NIMEAZIMIA KUWAKUSANYA MATAIFA. NIPATE KUWAMWAGIA GHADHABU YANGU

by Admin | 10 October 2022 08:46 pm10

Sefania 3:8 “Basi ningojeni, asema Bwana, hata siku ile nitakapoondoka kuteka mateka; maana nimeazimia kuwakusanya mataifa, ili nizikutanishe falme, nipate kuwamwagia ghadhabu yangu; naam, ukali wote wa hasira yangu; kwa maana dunia yote itateketezwa kwa moto wa wivu wangu”.

Majira yaliyopo mbele yetu, si rafiki kabisa ndugu yangu, bali ni majira ya vita. Fahamu kuwa hii dunia haitaisha katika amani..Vipo vita vikubwa na vibaya vinavyokuja mbele yetu… Hilo haliepukiki kwasababu biblia ilishatabiri. Na sasa zipo vita kuu mbili(2), ambazo zitapiganwa kinyume na Mungu kabla ya huu ulimwengu kuisha..

Tukisema ‘kinyume na Mungu’ Tunamaanisha kinyume na Israeli, kwasababu Mungu yupo katika taifa lake Israeli..Ndilo taifa pekee Mungu aliloliunda kwa lengo la kuyabariki mataifa na pia kwa lengo la kuyakomesha mataifa.

Vita ya kwanza itakuwa ni ile tunayoisoma katika kitabu cha Ezekieli 38&40, Hii itapiganwa kipindi kifupi sana kabla ya unyakuo, au kipindi kifupi sana baada ya unyakuo. Kwaufupi ni kwamba taifa hili la Urusi, ndilo litakalosimama kama kichwa cha vita hiyo, likiyaongoza na mataifa mengine machache ya kando kando ,lakini litapigwa na habari yao itakuwa imeishia hapo. Ikiwa utataka kupata maelezo zaidi kuhusiana na  vita hii tutumie ujumbe inbox (+255693036618 / +255789001312), tukutumie somo lake.

Lakini vita nyingine, ni vita ijulikanayo kama vita ya Harmagedoni.. Hii haitakuwa tena ya mataifa machache tu..Hapana, bali itahusisha mataifa yote duniani. Yataungana, yakiwa na lengo moja la kuifuta Israeli katika uso wa dunia..Na sababu ambayo itapelekea ni kwamba Mungu ataitumia Israeli, kuyaudhi mataifa haya..aidha kwa kupitia manabii atakaowanyanyua, au kwa kupitia watawala watakaokuwepo. Na itapiganwa mwishoni kabisa mwa ulimwengu.

Zekaria 12:2 “Angalia, mimi nitafanya Yerusalemu kuwa kikombe cha kuyumba-yumba kwa watu wa kabila zote, wazungukao pande zote; tena kitakuwa juu ya Yuda pia wakati wa kuhusuriwa Yerusalemu.

3 Tena itakuwa siku hiyo, nitafanya Yerusalemu kuwa jiwe la kuwalemea watu wa kabila zote; wote watakaojitwika jiwe hilo watapata jeraha nyingi; na mataifa yote ya dunia watakusanyika pamoja juu yake”.

Hata taifa lako unaloishi wewe  litahusika wakati huo, watakuwa wamejiandaa na mabomu yao ya nyuklia na majeshi, ili kwenda kuisambaratisha nchi ile ndogo. Wakati huo Israeli wakiwa wanyonge, na wamezingirwa na majeshi, Ndipo Kristo mkombozi wao atakapotokea mawinguni. Na atashuka katika ule mlima wa Mizeituni, na kuanzia hapo, atafanya vita ya kuyateketeza mataifa yote ulimwenguni..halitasalia hata moja litakalokosa kunywa kikombe hicho cha ghadhabu ya Mungu.

Pitia kwa utulivu maandiko haya;

Ufunuo 19:11 “Kisha nikaziona mbingu zimefunuka, na tazama, farasi mweupe, na yeye aliyempanda, aitwaye Mwaminifu na Wa-kweli, naye kwa haki ahukumu na kufanya vita.

12 Na macho yake yalikuwa kama mwali wa moto, na juu ya kichwa chake vilemba vingi; naye ana jina lililoandikwa, asilolijua mtu ila yeye mwenyewe.

13 Naye amevikwa vazi lililochovywa katika damu, na jina lake aitwa, Neno la Mungu.

14 Na majeshi yaliyo mbinguni wakamfuata, wamepanda farasi weupe na kuvikwa kitani nzuri, nyeupe, safi.

15 Na upanga mkali hutoka kinywani mwake ili awapige mataifa kwa huo. Naye atawachunga kwa fimbo ya chuma, naye anakanyaga shinikizo la mvinyo ya ghadhabu ya hasira ya Mungu Mwenyezi.

16 Naye ana jina limeandikwa katika vazi lake na paja lake, MFALME WA WAFALME, NA Bwana WA MABwana.

17 Kisha nikaona malaika mmoja amesimama katika jua; akalia kwa sauti kuu, akiwaambia ndege wote warukao katikati ya mbingu, Njoni mkutane kwa karamu ya Mungu iliyo kuu;

18 mpate kula nyama ya wafalme, na nyama ya majemadari, na nyama ya watu hodari, na nyama ya farasi na ya watu wawapandao, na nyama ya watu wote, waungwana kwa watumwa, wadogo kwa wakubwa.

19 Kisha nikamwona huyo mnyama, na wafalme wa nchi, na majeshi yao, wamekutana kufanya vita na yeye aketiye juu ya farasi yule, tena na majeshi yake”.

Pitia tena hili andiko, uone Kristo atakavyoshuka juu ya mlima wa mizeituni na kuanza maangamizi kwa watu waovu.

Zekaria 14:2 “Kwa maana nitawakusanya mataifa yote walete vita juu ya Yerusalemu; na huo mji utapigwa, nazo nyumba zitatekwa, nao wanawake watatendwa jeuri; na nusu ya watu wa mji watatoka kwenda utumwani; ila mabaki ya watu wa mji hawatakatiliwa mbali.

3 Hapo ndipo atakapotokea Bwana, naye atapigana na mataifa hayo, kama vile alipopigana zamani siku ya vita.

4 Na siku hiyo miguu yake itasimama juu ya mlima wa Mizeituni, unaoelekea Yerusalemu upande wa mashariki, nao mlima wa Mizeituni utapasuka katikati yake, upande wa mashariki na upande wa magharibi; litakuwako huko bonde kubwa sana; na nusu ya mlima ule utaondoka kwenda upande wa kaskazini, na nusu yake itaondoka kwenda upande wa kusini”.

Hapa ndipo utakapokuwa mwisho wa mataifa yote ulimwenguni.

Leo hii umeshaanza kuona ni jinsi gani, dunia inavyopata shida kwa taifa la Israeli?. Taifa hili kwasasa lina maadui wengi kuliko marafiki, limeshaonekana kama taifa asi la dunia. Na hapo Bwana hajalirudia taifa hili. Utafika wakati, hii neema itaisha kwetu sisi mataifa, ndipo watakapogeukiwa wao, na watatubu, kwa makosa waliyoyafanya ya kumsulubisha Bwana wao..

Soma..

Zekaria 12:9 “Hata itakuwa siku hiyo, ya kwamba nitatafuta kuwaangamiza mataifa yote watakaokuja kupigana na Yerusalemu.

10 Nami nitawamwagia watu wa nyumba ya Daudi, na wenyeji wa Yerusalemu, roho ya neema na kuomba; NAO WATAMTAZAMA YEYE AMBAYE WALIMCHOMA; nao watamwombolezea, kama vile mtu amwombolezeavyo mwanawe wa pekee; nao wataona uchungu kwa ajili yake, kama vile mtu aonavyo uchungu kwa ajili ya mzaliwa wake wa kwanza.

11 Siku hiyo kutakuwa na maombolezo makuu huko Yerusalemu, kama maombolezo ya Hadadrimoni katika bonde la Megido.

12 Nayo nchi itaomboleza, kila jamaa peke yake; jamaa ya nyumba ya Daudi peke yao, na wake zao peke yao; jamaa ya nyumba ya Nathani peke yao, na wake zao peke yao;

13 jamaa ya nyumba ya Lawi peke yao, na wake zao peke yao; jamaa ya nyumba ya Shimei peke yao, na wake zao peke yao.

14 Jamaa zote zilizosalia, kila jamaa peke yake, na wake zao peke yao”.

Ndugu, Wakati huu upo karibuni kutokea.. Je! Umejipangaje/Tumejipangaje? Neema ndio tunaiaga hivyo? Inawarudia wayahudi, ilipoanzia.. kama wewe unasubiri kila siku kupigiwa kelele za injili utubu..Fahamu kuwa zama hizo zimeshaisha..jicho la Mungu linaanza kurudi Israeli sasa.. Na siku sio nyingi, UNYAKUO, utapita, watakaobakia ndio watakaoshuhudia hayo yote. Lakini tuliokoka tutakuwa mbinguni kwenye karamu ya mwanakondoo.

Tubu leo mpe Yesu maisha yako, ukabatizwe katika ubatizo sahihi, na kupokea Roho Mtakatifu. Huu  Ulimwengu si rafiki, yasalimishe maisha yako kwa Bwana.

Maran Atha.

Tafadhali shea na wengine ujumbe huu;

Pia Kwa maombezi/ Ushauri/ Maswali/ Whatsapp:
Tuandikie katika BOXI la Maoni hapo chini au
Piga namba hizi: +255693036618 au +255789001312

Mada Nyinginezo:

WATAMTAZAMA YEYE AMBAYE WALIMCHOMA; NAO WATAMWOMBOLEZEA.

UTAWALA WA MIAKA 1000.

Nini maana ya ombeni kukimbia kwenu kusiwe wakati wa baridi wala siku ya sabato?.

MAPIGO YA VITASA SABA, NA SIKU YA BWANA.

SIKU YA UNYAKUO ITAKUKUTAJE?

HATARI! HATARI! HATARI!

Rudi nyumbani

DOWNLOAD PDF
WhatsApp

Source URL: https://wingulamashahidi.org/2022/10/10/nimeazimia-kuwakusanya-mataifa-nipate/