KIFAHAMU KIGEZO  CHA KUSAMEHEWA NA MUNGU.

by Admin | 31 August 2021 08:46 pm08

Shalom nakusalimu katika jina kuu la Bwana wetu Yesu Kristo. Leo nataka tujifunze jambo la muhimu sana ambalo Bwana anataka tufahamu tunapokwenda mbele zake hususani katika kumwomba msamaha au rehema..hili ni jambo la muhimu sana..naomba usome hadi mwisho.

Kwa kawaida hakuna mtu asiyemkosea Mungu..hata kama hutamkosea kwa dhambi ya moja kwa moja zipo dhambi nyingine ndogo ndogo  ambazo si rahisi kuzitambua kwa haraka..kwamfano unaweza kumkwaza jirani yako kwa kauli fulani.ambayo pengine wewe uliiona ni sawa tu, lakini kumbe hujui tayari ulishatenda dhambi mbele za Mungu, kumfanya mwenzako ajisikie vibaya…na ndio maana maisha ya toba ni ya muhimu sana kwa mkristo yeyote..

Sasa jambo ambalo wengi hatujui ni kuwa msamaha wa Mungu unayo masharti yake..huwa hauji hivi hivi tu kama unavyodhani..Na leo tutaona ni kwanini..

Embu kaa chini uitafakari kwa makini ile sala ya Bwana..ukisoma pale vizuri utaona wanafunzi wake walipomwomba awafundishe kuomba hakusita kuwafundisha, mwanzoni alianza kwa kuwaambia vipengele vya kuombea, bila masharti au vigezo vyovyote ..kwamfano aliposema “utupe leo riziki zetu hakutoa” sababu yake mbele kwanini iwe hivyo..hakusema kwa kuwa na sisi tunawapa wengine riziki zetu..hapana..bali alisema tuombe tu hivyo hivyo na Mungu atatugawia..vilevile aliposema “usitutie majaribu” hakusema kwasababu na sisi hatuwatii watu wengine majaribuni hapana..alisema tuombe tu hivyo hivyo inatosha na yeye mwenyewe atatuepusha na majaribu yote…

Lakini alipofikia kipengele cha Utusamehe makosa yetu..utaona hapo hapo alitoa na sababu ya kwanini sisi tusamehewe..na sababu yenyewe ni kwasababu na sisi tunawasamehe waliotukosea makosa yetu..

Hapo ndipo Mungu anapataka kila mmoja wetu ajue na aliweke hilo akilini kwamba hayo mawili yanakwenda sambamba..hapo hamvumilii mtu yeyote..na ndio maana kayaambatanisha yote mawili  kwa pamoja.

Tusome..

Mathayo 6:9 “Basi ninyi salini hivi; Baba yetu uliye mbinguni, Jina lako litukuzwe, Ufalme wako uje,

10 Mapenzi yako yatimizwe, hapa duniani kama huko mbinguni.

11 Utupe leo riziki yetu.

12 Utusamehe deni zetu, kama sisi nasi tuwasamehevyo wadeni wetu.

13 Na usitutie majaribuni, lakini utuokoe na yule mwovu. [Kwa kuwa ufalme ni wako, na nguvu, na utukufu, hata milele. Amina.]

14 Kwa maana mkiwasamehe watu makosa yao, na Baba yenu wa mbinguni atawasamehe ninyi.

15 Bali msipowasamehe watu makosa yao, wala Baba yenu hatawasamehe ninyi makosa yenu”.

Umeona bado huko mwishoni kabisa Kristo analiwekea tena msisitizo neno lile lile alilolisema katika hiyo sala..kwamba Mungu anasamehe tu pale tunaposamehe..ndugu Mungu anaweza kukupa kila kitu unachomwomba hata kama wewe huwapi  wengine hivyo vitu…anaweza kukufanyia jambo lolote lile utakalo hata kama huwafanyii wengine hayo..unaweza ukawa mchoyo wa kupindukia na mbinafsi kwelikweli hutaki kuwapa watu vyakula vyako vinaozea huko ghalani..lakini ukamwomba Mungu akupe nafaka nyingi zaidi na akakupa tena tele mpaka ukakosa pa kuweka.

Lakini kwenye suala la kumwomba msamaha kama hutamsamehe ndugu yako aliyekukosea..hutamsamehe mke wako/mume wako aliyekuvunja moyo au kukusaliti ..sahau Mungu kukusamehe na wewe makosa yako..hiyo ondoa akilini kumbuka Mungu yupo makini (STRICT) sana na neno lake…akisema amesema..usijidanganye wala usidanganywe na mtu..huna msamaha wowote wa dhambi zako zote zilizokutangulia wala unazozitenda leo hii..

Ukifa leo ni moja kwa moja kuzimu..hakuna mzaha hapo..Na ndio maana jambo la KUSAMEHE linapaswa liwe ni sehemu ya maisha yetu ya kila siku. Haijalishi amekuudhi kiasi gani, amekutukana mara ngapi..kama bado una vinyongo vya tokea mwaka juzi, hutaki kuachilia na bado unaona okay..utakufa vibaya sana Ndugu ukiendelea hivyo, haijalishi utasema umeokoka. Dhambi hii imewashusha wengi kuzimu. Ni wengi kweli kweli kwasababu neno msahama kwao ni gumu lakini bado wanawataka na wenyewe wasamehewe na Mungu.

Bwana atutie nguvu. Tujifunze kusamehe Tutembee katika kanuni zake.Ili tuishi kwa amani hapa duniani, tuikwepe hukumu ya Mungu.

Shalom.

Tafadhali washirikishe na wengine habari hizi njema,

Kwa maombezi/Ratiba za ibada/ Ushauri/ Maswali.
Piga namba hizi: +255693036618 au +255789001312

pia kama utapenda uyapate mafundisho haya kwa njia ya Whatsapp au email basi tutumie ujumbe kwenye namba hizo hizo.

Mada Nyinginezo:

SAMEHE KUTOKA NDANI YA MOYO WAKO.

Je! Kuna dhambi kubwa na ndogo, na kama hakuna je! Mtu aliyeua na aliyetukana je watapata adhabu sawa?

NI KIPI KINAMZUIA MUNGU KUZUNGUMZA NA SISI?

SISI NI WINDO BORA SANA, LA DHAMBI.

Kama Mungu ndiye kaumba kila kitu, je ni yeye huyo huyo ndiye aliyeumba dhambi pia?

Rudi nyumbani

DOWNLOAD PDF
WhatsApp

Source URL: https://wingulamashahidi.org/2021/08/31/kifahamu-kigezo-cha-kusamehewa-na-mungu/