AKAJIFUNGA VAZI LAKE, AKAJITUPA BAHARINI.

by Admin | 18 March 2022 08:46 pm03

Bwana Yesu asifiwe.

Ulishawahi kulitafakari kwa ukaribu lile tukio, ambalo Bwana Yesu aliwatokea wanafunzi wake kwa sura nyingine, walipokuwa baharini wanavua?. Utaona muda wote aliokuwa anazungumza nao wasimtambue Petro alikuwa uchi, Lakini Yohana alipomtambua, kuwa ni Bwana Yesu yupo katikati yao, moja kwa moja alimwambia Petro ufunuo huo.

Na tukio lililofuata pale, utaona Petro hakwenda kumkumbatia, au kumsalimia, au kumsujudia..Bali, tukio la kwanza alilolifanya ni kuificha aibu yake mbele za Bwana. Ndio maana muda ule ule akavaa nguo zake, na akaona hilo halitoshi akajitupa kabisa baharini, kujisitiri,

Yohana 21:5 “Basi Yesu akawaambia, Wanangu, mna kitoweo? Wakamjibu, La.

6 Akawaambia, Litupeni jarife upande wa kuume wa chombo, nanyi mtapata. Basi wakatupa; wala sasa hawakuweza kulivuta tena kwa sababu ya wingi wa samaki.

7 Basi yule mwanafunzi ambaye Yesu alimpenda akamwambia Petro, Ndiye Bwana. Naye Simoni Petro, aliposikia ya kwamba ni Bwana, akajifunga vazi lake, (maana alikuwa uchi), akajitupa baharini.

Hiyo ni kutufundisha nini? Kuwa Bwana anapenda heshima, hapendezwi na watu wasiojiheshimu miili yao, pale wanaposimama mbele yake. Petro ni mwanaume, anasimama mbele ya mwanaume mwenzake, lakini anaona aibu kukaa uchi..

Jiulize wewe mwanamke, ambaye, unajisikia amani, kuvaa vimini, Una Roho Mtakatifu kweli? Na kibaya Zaidi unamfuata Yesu kanisani, unajifanya kumlilia, na kumwimbia na mavazi ambayo huwezi kwenda nayo hata kwa wazazi wako!!. Huoni kama unamvunjia Kristo heshima?

Unajisikiaje, unapovaa suruali kama mwanaume halafu unakwenda kumwabudu Kristo?. Unavaa nguo za migongo wazi, unatembea barabarani, halafu unasema umeokoka, kivipi? Wewe sio mtumwa wa Kristo,  kwasababu watumwa wa Kristo, kama Petro huwa wanaona aibu kukaa uchi, mpaka wanajitupa baharini.

Embu kachome hizo nguo, kuonyesha kweli unamuheshimu Kristo, vaa mavazi ya kujisitiri ya kike, kwani unapunguka nini Ukivaa sketi ndefu au gauni, dada utaumwa? Sasa kwanini ufunue mapaja yako barabarani, kila mtu ayatazame?

Petro alipokwisha kujisitiri, ndipo utaona Bwana Yesu anazungumza naye, lugha ya kiutumishi.. Anamwambia Petro wanipenda? Anasema ndio, Bwana anaendelea kumwambia Chunga, kondoo wangu!, Lisha kondoo zangu!. Lakini hapo kabla hakuzungumza naye lugha kama hizo kwasababu, alikuwa uchi mbele zake.

Jitose baharini dada, Ona aibu, kuwa tayari kuacha mavazi ya kikahaba, achana na fasheni, Onekana mshamba mbele za watu, lakini kwa Kristo mwerevu. Hakuna namna vimini na suruali vitakusogeza kwa Kristo, hakuna namna dada!, ni lazima uukimbie ulimwengu tu.

1Yohana 2:15 “Msiipende dunia, wala mambo yaliyomo katika dunia. Mtu akiipenda dunia, kumpenda Baba hakumo ndani yake”.

Injili za manabii wa uongo zinazokuambia Mungu anaangalia roho, haangalii mwili, jiangalie sana, kama ni hivyo  basi hata hiyo afya na rizki unazomuomba kila siku hana haja ya kukupa kwasababu haangalii mwili anangalia Roho yako tu, akupe uzima wa milele.

Ndugu,Vyote Bwana anavijali, isitoshe, hata siku ile ya mwisho, miili yetu pia itaokolewa, haitapotezwa na kutupwa motoni kama watu wanavyodhani, bali itaokolewa kwa kuvikwa miili ya kimbinguni(1Wakorintho 15:53-54). Yaani kwa ufupi hutakwenda mbinguni, kama mwili wako haujakombolewa.

Maandiko kama haya, hayajaandikwa kama stori kutuonyesha jinsi gani Petro anajua kujirusha baharini, na kuvaa nguo, bali ni kutufundisha sisi, tuwejeke sawa, pale tunapotaka kusimama mbele ya Bwana wetu, na mwokozi wetu.

Bwana atujalie kuliona hili.

Shalom.

Tafadhali washirikishe na wengine habari hizi njema,

Kwa maombezi/Ratiba za ibada/ Ushauri/ Maswali.
Piga namba hizi: +255693036618 au +255789001312

pia kama utapenda uyapate mafundisho haya kwa njia ya Whatsapp au email basi tutumie ujumbe kwenye namba hizo hizo.

Mada Nyinginezo:

UVUVI BORA HAUCHAGUI, CHA KUVUA.

Kwanini wakristo walipomuona Petro akigonga walisema “Ni malaika wake”?

Je suruali ni vazi la kiume tu?

ISHARA ITAKAYONENEWA

Rudi nyumbani

DOWNLOAD PDF
WhatsApp

Source URL: https://wingulamashahidi.org/2022/03/18/akajifunga-vazi-lake-akajitupa-baharini/