mtu hata siku 4 ndipo afe..Maana lengo la wao kumsulubisha mtu msalabani sio afe tu!, bali afe kifo cha mateso, kama ingekuwa lengo ni kumuua tu, wangemkata kata na mapanga afe!… Kwahiyo waliposhangaa Bwana Yesu kafa mapema vile pale msalabani, iliwaogopesha na kuwashtusha sana, kuwa Yule ni mtu wa namna gani..Mpaka Pilato naye alishtuka!!.

Marko 15:43  “akaenda Yusufu, mtu wa Arimathaya, mstahiki, mtu wa baraza ya mashauri, naye mwenyewe anautazamia ufalme wa Mungu; akafanya ujasiri, akaingia mbele ya Pilato akauomba mwili wake Yesu.

44  LAKINI PILATO AKASTAAJABU, KWAMBA AMEKWISHA KUFA. akamwita yule akida, akamwuliza KWAMBA AMEKUFA KITAMBO”

Umeona jinsi Bwana Yesu alivyokuwa wa kipekee???. Hakuwa mtu wa kawaida Yule, bali alikuwa ni “Mungu katika Mwili wa kibinadamu”, kwasababu katika hali ya kawaida hakuna mwanadamu anayeweza kuamua kuutoa uhai wake. Unakaa tu na kuamua, kuiondoa roho yako??..hilo jambo haliwezekani kibinadamu.

Na kumbuka ipo tofauti kati ya “kuutoa uhai wake” na “kujiua”. Bwana Yesu hakujiua!, maana yake ingempasa afanye jambo la kujidhuru,  lakini yeye hakufanya hivyo, bali aliutoa uhai wake… Maana yake kama angeamua asiutoe uhai wake angeweza pia kukaa pale msalabani daima, wangempiga na kumtesa lakini asingekufa na wangeshangaa kwanini hafi.. Hiyo ni kwasababu Nguvu za Mauti na Uhai tayari zilikuwa mikononi mwake.

Na hajaishia hapo, anaendelea kusema “Ana uwezo wa kuutoa uhai wake na kuutwa tena”. Maana yake ana uwezo wa KUJIFUFUA PIA!!. Na agizo hilo alipokea kutoka kwa baba. Yaani agizo la kuutoa uhai wake na kuurudisha. Baba alimwambia afanye hivyo.. “sasa sio kosa kusema Bwana Yesu, alifufuliwa na Baba, ni sahihi kabisa kwasababu nguvu zote zinatoka juu, na ili utukufu wote apokee yeye, ni sahihi kusema Baba alimfufua, lakini kiuhalisia ni kwamba Baba alimpa maagizo na uwezo wa kujifufua mwenyewe.”

SASA NINI LENGO LA KUUTOA UHAI WAKE NA KUJIRUDISHIA??

Lengo la Bwana Yesu kuutoa uhai wake na kujirudishia sio kutuonyesha sisi kuwa yeye ni mtaalamu au mtu wa miujiza! Hapana, bali kulikuwa na maana kubwa sana kiroho, kwanini autoe uhai wake na kujirudishia.

Ili tuelewe vizuri hebu tafakari mfano ufuatao.

Umenunua simu na haiwezi kuingia internet, wenye mtandao wakakwambia wanakutumia settings za internet, zikubali na baada ya HAPO ZIMA SIMU YAKO NA KUIWASHA TENA, ili ziweze kufanya kazi. Sasa lengo la wao kukuambia uzime simu yako na kuiwasha baada ya kupokea hizo settings, si kwasababu hawapendi simu yako iwe imewaka muda wote, hapana!.. Lengo la wao kukuambia ufanye vile ni kwasababu zile settings ili ziweze kufanya kazi ni lazima program zote kwenye simu ziache kufanya kazi kwa muda ili hizo mpya zinapoingia zipate nafasi, na unapowasha simu unakuta tayari zile settings za internet zimeanza kufanya kazi kwenye simu yako, na unajikuta unaweza kuingia internet.  Lakini usipofanya hivyo (usipozima simu yako na kuiwasha), utabaki nazo tu ndani ya simu yako na hazitakusaidia chochote.

Na kama umegundua simu yenye uwezo mkubwa kidogo ina uchaguzi wa kujiwasha na kujizima yenyewe yaani “restart button”, kiasi kwamba ukibonyesha hiyo “restart” simu inajizima yenyewe na kujiwasha, pasipo wewe kuizima wala kuiwasha.

Na Bwana Yesu, ni hivyo hivyo baada ya kupokea maagizo ya uzima wa milele, kwamba injili lazima ihubiriwe ulimwenguni kote, Ilikuwa ni lazima “afe na kufufuka”. Kulikuwa hakuna namna..vinginevyo ukombozi usingeenea kila mahali.. Ni kama tu zile settings za internet, zisipofanya kazi katika simu haiwezekani kujiunganisha na ulimwengu wote. Na zinaingia kwa kuizima simu na kuiwasha tena.

Hiyo ndio sababu ya Bwana Yesu kuuondoa  uhai wake yeye mwenyewe na kuurudisha tena. Haleluya!!. Kwa lugha ya kueleweka ni kama ali-restart uhai wake. Alisema maneno yafuatayo..

Yohana 12: 24  “Amin, amin, nawaambia, Chembe ya ngano isipoanguka katika nchi, ikafa, hukaa hali iyo hiyo peke yake; bali ikifa, hutoa mazao mengi”.

Umeona kwahiyo Bwana Yesu ilimpasa afe, na kufufuka kwa faida yetu sisi, hususani sisi watu wa Mataifa.. Ndio maana hapo alisema “anao kondoo wa zizi linguine” maana yake ni sisi watu wa Mataifa…kondoo wa zizi lake ni wayahudi. Hivyo ili atupate na sisi watu wa mataifa ilimpasa atoe uhai wake na kuutwaa tena..

Yohana 10:15  “kama vile Baba anijuavyo, nami nimjuavyo Baba. Nami NAUTOA UHAI WANGU KWA AJILI YA KONDOO.

16  Na kondoo wengine ninao, ambao si wa zizi hili; na hao nao imenipasa kuwaleta; na sauti yangu wataisikia; kisha kutakuwako kundi moja na mchungaji mmoja”

Je umemwamini Yesu?.. Je unamheshimu yeye ambaye aliutoa uhai wake ili kuja kukupata wewe kondoo wa mbali uliyepotea??.  Je umemthamini kwa kutii maagizo yake ya msingi, ya kutubu dhambi zako, na kubatizwa katika ubatizo sahihi wa maji mengi na kwa jina la Yesu, pamoja na kupokea kipawa cha Roho wake Mtakatifu juu yako?. Kama bado ni vyema ukafanya hivyo maadamu bado unayo nafasi…

Kumbuka hii ni neema ya kipekee sana tuliyopewa…haitadumu milele..

Waebrania 10:28  “Mtu aliyeidharau sheria ya Musa hufa pasipo huruma, kwa neno la mashahidi wawili au watatu.

29  Mwaonaje? HAIKUMPASA ADHABU ILIYO KUBWA ZAIDI MTU YULE ALIYEMKANYAGA MWANA WA MUNGU, NA KUIHESABU DAMU YA AGANO ALIYOTAKASWA KWAYO KUWA NI KITU OVYO, na kumfanyia jeuri Roho wa neema?”

Na pia…

Waebrania 2:3  “sisi je! Tutapataje kupona, tusipojali wokovu mkuu namna hii? Ambao kwanza ulinenwa na Bwana, kisha ukathibitika kwetu na wale waliosikia;

4  Mungu naye akishuhudu pamoja nao kwa ishara na ajabu na nguvu za namna nyingi, na kwa magawanyo ya Roho Mtakatifu, kama alivyopenda mwenyewe”

Neema ni ipo, lakini haitadumu milele, tukiipuuzia… Bwana anatuita wote tuingie zizini mwake, ni heri tukaingia, lakini tukiipuzia na kuidharau neema, siku moja mlango utafungwa na hautafunguliwa tena..

Maran atha!

Tafadhali washirikishe na wengine habari hizi njema,

Kwa maombezi/Ratiba za ibada/ Ushauri/ Maswali.
Piga namba hizi: +255693036618 au +255789001312

pia kama utapenda uyapate mafundisho haya kwa njia ya Whatsapp au email basi tutumie ujumbe kwenye namba hizo hizo.


Mada Nyinginezo:

TUMEFANYIKA KUWA WANA WA MUNGU!

UTAKASO NI SEHEMU YA MAISHA YA MKRISTO YA KILA SIKU.

WAKAMCHA BWANA, NA KUITUMIKIA MIUNGU YAO WENYEWE.

LAKINI NINYI, NDUGU, MSIKATE TAMAA KATIKA KUTENDA MEMA.

SIKUKUU 7 ZA KIYAHUDI ZINAFUNUA NINI KWETU?

Rudi nyumbani

Print this post

About the author

Admin administrator

Subscribe
Notify of
guest
1 Comment
Newest
Oldest Most Voted
Inline Feedbacks
View all comments
Ernest Athanas
Ernest Athanas
2 years ago

AMINA. Mungu akubariki na aibariki huduma ya Injili unayoihubiri kwa njia ya internet, na ikawe sababu ya kufunguliwa vifungo vya walio wengi.