ISHARA ITAKAYONENEWA

by Admin | 10 January 2022 08:46 pm01

Ni kwanini Bwana Yesu amefanyika kuwa ishara itakayonenewa?..Nini maana ya kunenewa?.

Luka 2:34 “Simeoni akawabariki, akamwambia Mariamu mama yake, Tazama, huyu amewekwa kwa kuanguka na kuinuka wengi walio katika Israeli, na kuwa ishara itakayonenewa”.

Kunenewa kunakozungumziwa hapo sio “kenenewa vizuri” bali “kunenewa vibaya”.

Wana wa Israeli, walitegemea Masihi atazaliwa katika jumba la Kifalme, ataishi maisha ya kifahari, atakuwa mkuu na Mfalme ndani ya muda mfupi sana. Na atakuwa na fahari kuliko Sulemani, na zaidi ya yote atakuwa hafi, anadumu milele.

Ndicho walichokuwa wanategemea, kukiona kwa Masihi atakayekuja.

Lakini alipokuja Masihi mwenyewe (yaani Yesu) na kuona kwanza anazaliwa zizini na si kwenye jumba la kifalme kama walivyopanga, wakapata mashaka.

Walipomwona anakula na kunywa na watu maskini tena wenye dhambi mashaka yakaongezeka zaidi.

Lakini zaidi ya yote waliposikia kwamba eti atakufa na kufufuka, ndio kabisa wakasema huyu sie!.

Yohana 12:32 “Nami nikiinuliwa juu ya nchi, nitawavuta wote kwangu.

33 Aliyanena hayo akionyesha ni mauti gani atakayokufa.

34 Basi mkutano wakamjibu, Sisi tumesikia katika torati ya kwamba Kristo adumu hata milele; nawe wasemaje ya kwamba imempasa Mwana wa Adamu kuinuliwa? Huyu Mwana wa Adamu ni nani?”.

Hivyo walikuwa wanazitafuta ishara kuu…katika vichwa vyao walikuwa wameshajiaminisha kuwa Masihi atakuwa kama Malaika-Mtu hawezi kufa, na atakuwa ameshika fimbo ya chuma kuyatiisha mataifa na wakati anazaliwa tu atakuwa tajiri.

Hivyo Ishara hiyo ya Ukuu uliopitiliza hawakuiona kwa Masihi, na kinyume chake masihi akaja kwa nyingine tofauti kabisa na ishara yenyewe ni ISHARA YA YONA.

Kikawaida hakuna mtu angependwa kufananishwa na Yona. Hakuna mtu anayevutiwa na tabia ya Yona, wala hakuna mtu anayetamani kuwa kama Yona, kwasababu ishara ya Yona sio nzuri.

Lakini Masihi aliichagua ishara hiyo badala ya ishara ya Ukuu na ufalme, Na kwa ishara hiyo ikawafanya watu kumnenea vibaya kama walivyomnenea nabii Yona.

Mathayo 12:38 “Hapo baadhi ya waandishi na Mafarisayo wakamjibu, wakasema, Mwalimu, twataka kuona ishara kwako.

39 Akajibu, akawaambia, Kizazi kibaya na cha zinaa chatafuta ishara, wala hakitapewa ishara, ila ishara ya nabii Yona.

40 Kwani kama vile Yona alivyokuwa siku tatu mchana na usiku katika tumbo la nyangumi, hivyo ndivyo Mwana wa Adamu atakavyokuwa siku tatu mchana na usiku katika moyo wa nchi”.

Tukio la Yona kukaa tumboni kwa samaki siku tatu, leo hii linaonekana kama la kipumbavu, lakini pasipo ile ishara watu wa Ninawi wasingetubu!..wangedhani Yona kajizukia tu na kuanza kuhubiri habari zake, lakini waliposikia kuwa alikaa tumboni siku tatu bila kufa, wakatafakati alipataje pataje hewa akiwa kule tumboni muda wa siku tatu, alikaajekaaje bila kufa kule, wakaogopa, wakajua ule ni uweza wa Mungu.

Hivyo wakatubu kwa ishara hiyo, lakini endapo Yona angetoka moja kwa moja Israeli na kwenda Ninawi bila ishara yoyote, watu wa Ninawi wasingemsikiliza.

Na hata leo ni hivyo hivyo, Masihi alipenda kuchagua njia ya Mauti kama ishara kuu, ili sisi tuzidi kumwamini.

Hebu tafakari angekuja tu na kuishi na kisha kupaa bila kufa, tungeaminije kwamba mtu akifa anaweza kufufuka tena?.
Hivyo ilibidi na yeye afe, azikwe na kisha afufuke ili sisi tuuone uweza wa kiungu uliopo ndani yake, na kupitia huo Umetufanya kumwamini yeye mara nyingi zaidi na vile vile kuleta mazao mengi zaidi kwake.

Yohana 12:23 “Naye Yesu akawajibu, akasema, Saa imefika atukuzwe Mwana wa Adamu.

24 Amin, amin, nawaambia, Chembe ya ngano isipoanguka katika nchi, ikafa, hukaa hali iyo hiyo peke yake; bali ikifa, hutoa mazao mengi”.

Swali ni je! Na wewe leo umemwamini Bwana kupitia Ishara hiyo Ya kufa na kufufuka kwake? Je unaineneaje hiyo ishara..unainenea vyema au vibaya?, Unamtazama Kristo kwa jicho gani leo?.

Unamtazamia Kristo yule wa kukupa majumba na magari ya kifahari, au unamtazamia yule aliyekufa kwaajili ya dhambi zako, yule anayekwambia utubu!
Kristo wa kweli anasema hivi.

Marko 8:34 “Akawaita mkutano pamoja na wanafunzi wake, akawaambia, Mtu ye yote akitaka kunifuata na ajikane mwenyewe, ajitwike na msalaba wake, anifuate.

35 Kwa kuwa mtu atakaye kuiponya nafsi yake, ataiangamiza, na mtu atakayeiangamiza nafsi yake kwa ajili yangu na kwa ajili ya Injili, huyu ataisalimisha.

36 Kwa kuwa itamfaidia mtu nini kuupata ulimwengu wote, akipata hasara ya nafsi yake?

37 Ama mtu atoe nini badala ya nafsi yake?”

Utatoa nini ili ujitoe kuzimu siku ile?, kwa uasherati unaoufanya?, Kwa ulevi unaoufanya, kwa wizi unaoufanya?..fedha hazitakutoa kuzimu siku ile, vile vile mzazi hatakutoa kuzimu, wala mpenzi, wala Raisi.

Ayubu 7:9 “Kama vile wingu likomavyo na kutoweka, Ni vivyo huyo ashukaye kuzimuni hatazuka tena kabisa.

10 Hatarudi tena nyumbani kwake Wala mahali pake hapatamjua tena”.

Mpokee leo Yesu akufanye kiumbe kipya, na ya kale yote yatakuwa yamepita, na atakufanya kuwa mpya.

Maran atha!

Tafadhali washirikishe na wengine habari hizi njema,

Kwa maombezi/Ratiba za ibada/ Ushauri/ Maswali.
Piga namba hizi: +255693036618 au +255789001312

pia kama utapenda uyapate mafundisho haya kwa njia ya Whatsapp au email basi tutumie ujumbe kwenye namba hizo hizo.


Mada Nyinginezo:

YONA: Mlango 1

YONA: Mlango wa 2


Mitume wote waliopita walikuwa ni watu weupe hata manabii wote waliopita hadi Ma-papa ni ngozi nyeupe. ni kweli ngozi nyeusi ililaaniwa ?

YONA: Mlango wa 4

MATARAJIO YA KILA MWANADAMU DUNIANI NI YAPI?

Rudi nyumbani

DOWNLOAD PDF
WhatsApp

Source URL: https://wingulamashahidi.org/2022/01/10/ishara-itakayonenewa/