Nini maana ya hekima ya maskini haisikilizwi? (Mhubiri 9:16)

by Admin | 26 July 2024 08:46 am07

Swali: Katika Mhubiri 9:16, neno la Mungu linasema kuwa hekima ya maskini haisikilizwi, je na sisi tunapaswa tusizisikilize hekima/mashauri ya watu wasio na kitu, ili kujinusuru..au andiko lina maana gani?


Jibu: Turejee..

Mhubiri 9:16 “Ndipo niliposema, Bora hekima kuliko nguvu; WALAKINI HEKIMA YA MASKINI HUDHARAULIWA, WALA MANENO YAKE HAYASIKILIZWI”.

Tukiusoma huo mstari peke yake ni rahisi kuona au kujifunza kuwa “hatupaswi kusikiliza watu maskini” hususani wanapopendekeza mambo.. (na watu maskini ni pamoja na kundi la watu wasio na elimu kabisa).. Lakini hebu tuanzie ule mstari wa 13, tuone kama hiyo ndio maana yake.

Mhubiri 9:13 “Pia nimeona hekima chini ya jua, nayo ni kama hivi, tena kwangu mimi ilionekana kuwa ni neno kubwa.

14 Palikuwa na mji mdogo, na watu ndani yake walikuwa wachache; akaja mfalme mkuu juu yake, akauhusuru, akajenga ngome kubwa ili kuupiga.

15 BASI, KULIONEKANA HUMO MTU MASKINI MWENYE HEKIMA, naye kwa hekima yake akauokoa mji ule lakini hata hivyo hapakuwa na mtu ye yote aliyemkumbuka yule mtu maskini.

16 Ndipo niliposema, BORA HEKIMA KULIKO NGUVU; walakini hekima ya maskini hudharauliwa, wala maneno yake hayasikilizwi”.

Huyu Maskini alikuwa na Hekima ya kuuokoa mji, ijapokuwa hakuwa na elimu, wala ujuzi mwingi, pengine wala hakuwa katika siasa ya nchi, lakini alitoa wazo bora, na kufanya nchi isiingie katika vita. Lakini baada ya mji kuokoka na kuwa na Amani, hawakumkumbuka yule maskini kwa kumpa thawabu.

Hilo halikumshangaza sana Sulemani, lililomshangaza Zaidi ni kuona  kuwa “KWANINI HEKIMA ZA MASKINI HAZISIKILIZWI”.. na wakati hao wanazo hekima za kuweza hata kuunusuru mji usiangamie!!!, kama mfano wa huyo tuliyemsoma hapo juu.

Hilo likamshangaza sana Sulemani, na ushauri wake ni kwamba tuwatafute hao (maskini) na kujaribu kusikiliza mashauri yao na tusiwadharau kwani baadhi yao wamebeba vitu vikubwa…

Na ndipo akasema Bora kuwa na hekima kama huyu kijana maskini kuliko kuwa na nguvu (za kimwili na kifedha na kielimu) na kukosa hekima.

Mhubiri 9:16 “Ndipo niliposema, Bora hekima kuliko nguvu; WALAKINI HEKIMA YA MASKINI HUDHARAULIWA, WALA MANENO YAKE HAYASIKILIZWI”.

Hivyo kwa tafakari hiyo tutakuwa tumeshapata jibu kuwa sio kwamba Biblia inatufundisha kutowasikiliza maskini au kuwadharau…bali kinyume chake inatufundisha “tusiwe na dharau nao, kwani kwa sehemu moja, wapo baadhi wenye hekima hata za kuweza kuokoa Taifa, mfano wa huyo tuliyemsoma hapo juu”.

Hivyo ndugu usimdharau mtu ambaye unaona ni mnyonge kuliko wewe, ambaye unaona pengine hana mali kama ulizonazo wewe, au hana uwezo kama ulionao wewe, au hana elimu kama uliyo nayo wewe… Watu hao unaowadharau wewe baadhi yao wamebeba vitu vikubwa sana kwaajili yako, ambavyo vinaweza kukusaidia wewe au watu wako!.

Hivyo sikiliza watu wote, na chuja mambo yote. Si wote walio maskini ni wajinga, na pia si maskini wote wana hekima… vile vile si wote walio matajiri wanazo akili, wengi hawana akili wala hekima ingawa mbele za watu wanaweza kusifika..

Biblia inasema heri kijana maskini mwenye hekima, kuliko mfalme mzee halafu mpumbavu (Soma Mhubiri 4:13).

Hivyo hatuna budi kuwa watu wanyenyekevu daima na wenye kusikiliza.

Bwana atusidie.

Washirikishe na wengine habari hizi njema kwa kushea

Ikiwa utapenda kupata msaada wa kumpokea Yesu maishani mwako bure, Basi wasiliana nasi kwa namba uzionazo chini ya makala hii.

Pia kwa kupokea mafundisho ya kila siku kwa njia ya WHATSAPP, jiunge na channel yetu kwa kupofya link hii >> https://whatsapp.com/channel/0029VaBVhuA3WHTbKoz8jx10

Kwa mawasiliano: +255789001312 au +255693036618

Bwana akubariki.

Mafundisho mengine:

Heri walio maskini wa roho; Maana ufalme wa mbinguni ni wao.

JINSI MUNGU ATAKAVYOTOA THAWABU ZAKE, NA VIGEZO ATAKAVYOTUMIA. (Sehemu ya 1)

NGUVU YA HEKIMA NA AKILI

HEKIMA NI NINI? NA UFAHAMU UNAPATIKANA WAPI?

TOA HUDUMA ILIYO BORA.

Rudi Nyumbani

DOWNLOAD PDF
WhatsApp

Source URL: https://wingulamashahidi.org/2024/07/26/nini-maana-ya-hekima-ya-maskini-haisikilizwi-mhubiri-916/