BWANA AYAGANGE NA MACHO YETU PIA.

by Admin | 8 December 2020 08:46 pm12

Jina la Bwana wetu Yesu Kristo libarikiwe. Karibu tulitafakari Neno la Mungu pamoja, kwani ndicho chakula pekee kinachoweza kuziponya roho zetu kabisa kabisa.

Lipo swali tunaweza kujiuliza ni kwanini kuna wasaa ilimgharimu Bwana wetu kulia sana na kutoa machozi ? Tunajua alikuwa ni mkamilifu , alikuwa hana hofu na chochote, na lolote alilomwomba Mungu, dakika hiyo hiyo alipewa, lakini ni kwanini wakati mwingine ilimpasa atoe machozi mengi, na kulia ili apoke?

Kitabu cha Waebrania kinatuambia hivyo;

Waebrania 5:7 “Yeye, siku hizo za mwili wake, alimtolea yule, awezaye kumwokoa na kumtoa katika mauti, maombi na dua pamoja NA KULIA SANA NA MACHOZI, akasikilizwa kwa jinsi alivyokuwa mcha Mungu”;

Wakati  mwingine Bwana wetu Yesu alilia sana kama katoto kadogo, mbele za Mungu wake, alitoa machozi mengi, Yesu huyo ambaye leo hii  tunamwita Bwana wa Mabwana na Mfalme wa Wafalme, na kama hilo halitoshi tunamwita mwanaume wa wanaume.

Lakini mwanaume huyu alilia, alitoa machozi katika kumwomba Mungu wake, na kwasababu hiyo Mungu akamsikia, japokuwa hata asingefanya hivyo angesikiwa tu, lakini hisia zake zilizidi uwezo wake, na mamlaka yake, na nguvu zake..alipokuwa mbele za Baba yake machozi yalimtoka mwenyewe  tu, pale alipoutafakari uwezo wake jinsi ulivyo mkuu, yalimtoka mwenyewe alipoona Upendo wa Baba yake unavyozidi upeo, yalimtoka mwenyewe pale alipowahurumia watu aliopewa na Baba yake.

Jambo hilo halikuishia tu kwake, tunaona pia aliwaambukiza mpaka na mitume wake waliomtumikia baadaye..Kwa mfano utamwona Paulo wakati mwingi sio tu alilia katika kuomba bali hata alipokuwa anawahubiria watu alitoa machozi, kwa vile alivyokuwa anawahurumia roho zao.

Matendo 20:31 “Kwa hiyo kesheni, mkikumbuka ya kwamba miaka mitatu, usiku na mchana, sikuacha kumwonya kila mtu kwa machozi”.

Soma tena..

2Wakoritho 2:4 “Maana katika dhiki nyingi na taabu ya moyo niliwaandikia na machozi mengi; si kwamba mhuzunishwe, bali mpate kujua upendo wangu nilio nao kwenu jinsi ulivyo mwingi”.

Na…

Wafilipi 3:18 “Maana wengi huenenda, ambao nimewaambieni mara nyingi habari zao, na sasa nawaambia hata kwa machozi, kuwa ni adui za msalaba wa Kristo”;

Unaona hisia hizo nyingi za Paulo ndizo zilizochangia pia hata huduma yake duniani kuwa na mafanikio makubwa. Kwasababu aliyachukulia mambo ya Mungu kwa uzito mkubwa, aliithamini neema katika hisia za hali ya juu sana, ambazo zilimpelekea hata  kutoa machozi wakati mwingi alipokuwa anafanya kazi ya Mungu.

Na sisi pia, tuziamshe hisia zetu kwake. Mwingine anaweza kusema mimi siwezi! Ndio huwezi kulia kwasababu hujakaa chini na kuutafakari kwa makini uweza wake wote kwako, aliokufanyia tangu umekuja hapa duniani.

 Ungetafakari kwa undani ni kwanini Mungu amekupa uhai mpaka leo hii, na hujampa chochote, ni kwanini unavuta hewa yake bure, na hajawahi kukuchaji hata senti, ni kwanini umekuchagua wewe na kukupa wokovu na muda huo huo kuna wengine hawataki hata kusikia habari za mUNGU, ukidhani kwamba wewe kichwa chako ni chepesi sana kuelewa kuliko wale?, Hilo ondoa akilini, ni kwamba Mungu kachagua tu kukuvuta wewe kwake, hilo tu, huna cha ziada ulichomfanyia.  Ukikumbuka siku ile ulikuwa katika jaribu fulani akakuvusha, kama sio yeye ungekuwa ni marehemu sana.. Ukikumbuka hayo yote, hutabaki kama ulivyo,

Ukikumbuka ni  kwanini mwaka huu unakwisha, wewe hujafa na KORONA, wakati mamilioni ya watu wamekufa na bado wanaendelea kufa duniani leo hii.. nakwambia utabaki kama ulivyo.. utalia tu, na kutoa machozi kwa kumpa Mungu shukrani, kwa kulibariki jina lake.

Unapoumaliza huu mwaka, usizizuie hisia zako kwa Mungu. Huu ni mwaka ambao sote tunahitaji kumshukuru Mungu, kwa nguvu zaidi kuliko hata miaka mingine yote iliyowahi kututangulia.

“Mshukuruni Bwana kwa kuwa ni mwema; Kwa maana fadhili zake ni za milele”. (1Nyakati 16:34)

Mungu atujalie kulijua hilo, ayagange macho yetu.

Shalom.

Tafadhali washirikishe na wengine habari hizi njema, na pia kama utapenda tuwe tunakutumia mafundisho ya Neno la Mungu ya mara kwa mara kwa njia ya email yako au Whatsapp basi tutumie ujumbe kwenye namba hii +255693036618 au +255789001312 Jiunge na magroup yetu ya whatsapp kwa kubofya hapa > WHATSAPP-Group

Mada Nyinginezo:

 Rudi nyumbani

DOWNLOAD PDF
WhatsApp

Source URL: https://wingulamashahidi.org/2020/12/08/bwana-ayagange-na-macho-yetu-pia/