NGUVU ILIYOPO KATIKA MAAMUZI.

by Admin | 16 December 2019 08:46 pm12

Nguvu iliyopo katika maamuzi.


Jina la Bwana wetu Yesu Kristo libarikiwe. Karibu tujikumbushe Biblia…

Leo kwa Neema za Bwana tutajikumbusha mambo ambayo tulishawahi kujifunza huko nyuma..Kwasababu biblia inatufundisha hivyo katika 2Petro 1:12-13, 2Petro 3:1-2, na 1Wakorintho 4:17.

Na leo tutajikumbusha jambo muhimu sana ambalo linatutatiza wengi…Na hilo si lingine Zaidi ya nguvu iliyopo katika maamuzi.

Nguvu za Mungu haziwezi kuzidi maamuzi yetu sisi…Tunapomtumikia Mungu hatumtumikii kama maroboti kwamba maroboti yanakuwa hayajitambui lakini yanapelekwa tu mahali ambapo yule anayetaka kuyapeleka yawepo…Maroboti hayana maamuzi

Lakini sisi Mungu wetu hatuumba hivyo wala hatutumikishi hivyo…Ametuumbia jambo linaloitwa maamuzi, na hivyo yeye au kiumbe chochote hakiwezi kuingilia maamuzi yetu…hata shetani hawezi!!…Sio kwamba hawezi kutufanya kuwa kama maroboti hapana uwezo huo anao…lakini hajapenda kutufanya hivyo..

Kwahiyo Mungu anapomvuta mtu kwake, ambaye amemkusudia uzima wa milele..anachofanya ni kumshawishi kwa kumpa kila sababu ya yeye kutubu…Anamfumbua macho na kuona hali aliyopo kwamba anakwenda kupotea kama asipochukua hatua hii au ile..Ni kama mtu mwingine wa pili yupo pembeni yake..anamshawishi afanye maamuzi Fulani…na endapo akikubali anakuwa anajiungamanisha na yule mtu…Lakini Roho Mtakatifu hafikii hatua ya kumteka mtu na kumfanya mateka..

Wengi wanaomba Mungu awazuie wasifanye uasherati kwa lazima…Hicho kitu hakipo!..Roho Mtakatifu ni msaidizi sio mfanyaji…Wafanyaji ni sisi, yeye ni msaidizi tu…Unapomfuata Kristo unatakiwa kwanza wewe binafsi kuutii ushauri wa Roho Mtakatifu wa kuacha uasherati…Ukishaamua wewe kutii kwa kuacha yeye anakuja hapo kukusaidia…Kwahiyo ukichukua maamuzi yako ukajumlisha na msaada wake..Hapo kamwe uasherati hautakushinda….

Kadhalika huwezi kumwomba Mungu akuachishe pombe au sigara kwa lazima…Kwamba utokee tu umeacha sigara au umeacha pombe…Nataka nikuambie Roho Mtakatifu hatendi kazi namna hiyo…Kama unataka kuacha pombe ambazo zimekufanya mtumwa kwa muda mrefu…Hatua ya kwanza ni wewe kumtii Roho Mtakatifu ambaye yupo pembeni yako anayekuambia uache pombe….hivyo mtii kwa kwenda kuvunja hizo chupa za bia zilizopo nyumbani kwako…kwa kuacha kwenda Bar, kwa kuacha kutembea na kampani za wanywaji pombe na kwa kuacha kabisa kunywa pombe…Ukishaamua kwa vitendo kama hivyo…

Basi yule msaidizi aliyeko pembeni yako, anakusaidia kushinda tamaa ya kunywa tena pombe anakuongezea nguvu …Lakini usipoamua…Miaka na miaka itapita utabakia hivyo hivyo,..utahudhuriwa kanisani, utawekewa mikono na kila aina ya mtumishi, lakini hakuna kitakachotokea.

Ni kwanini?..Ni kwasababu Nguvu za Roho Mtakatifu haziwezi zikazidi nguvu za maamuzi yako.

Na ndio maana Bwana Yesu anajulikana pia kama Mshauri wa Ajabu..

Isaya 9:6 “Maana kwa ajili yetu mtoto amezaliwa, Tumepewa mtoto mwanamume; Na uweza wa kifalme utakuwa begani mwake; Naye ataitwa jina lake, Mshauri wa ajabu, Mungu mwenye nguvu, Baba wa milele, Mfalme wa amani”.

Mshauri ni mtu ambaye haingilii maamuzi yako lakini yupo karibu sana na mawazo yako kuyaboresha.

Kadhalika na uongo mwingine uliozagaa kila mahali ni wa watu kutenda dhambi na kusema ni shetani kawapitia…Ndugu usidanganyike hata kidogo kwa uongo huo!

Mtu anayekwenda kuzini..shetani hajampitia….kilichofanyika katika ulimwengu wa roho ni roho za mashetani zilitumwa kwa huyo mtu kumshawishi na kumpa kila sababu ya yeye kwenda kufanya uasherati…Ni kama mtu mwingine wa pembeni tena anamshawishi akafanye uasherati..atamkumbusha picha za ngono alizowahi kuziangalia, atamkumbusha uasherati wa mwisho aliowahi kuufanya na yule mtu atajaa tamaa na hivyo kwa maamuzi yake mwenyewe atanyanyuka na kwenda kutafuta kufanya kile kitendo…

Sasa huyo mtu hajashikwa na kufungwa na kupelekwa kwa lazima kufanya uasherati..la! bali kutokana na nguvu ya ushawishi iliyomshawishi na kuitii kwa hiari yake mwenyewe kaenda kufanya alichokifanya…Sasa huyu anaweza kujifariji ni shetani lakini hajui kwamba ni yeye ndiye kaamua kwenda kufanya..laiti angekataa kile kitu katika mawazo yake kamwe shetani asingeweza kumlazimisha…Kwasababu hakuna kiumbe chochote kilichoumbwa kinachoweza kuzidi maamuzi ya mtu!.nguvu iliyopo katika maamuzi ni kubwa sana.

Hivyo ndugu kama ulikuwa umekaa kwa muda mrefu huwezi kuacha kufanya masturbation..na ulikuwa unaamini kwamba ipo siku moja tu itatokea miujiza Mungu atakushukia na utaacha…nataka nikuambie ukweli…utasubiri hiyo siku miaka na miaka na haitafika!!!…Unachotakiwa kufanya ni leo leo kuamua kusema ninatubu dhambi zangu na kusema NIMEACHA!..na unaambatanisha vitendo juu yake kama dalili ya Imani yako…unafuta picha zote za ngono kwenye simu yako..unayazuia mawazo ya uasherati yajapo kichwani unayakataa..unakaa mbali na kitu chochote ambacho unajua ukikaa nacho dakika chache kitakupeleka katika mawazo ya uasherati…

Makala za kizinzi unaacha kuzisoma…magroup ya kizinzi unajiondoa, na ukikutana hata na post yoyote yenye maudhui ya kiuasherati unairuka huisomi…Vitabu na magazeti ya kiasherati unaacha kuyasoma…kuna magazeti ambayo kwa nje yanaonekana ni magazeti ya kimaadili ya kupunguza zinaa lakini ndani yake ndiyo yanayochochea zinaa kwa kasi kubwa…yana roho za usherati! Hivyo sio ya kusoma kabisa..mada mada na vikao vya mizaha unajitenga navyo…hata ukizungumza na mtu ukiona anaanza kwenda kwenye mada hizo unazikatisha…Lakini ukijiachia na kuendelea kusoma hayo magazeti, na Makala, na posti za mapenzi na magroup ya kiuasherati…pamoja na movie na matamthilia ya kidua yenye maudhui ya mapenzi…na huku unaamini kwamba siku moja nguvu za Roho Mtakatifu zitakushukia na kukuteka na utajikuta tu umeacha kwa lazima…nataka nikuambie usiangamie kwa kukosa maarifa!!..hiyo siku haitafika.

Walioacha hawakuacha kwa njia hiyo…walimtii Mungu kwanza ambaye anaugua ndani yao kuhusu dhambi zao..na baada ya kumtii wakaamua kuacha kwa vitendo..ikiwemo kujitenga na vishawishi vyote vya kiuasherati…Huko ndiko kujikana nafsi…Na mambo mengine yote ni hivyo hivyo..ukitaka kuacha usengenyaji ni hivyo hivyo, ukitaka kuacha wizi ni hivyo hivyo…ukitaka kuacha uchawi ni hivyo hivyo…unaamua kwanza binafsi kuacha na unakwenda kuchoma vibuyu vyote ulivyonavyo..na kufuta namba za waganga wa kienyeji..na kampani za marafiki wanaohudhuria huko.

Na baada ya kufanya hayo yote…Hakikisha unakwenda kukamilisha hatua za wokovu ikiwemo kubatizwa, kufanya ushirika na waaminio wenzako, na kudumu katika kujifunza Neno la Mungu kila siku.

Bwana akubariki sana.

Mada Nyinginezo:

JE! UMEBATIZWA UBATIZO SAHIHI?

SIKUJA KULETA AMANI DUNIANI, BALI MAFARAKANO.

ROHO HUTUOMBEA KWA KUUGUA KUSIKOWEZA KUTAMKWA!

BONDE LA KUKATA MANENO.

Ubatizo wa moto ni upi?

Rudi Nyumbani:

DOWNLOAD PDF
WhatsApp

Source URL: https://wingulamashahidi.org/2019/12/16/nguvu-iliyopo-katika-maamuzi/