NI KIPI KINAMZUIA MUNGU KUZUNGUMZA NA SISI?

by Admin | 29 August 2021 08:46 pm08

Jina la Bwana na mwokozi wetu Yesu Kristo libarikiwe, yapo mambo mengi yanayozuia Mungu kuzungumza na sisi katika maisha yetu, lakini leo tutalizungumzia jambo moja kuu linalosababisha Bwana apunguze kusema na sisi, au aache kusema na sisi kabisa.

Na jambo lenyewe ni tabia ya “KUJIFANYA HUJUI NA WAKATI UNAJUA”. Hii ni tabia moja iliyo ya hatari sana ambayo ina madhara makubwa sana kwa mtu. Unapojua jambo Fulani halafu unajifanya hujui, na wakati huo huo unakwenda kumuuliza Mungu, au kumwomba!, ni jambo linalosababisha Mungu kukaa kimya mbele yako.

Hebu tusome kisa kimoja katika biblia ambacho kitatusaidia kuelewa vyema..

Marko 11:27  “Wakafika Yerusalemu tena; hata alipokuwa akitembea hekaluni, walimwendea wakuu wa makuhani, na waandishi, na wazee,

28  wakamwambia, Ni kwa mamlaka gani unatenda mambo haya? Naye ni nani aliyekupa mamlaka hii uyatende haya?

29  Yesu akawaambia, Nitawauliza neno moja, nanyi mnijibu, kisha nitawaambia ni kwa mamlaka gani nayatenda haya.

30  Ubatizo wa Yohana ulitoka mbinguni, au kwa wanadamu? Nijibuni.

31  Wakasemezana wao kwa wao, wakisema, Kama tukisema, Ulitoka mbinguni, atasema, Mbona, basi, hamkumwamini?

32  Ila tukisema, Ulitoka kwa wanadamu, waliogopa watu; maana watu wote walimwona Yohana kuwa nabii halisi.

33  Wakamjibu Yesu, wakasema, Hatujui. Yesu akawaambia, WALA MIMI SIWAAMBII NINYI NI KWA MAMLAKA GANI NAYATENDA HAYA”

Nataka tuangalie hicho kipengele cha mwisho, Bwana anakataa kuwaambia ni kwa mamlaka gani anatenda hayo.

Sasa swali la kujiuliza ni kwanini alikataa kuwaambia?.. Jibu ni rahisi, ni kwasababu walikuwa wanaujua ukweli lakini wakawa wanajifanya hawajui!.. Walikuwa wanajua kabisa Yohana alitumwa na Mungu, lakini wanajifanya hawajui katumwa na nani?. Hiyo ni tabia moja mbaya sana, ambayo hata sasa inaendelea katika roho.

Watu wengi wanayajua maandiko na ukweli wote, lakini hawataki kufanya au kutenda kama maandiko yanavyosema, na wakati huo huo wanakwenda kumwuliza Bwana na kumwomba katika maombi!..pasipo kujua kuwa wapo katika hatari ya kutokujibiwa chochote!..

Wanajua kabisa miili yao ni hekalu la Roho Mtakatifu, na kwamba hawapaswi kuiharibu wala kuichafua kwa vyovyote vile, lakini bado wanaiharibu kwa uzinzi, kwa uvaaji mbaya, kwa ulevi,  kwa uchoraji tattoo n.k.. Na wakati huo huo wanakwenda mbele za Bwana kuuliza, au kuomba uthibitisho!..Mwisho wa siku, kunakuwa hakuna majibu yoyote kwa walichokitazamia.

Ndugu dada au kaka, kama kuna kitu kimeandikwa katika maandiko, ambacho kipo wazi kabisa na ni cha moja kwa moja, huna haja ya kwenda kutafuta uthibitisho wa jambo hilo kwa maombi..hutajibiwa chochote!, utaishia kuomba kila siku na kurudia na kurudia, hutapata majibu yoyote!.. zaidi sana unaweza kujikuta unafungua mlango wa kuvamiwa na maroho yadanganyayo! Kwasababu umelikataa Neno la Mungu lililo wazi unakwenda kutafuta maono.. Siku zote fahamu kuwa Neno la Mungu(yaani biblia takatifu) ndio sauti ya Mungu, iliyo dhahiri na iliyowazi mbele yetu..

Kwamfano maandiko yanaposema..

1Wakorintho 6:9  “Au hamjui ya kuwa wadhalimu hawataurithi ufalme wa Mungu? Msidanganyike; waasherati hawataurithi ufalme wa Mungu, wala waabudu sanamu, wala wazinzi, wala wafiraji, wala walawiti,

10  wala wevi, wala watamanio, wala walevi, wala watukanaji, wala wanyang’anyi”.

Hapo unahitaji ufunuo gani kuelewa hilo andiko??.. Inahitaji maombi gani ili uulewe!.. Unahitaji kufunga nini Mungu akufunulie kuwa ULEVI ni dhambi au uzinzi, au kuabudu sanamu?, na ilihali maandiko yanasema wazi kabisa hapo waabudu sanamu hawataurithi uzima wa milele?..Ukiwa na tabia hiyo kamwe hutamsikia Mungu akizungumza na wewe..

Bwana atusaidie tusiwe wanafiki mbele zake wala tusimjaribu.. Vile vile tulizingatie neno lake na kuliishi.

Maran atha!

Group la whatsapp jiunge na magroup yetu ya whatsapp kwa kubofya hapa > Group-whatsapp

Tafadhali washirikishe na wengine habari hizi njema,

Kwa maombezi/Ratiba za ibada/ Ushauri/ Maswali.
Piga namba hizi: +255693036618 au +255789001312

pia kama utapenda uyapate mafundisho haya kwa njia ya Whatsapp au email basi tutumie ujumbe kwenye namba hizo hizo.


Mada Nyinginezo:

Akawaambia Enendeni ulimwenguni mwote,MKAIHUBIRI INJILI KWA KILA KIUMBE.(Marko16:15.) Yesu Anamaanisha nini kusema MKAIHUBIRI INJILI KWA KILA KIUMBE?

TEGEMEA MUNGU KUZUNGUMZA NAWE KATIKA MAMBO MADOGO

Ni kwa namna gani malaika wa mbinguni wanaweza kutuhubiria sisi injili?

INJILI YA MANENO LAINI ITAKUGHARIMU.

Rudi nyumbani

DOWNLOAD PDF
WhatsApp

Source URL: https://wingulamashahidi.org/2021/08/29/ni-kipi-kinamzuia-mungu-kuzungumza-na-sisi/