KIFUNGO CHA MWAMINI KIPO WAPI?

by Admin | 8 April 2024 08:46 pm04

Unaweza kuuliza je! Mwamini anaweza kufungwa na adui?. Jibu ni ndio anaweza kufungwa. Utauliza tena, kama anafungwa sasa kazi ya Yesu msalabani ilikuwa ni nini ikiwa hajawekwa huru kweli kweli.

Jibu ni kwamba mwamini yeyote, hawezi kuwa na kifungo katika roho yake, yaani hawezi kufungwa roho aidha na mapepo, au wanadamu au chochote kile. Hawezi kuwa na laana yoyote ndani yake, aidha ya ukoo au ya mabibi. Kwasababu yeye ni mbarikiwa amewekwa huru na Yesu, na ndio kazi Yesu aliyokuja kuifanya kuwaweka huru walioonewa na ibilisi.Hivyo mtu yeyote aliyemwamini Yesu kwa ‘TOBA’, ubatizo na kupokea Roho. Huyo hana kifungo chochote kwasababu uhai wake unakuwa umefichwa ndani ya Kristo.

Lakini Shetani anauwezo wa kumzuia, katika mambo mengi, asipojua ni nini anapaswa afanye. Na hicho ndicho kifungo cha nje akifanyacho adui. Kukuzuia wewe mwamini, ndicho alichokifanya kwa Paulo wakati Fulani alipotaka kwenda kuhubiri  injili kwa Wathesalonike akasema shetani alinizuia (1Wathesalonike 2:8).

Lakini pia tunamwona Mtume mwingine aliyeitwa Petro.

sasa hebu tuangalie kisa hiki kwenye maandiko Kilichomhusu yeye, tuone ni maeneo gani huwa adui analenga mahususi.

Matendo 12:4  Alipokwisha kumkamata, akamweka gerezani akamtia mikononi mwa vikosi vinne vya askari wanne wanne, wamlinde, akitaka baada ya Pasaka kumtoa na kumweka mbele ya watu.

5  Basi Petro akalindwa gerezani, nalo kanisa likamwomba Mungu kwa juhudi kwa ajili yake.

6  Hata wakati Herode alipotaka kumtoa, usiku ule ule Petro alikuwa analala katikati ya askari wawili, amefungwa minyororo miwili; walinzi mbele ya mlango wakalilinda gereza.

7  Mara malaika wa Bwana akasimama karibu naye, nuru ikamulika kule chumbani, akampiga Petro ubavuni, akamwamsha, akisema, Ondoka upesi. MINYORORO YAKE IKAMWANGUKA MIKONONI.

8  Malaika akamwambia, Jifunge, KAVAE VIATU VYAKO. Akafanya hivyo. Kisha akamwambia, JIVIKE NGUO YAKO, ukanifuate.

9  Akatoka nje, akamfuata; wala hakujua ya kuwa ni kweli yaliyofanywa na malaika; bali alidhani kwamba anaona maono.

Umeona maeneo aliyofungwa Petro?

Wafungwa wa zamani, ilikuwa ili aitwe mfungwa, ni lazima mambo hayo matatu  yakamilishwe juu yake; nayo ni.

1) Kufungwa, Minyororo mikononi

2)Kuondolewa Mavazi, na kupewa mengine ya gerezani.

3)Kuondolewa viatu miguuni

Na hiki ndicho kitu anachokifanya  pia adui kwa mwamini. Anaanza kwa kukufunga mikono yako rohoni, kisha kuyaondoa mavazi yako, na mwisho viatu vyako miguuni. Baada ya hapo unakuwa tayari huna nguvu ya kumshinda.

Mikono ni nini?

Ni “maombi na mifungo”

Mikono ni viungo mama katika mwili. Husaidia viungo vingi kufanya shughuli zake. Silaha hushikwa na mikono,  hata ngumi hurushwa kwa mikono. Hivyo adui anajua akizuia mikono yako. Huwezi kufanya lolote. Mikono ya mwamini, ni “maombi na mifungo”.

Mtu ambaye ni mwombaji, kiwango cha Roho ndani yake huwa ni kikubwa, na hivyo hakuna mnyororo wowote, unaoweza kumshika. Ndio maana utaona baada ya kanisa kumwombea Petro kwa juhudi, akafunguliwa. Vilevile Paulo na Sila walipokuwa wamefungwa kipindi kile, hawakulala tu, bali usiku wa manane walikuwa wakiomba, na matokeo yake vifungo vikawaachia.

Matendo 16:25  Lakini panapo usiku wa manane Paulo na Sila walikuwa wakimwomba Mungu na kumwimbia nyimbo za kumsifu, na wafungwa wengine walikuwa wakiwasikiliza. 26  Ghafla pakawa tetemeko kuu la nchi, hata misingi ya gereza ikatikisika, na mara hiyo milango ikafunguka, vifungo vya wote vikalegezwa.

Umeona, maombi, huondoa minyororo mikononi. Kuwa mwombaji, uzishinde nguvu za mwovu. Shetani anawaogopa waombaji

Mavazi ni nini?

Ufunuo 19:8  Naye amepewa kuvikwa kitani nzuri, ing’arayo, safi; kwa maana kitani nzuri hiyo ni matendo ya haki ya watakatifu

Mavazi, ni matendo mema. Ukikosa matendo mema,(Utakatifu), si rahisi kumshinda adui, utakuwa mwamini asiye na matunda yoyote, itaishi tu kama mwanadamu ambaye anamapungufu ya akili rohoni, hutaweza kufanya lolote.Ndani una makunyanzi, mawaa, ambazo katika hizo shetani anakuwa na haki ya kukulaumu.

Ishi kama mkristo, ukiwa rafiki wa dunia, fahamu kuwa unajifanya adui kwa Mungu moja kwa moja. Nuru yako isipoangaza nje, huwezi mshinda shetani. Ni lazima uwe kikombe safi, nje na ndani. Huwezi kusema umeokoka halafu matendo yako hayaendani na imani yako.Unajidanganya, bado hujaifahamu neema ya Mungu.

Miguu ni nini?

Waefeso 6:14  Basi simameni, hali mmejifunga kweli viunoni, na kuvaa dirii ya haki kifuani, 15  na kufungiwa miguu utayari tupatao kwa Injili ya amani.

Miguu ni utayari, wa kuhubiri. Adui anapenda kukawiisha nia za watu, kwa kuwavuta katika mambo yao mengine, na kusahau yaliyo ya msingi kwao, ndio hapo atawasonga kwa anasa, udanganyifu wa mali, na shughuli za ulimwengu huu. Na mwisho wa hapo wanabakia kuwa hawana matunda.

Hivyo ndugu uliyeokoka, usiruhusu adui kukuzuia popote. Jijengee desturi ya kuwa mwombaji wa kila siku. Mikono yako isifungwe. Penda kuishi maisha matakatifu, vazi lako lisibadilishwe, kuwa tayari kuhubiri injili wakati wowote, ukifaao na usiokufaa, epuka udhuru wa mwili au kazi, pinga sana hapo jiwekee ratiba yako, ili upate sehemu ya kuwaeleza wengine habari za Yesu Kristo anayewaokoa wanadamu.

Tukizingatia hayo. Tutakuwa tumemshinda shetani ndani na nje. Hatujafungwa ndani wala nje.

Bwana akubariki

Shalom.

Washirikishe na wengine habari hizi njema kwa kushea

Ikiwa utapenda kupata msaada wa kumpokea Yesu maishani mwako bure, Basi wasiliana nasi kwa namba uzionazo chini ya makala hii.

Pia kwa kupokea mafundisho ya kila siku kwa njia ya WHATSAPP, jiunge na channel yetu kwa kupofya link hii >> https://whatsapp.com/channel/0029VaBVhuA3WHTbKoz8jx1

Kwa mawasiliano: +255789001312 au +255693036618

Bwana akubariki.

Mafundisho mengine:

Biblia inapotumia neno “Bila kazi ya mikono”, ina maana gani?

Kongwa ni nini kwenye biblia?(Wagalatia 5:1)

VITA DHIDI YA MAADUI

MLANGO MWINGINE WA ADUI KUTULETEA MAJARIBU.

Rudi Nyumbani

DOWNLOAD PDF
WhatsApp

Source URL: https://wingulamashahidi.org/2024/04/08/kifungo-cha-mwamini-kipo-wapi/