TUNA WAJIBU WA KUOMBEANA KWA KINA.

by Admin | 29 April 2020 08:46 pm04

Jina la Bwana Yesu libarikiwe. Karibu tujifunze Neno la Mungu..

Biblia inasema..katika Yakobo 5:16

“Ungameni dhambi zenu ninyi kwa ninyi, na kuombeana, mpate kuponywa. Kuomba kwake mwenye haki kwafaa sana, akiomba kwa bidii”.

Maana yake ni kwamba tunapoombeana kuna neema ya ziada inashuka juu yetu…(Mungu anaachilia uponyaji)..Tunapomwomba Bwana atuhurumie sisi na kuwahurumia wengine, tunafungua wigo mpana wa Yule tunayemwombea kuponywa na kwetu sisi pia kuponywa pamoja na kufunika wingi wa dhambi..(Yakobo 5:20).

Hebu tukitafakari kile kisa cha Sodoma na Gomora…Kama wengi wetu tujuavyo kuwa kabla Mungu hajashusha moto kutoka mbinguni kuiteketeza miji ile..Mungu alimfunulia kwanza Ibrahimu makusudio yake hayo…lakini tunajua Ibrahimu kitu alichokifanya…japokuwa alikuwa anajua ni kweli Sodoma na Gomora kumeoza lakini hakuishitaki miji ile mbele za Mungu, na badala yake alitafuta njia ya kuiponya na ghadhabu ya Mungu…

Ndipo akaanza kwa kumwuliza Mungu kama watakuwepo wenye haki 50, je ataangamiza hao 50 pamoja na waovu…na kama tunavyojua Bwana alimwambia kama akikuta huko wenye haki 50 hataangamiza miji ile…lakini tunazidi kusoma Ibrahimu alimshusha Mungu idadi mpaka kufikia kwa wenye haki 10 kama watakuwepo…Lakini Mungu jibu lake lilikuwa ni lile lile…kwamba kama atakuta wenye haki 10 hataangamiza miji hiyo kwaajili ya hao wenye haki 10.(Mwanzo 18:23-33).

Lakini tunaona Ibrahimu aliishia idadi ya 10 tu!…Lakini hebu jiulize laiti angeendelea kidogo kuishusha ile idadi hadi tano na hata kufikia mmoja?..Labda pengine miji hiyo mpaka leo ingekuwepo…Kwasababu ndani ya miji ile alikuwepo mwenye haki mmoja LUTU.

Lakini kwasababu Ibrahimu hakulijua hilo, yeye alijua kwa namna yoyote ile mji mzima hauwezi ukakosa wenye haki 10, alijua watakuwepo wenye haki hata elfu…Hivyo aliachana na Mungu kwa amani kwasababu alijua Mungu huko aendako hawezi kukosa kabisa wenye haki 10, na hivyo miji ile itabaki salama tu, Hivyo Ibrahimu aliondoka akijua kuwa kwa maombi yale tayari kaiokoa Sodoma na Gomora…Lakini kumbe hakujua mwenye haki ni mmoja tu kule..ambaye ni ndugu yake aliyeitwa Lutu…Ndipo asubuhi anaamka na ghafla anaona upande wa mashariki moshi mkubwa unafuka juu!..kitendo hicho kilimuhuzunisha sana.

Lakini ni dhahiri kuwa laiti Ibrahimu angejua kuwa kuna mwenye haki mmoja tu ndani ya miji ile yote..asingemwacha Mungu bila kumwomba, wala asingeishia pale kwenye idadi ya watu kumi tu,…ni lazima angemshusha Mungu mpaka mtu mmoja na angezungumza na Mungu kwaajili ya huyo mwenye haki mmoja ili aunusuru mji wote, na suluhisho lingepatikana pale pale.

Tunachoweza kujifunza hapo ni kwamba ni lazima kuombeana sisi kwa sisi kwa kina, sio juu juu tu!..tusichukulie tu kwamba hali ni salama au shwari kwa ndugu zetu au kwa jamii ya watu wetu au kwa Taifa letu zima…Hali si shwari kama tunavyofikiri..Hivyo tusipoingia katika maombi ya kina ya kuomba rehema na Neema, uharibifu utashuka kwetu na kwa ndugu zetu ghafla.

Yakobo 5:16 “Ungameni dhambi zenu ninyi kwa ninyi, na kuombeana, mpate kuponywa. Kuomba kwake mwenye haki kwafaa sana, akiomba kwa bidii”.

Ayubu alikuwa ni mwenye haki lakini hakuacha kuwaombea wanawe, vivyo hivyo na sisi kama Kanisa la Kristo hatuna budi kuombeana sisi kwa sisi, wakati mwingine kwa kutajana majina,..Ili Mungu asiishie kutuponya sisi tu bali mpaka na jamii nzima.

Bwana atubariki na kutusaidia.

Mada Nyinginezo:

USIWE NA HAKI KUPITA KIASI.

NDUGU,TUOMBEENI.

FAIDA ZA MAOMBI.

CHUKIZO LA UHARIBIFU

CHAPA YA MNYAMA

Rudi Nyumbani:

DOWNLOAD PDF
WhatsApp

Source URL: https://wingulamashahidi.org/2020/04/29/tuna-wajibu-wa-kuombeana-kwa-kina/