Kuharimishwa ni nini, na kwanini Paulo aombe hivyo?(Warumi 9:2).

by Admin | 8 January 2024 08:46 pm01

Jibu: Ili tuweze kuelewa vizuri tuanzia ule mstari wa kwanza, na tusome mpaka ule wa 5

Warumi 9:1  “Nasema kweli katika Kristo, sisemi uongo, dhamiri yangu ikinishuhudia katika Roho Mtakatifu,

2  ya kwamba nina huzuni nyingi na maumivu yasiyokoma moyoni mwangu.

3  Kwa maana ningeweza kuomba MIMI MWENYEWE NIHARIMISHWE NA KUTENGWA NA KRISTO KWA AJILI YA NDUGU ZANGU, JAMAA ZANGU KWA JINSI YA MWILI;

4  ambao ni Waisraeli, wenye kule kufanywa wana, na ule utukufu, na maagano, na kupewa torati, na ibada ya Mungu, na ahadi zake;

5  ambao mababu ni wao, na katika hao alitoka Kristo kwa jinsi ya mwili. Ndiye aliye juu ya mambo yote, Mungu, mwenye kuhimidiwa milele. Amina”

“Kuharimishwa” maana yake ni “kutengwa mbali na mtu/kitu (kwa ufupi kufanywa haramu)”.

Paulo aliomba kama ingewezekana Aharamishwe kwaajii ya ndugu zake katika mwili (yaani waisraeli), ili waokolewe.

Sasa kwanini aliomba vile, na je jambo hilo linawezekana?

Awali ya yote ili tuelewe vizuri hebu tuweke msingi kwanza kwa kuelewa agenda ya Wokovu ulioletwa na YESU KRISTO.

Wokovu kwamba ulianzia kwa Wayahudi, (soma Yohana 4:22) na baadaye ukahamia kwa watu wa mataifa.

Na kipindi Wokovu (injili) inahubiriwa kwa wayahudi, sisi watu wa mataifa tulikuwa tumeharimishwa, maana yake tulikuwa tumetengwa mbali na injili/neema, na kufanyika watu tusiostahili..

Waefeso 2:11 “Kwa ajili ya hayo kumbukeni ya kwamba zamani ninyi, mlio watu wa Mataifa kwa jinsi ya mwili, mnaoitwa Wasiotahiriwa na wale wanaoitwa Waliotahiriwa, yaani, tohara ya mwilini iliyofanyika kwa mikono;

12  kwamba zamani zile mlikuwa hamna Kristo, MMEFARAKANA NA JAMII YA ISRAELI, wageni wasio wa maagano ya ahadi ile. MLIKUWA HAMNA TUMAINI, HAMNA MUNGU DUNIANI”

Umeona?..kumbe kuna wakati sisi watu wa mataifa hatukuwa na Mungu (neema),Na wakati ulipofika waisraeli (wayahudi) walipomkataa Masihi YESU KRISTO, na kusema yeye siye yule aliyetabiriwa, Ndipo Ikafanya Neema iondoke kwao na kuja kwetu sisi watu wa mataifa, hivyo nao pia WAKAHARIMISHWA ili sisi tupate Neema..

Sasa Utauliza hilo tunalithibitisha vipi kimaandiko..

Warumi 11:30 “ KWA MAANA KAMA NINYI ZAMANI MLIVYOMWASI MUNGU, LAKINI SASA MMEPATA REHEMA KWA KUASI KWAO”

31  KADHALIKA NA HAO WAMEASI SASA, ILI KWA KUPATA REHEMA KWENU WAO NAO WAPATE REHEMA.

Soma pia  Matendo 28:28 na Matendo 13:46,utaona jambo hilo Zaidi.

Sasa Mtume Paulo kwa kulijua hilo kwamba “Neema imewaondokea Wayahudi wengi” na imeenda kwa watu wa MATAIFA, kwa mantiki hiyo hiyo akatamani kama ingewezekana IONDOKE kwake (yaani aharimishwe), ili irudi tena kwa WAISRAELI ndugu zake wapate kuokolewa.

Na neema ikiondoka juu ya mtu/watu maana yake ile nguvu ya kumwamini KRISTO inakuwa haipo tena!, kila kitu kumhusu YESU ni upumbavu kwa mtu huyo au watu hao, (Mfano wa PAULO alivyokuwa kabla ya kuokoka..alikuwa anaona injili ni upuuzi na Zaidi sana alikuwa anawaua wafuasi wa BWANA YESU). (Hiyo yote ni kutokana na neema kutokuwepo juu yake).

Sasa swali ni je! Jambo hilo aliloliomba Paulo linawezekana?..yaani Mungu anaweza kumharimisha yeye ili ndugu zake wapone?

Jibu ni LA! Ni jambo ambalo haliwezekani,..Paulo alisema vile kutokana na huruma na upendo kwa ndugu zake!..Ni sawa na mtu aliye mzima, aone ndugu yake anateseka na ugonjwa mbaya..na aombe ahamishiwe yale maumivu kwake kutokana na kumhurumia yule mgonjwa, na ndivyo Paulo alichokuwa anakiomba.

Kadhalika Mungu hawezi kuihamisha Neema aliyokupa na kuipeleka kwa mtu mwingine kwa wewe kumwomba...(hawezi kukupokonya uzima wa milele ikiwa umestahili uzima wa milele) Neema huwa inaondoka kutoka kwa mtu kwa njia ya matendo yake(kama matendo yake yakiwa hayafai, lakini si kwa kumwomba Mungu aihamishe kutoka kwako.

Je umeokoka?..kama bado unasubiri nini?

Fahamu kuwa tunaishi siku za mwisho na BWANA YESU yupo mlangoni.

Bwana akubariki.

Tafadhali shea na wengine ujumbe huu;

Pia Kwa maombezi/ Ushauri/ Maswali/ Whatsapp:
Tuandikie katika BOXI la Maoni hapo chini au
Piga namba hizi: +255789001312 au +255693036618

Mafundisho mengine:

MPAKA UTIMILIFU WA MATAIFA UTAKAPOWASILI.

JINSI YA KUITUMIA VYEMA NEEMA YA MUNGU ILIYO JUU YANGU.

SI KWA MATENDO BALI NEEMA.

MAMBO YATAKAYOTOKEA ISRAELI SIKU ZA HIVI KARIBUNI.

Je mwanamke anaruhusiwa kupanda madhabahuni akiwa katika siku zake?

Rudi nyumbani

DOWNLOAD PDF
WhatsApp

Source URL: https://wingulamashahidi.org/2024/01/08/kuharimishwa-ni-nini-na-kwanini-paulo-aombe-hivyowarumi-92/