Maandiko yanasema Eliya aliomba kwa bidii hadi akasimamisha mvua kunyesha kwa MUDA wa miaka 3 na nusu.(Yakobo5:17) Je! kuomba kwa bidii ni kuomba kwa namna gani?

by Admin | 2 September 2019 08:46 pm09

JIBU: Tusome:

Yakobo 5:17 “Eliya alikuwa mwanadamu mwenye tabia moja na sisi, akaomba kwa bidii mvua isinyeshe, na mvua haikunyesha juu ya nchi muda wa miaka mitatu na miezi sita.

18 Akaomba tena, mbingu zikatoa mvua, nayo nchi ikazaa matunda yake.” 

Kwakuwa habari hii inamzungumzia Eliya hivyo ili kuelewa vizuri hiyo bidii aliyokuwa nayo ni vizuri tukarejea kwenye tukio halisi lenyewe ili tuone ni jinsi gani aliomba. Sasa ukiangalia vizuri utaona biblia haijatoa maelezo mengi juu ya maombi aliyoyaomba siku ile alipozuia mvua. Inaonyesha tu Eliya akitokea kwenye tukio na kuzungumza maneno yale na kuondoka,

 1Wafalme 17:1 “Basi Eliya Mtishbi, wa wageni wa Gileadi, akamwambia Ahabu, Kama Bwana, Mungu wa Israeli, aishivyo, ambaye ninasimama mbele zake, hakutakuwa na umande wala mvua miaka hii, ila kwa neno langu.

2 Neno la Bwana likamjia, kusema,

3 Ondoka hapa, geuka, uende upande wa mashariki, ujifiche karibu na kijito cha Kerithi kinachokabili Yordani.

 Lakini siku ile anarudi, ili kuifungua tena mbingu kwa Neno la Mungu, tunaona halikuwa ni jambo la kutamka na kuondoka tu kuna vitu viliendelea pale embu Tusome:

1Wafalme 18:41 “Naye Eliya akamwambia Ahabu, Haya! Inuka, ule, unywe; kwani pana sauti ya mvua tele.

42 Basi Ahabu akainuka ili ale na kunywa. Naye Eliya akapanda juu mpaka kilele cha Karmeli; akasujudu kifudifudi, akainama uso mpaka magotini.

43 Akamwambia mtumishi wake, Kwea sasa, utazame upande wa bahari. Akakwea, akatazama, na kusema, Hakuna kitu. Naye akanena, Enenda tena mara saba.

44 Ikawa mara ya saba akasema, Tazama, wingu linatoka katika bahari, nalo ni dogo kama mkono wa mtu. Akanena, Enenda, umwambie Ahabu, Tandika, ushuke, mvua isikuzuie.

45 Ikawa, muda si muda, mbingu zikawa nyeusi kwa mawingu na upepo, ikanyesha mvua nyingi. Ahabu akapanda garini, akaenda zake Yezreeli.” 

Hapo unaweza ukajifunza mambo kadhaa, cha kwanza Eliya kabla hata hajamwomba Mungu, alishaamini kuwa mvua inakwenda kunyesha siku hiyo katika nchi, na ndio maana alikuwa na ujasiri wa kumwambia Mfalme Ahabu inuka unywe kwani pana sauti ya mvua tele.

Pili alipoonenda magotini sasa ili kumwomba Mungu jibu lake halikuja ndani ya wakati alioutazamia pengine aliomba lisaa la kwanza, akitazamia kabla hata hajamaliza juu kutakuwa kumeshafunga, lakini Yule mtumishi wake alipoenda alirudisha repoti kuwa juu hakuna dalili yoyote ya mvua kunyesha, lakini aliendelea kukaa uweponi mwa Bwana akimshukuru kwa matendo yake makuu, lisaa lingine likapita akamwambia mtumishi wake haya nenda katazame tena, akarudi akasema hakuna kitu, ikaendelea hivyo hivyo lisaa la tatu, la nne, mpaka lisaa la 7 pengine, akamwambia nenda katazame usichoke, ndipo Yule mtumishi wake akarudi akasema ninaona kawingu kadogo kama cha mkono wa mtoto mchanga, Ndipo Eliya alipoacha kuomba akijua kuwa tayari imekwisha kuwa..

Na kama ingetokea hakuna kitu chochote kilichotokea ni wazi kuwa angeendelea hivyo hivyo hata mara 20 au 50, au 100 kwa nguvu ile ile akijua kuwa Mungu ameshamsikia..Huko ndiko kuomba kwa BIDII ambapo hata sisi tunapashwa tuwe nako, Ni rahisi kumwamini Mungu tunapompelekea mahitaji yetu lakini kudumu uweponi Mwake hatuwezi pale tunapoona majibu yanachelewa kidogo, hayajaja ndani ya wakati tuliotuzamia..Tunaanza kumtilia Mungu mashaka pengine hajatusikia. Lakini tukiendelea kushikilia na kumwamini Mungu kuwa ameshatenda, hata kama itapita siku, wiki, mwezi, miaka, ukizidi kushikilia nakwambia milango yote itafunguka mbele yetu. Hivyo kwa ufupi kuomba kwa bidii kunakozungumziwa hapo ni Kukaza kumwamini Mungu mpaka majibu yanapotokea. 

Ubarikiwe sana.


Mada Nyinginezo:

ROHO YA ELIYA KATIKA AGANO JIPYA INATENDAJE KAZI?

UFUNUO: MLANGO WA 11

KUNA TOFAUTI GANI KATI YA SALA NA DUA?

NJIA SAHIHI YA KUFUNGA.

“WOKOVU WETU U KARIBU NASI KULIKO TULIPOANZA KUAMINI”

VITA DHIDI YA MAADUI

TUMEPEWA, SI KUMWAMINI TU KRISTO, ILA NA KUTESWA KWA AJILI YAKE;


Rudi Nyumbani:

DOWNLOAD PDF
WhatsApp

Source URL: https://wingulamashahidi.org/2019/09/02/maandiko-yanasema-eliya-aliomba-kwa-bidii-hadi-akasimamisha-mvua-kunyesha-kwa-muda-wa-miaka-3-na-nusu-yakobo517-je-kuomba-kwa-bidii-ni-kuomba-kwa-namna-gani/