KABILA LA BENYAMINI.

by Admin | 26 March 2022 08:46 pm03

Jina la Bwana na mwokozi wetu Yesu, Kristo libarikiwe. Karibu tujifunze biblia..

Katika wana wa Yakobo, aliyekuwa mdogo kiumri kuliko wote alikuwa ni Benyamini, ambaye alikuwa ni mdogo wake Yusufu. Huyu Benyamini ndiye mtoto pekee wa Yakobo ambaye hakupata kumfaidi mama yake mzazi, hata kunyonya kutoka kwa mama yake, hakunyonya kabisa..kwani siku ile anazaliwa tu!, ndipo na mama yake anakata roho.

Na siku anazaliwa mama yake alimwite “Benoni” maana yake “mwana wa uchungu wangu”..lakini baba yake alimbadilisha hilo jina na kumwita “Benyamini” maana yake “mwana wa mkono wangu wa kuume” (Kutoka 35:16-20).

Kabila la Benyamini, wakati linaingia katika nchi ya ahadi, ndilo lililokuwa kabila lenye watu wachache kuliko yote.

Na Zaidi ya yote, baada ya kuingia katika nchi ya ahadi, maandiko yanaonesha kuwa kuna kipindi wabenyamini wengi waliuawa..wakabaki watu mia sita tu! (600). Na waliuawa kutokana na kosa la kumtendea ukatili yule Suri wa Mlawi, wa Bethlehemu-Yuda.

Kosa lile liligharimu Maisha ya wabenyamini wengi sana wakike na wakiume na watoto..na kama sio hekima ya Mungu kuingilia kati, basi kabila hili lingetoweka kabisa..Kwani waliosalia walikuwa ni wanaume 600 tu, katika kabila lote..na wengine wote walikufa..

Wakati makabila mengine kama Yuda yalikuwa na watu Zaidi ya milioni moja..kabila la Benyamini lilibakiwa na watu 600 tu!..(tena ni wanaume tu!, wanawake wote walikufa) na Zaidi ya yote bado ndio kabila dogo kuliko yote, kwani baba yao Benyamini ndiye aliyekuwa mdogo kuliko wote katika wa nawa Yakobo.

Waamuzi 21:17 “Wakasema, Lazima kuwa urithi kwa hao wa Benyamini waliopona, isiwe kabila kufutika katika Israeli”.

Hivyo lilikuwa ni kabila la kudharaulika kuliko yote!.. siku zote Wabenyamini hawakuwa watu wa heshima sana, ukilinganisha na makabila mengine kama Lawi, au Yuda au Efrahimu.

Lakini ijapokuwa ndio lilikuwa kabila dogo kuliko yote, na lenye watu wachache kuliko yote, na lililodharaulika kuliko yote, machoni pa watu.. lakini jicho la Mungu ni tofauti na la wanadamu, kwasababu Mungu haangalii kama wanadamu.

Ilipofika kipindi ambacho Israeli wanataka Mfalme wa kuwatawala mfano wa mataifa mengine yote, walikutana na jambo kinyume na mategemeo yao.

Wakati wanadhani kuwa pengine Mungu angemchagua mtu Fulani mashuhuri kutoka katika kabila mojawapo kubwa kubwa, tena lenye heshima.. kinyume chake, alimchagua mtu kutoka katika lile kabila dogo kuliko yote, tena katika ile familia ndogo kabisa.. Kinyume na matarajio yao. Na mtu huyo hakuwa mwingine Zaidi ya Mfalme Sauli.

1Samweli 9:21 “Basi Sauli akajibu, akasema, JE! MIMI SI MBENYAMINI, MTU WA KABILA ILIYO NDOGO KULIKO KABILA ZOTE ZA ISRAELI? NA JAMAA YANGU NAYO SI NDOGO KULIKO JAMAA ZOTE ZA KABILA YA BENYAMINI? kwa nini basi, kuniambia hivyo?”.

Sauli aliwatawala Israeli kwa muda miaka 40, sawasawa kabisa na alivyotawala Daudi na Sulemani.. Ijapokuwa Sauli alikuwa na kasoro kasoro nyingi, lakini Bwana alimchagua kuliongoza taifa lake takatifu kwa wakati huo.

Ni nini tunajifunza kwa kabila hili?

Tunachoweza kujifunza ni kuwa jicho la Mungu si la mwanadamu.. Yule ambaye anaonekana si kitu mbele za watu leo, yule anayeonekana kuwa hafai.. Mungu anaweza kumnyanyua kutoka mavumbini na kumpandisha juu.. Hivyo kwa vyovyote hatupaswi kujidharau, wala kuwadharau wengine.. wala tusiziogope dharau kwasababu jicho la Mungu ni tofauti na la wanadamu.

1Wakorintho 1:26 “Maana, ndugu zangu, angalieni mwito wenu, ya kwamba si wengi wenye hekima ya mwilini, si wengi wenye nguvu, si wengi wenye cheo walioitwa;

27 bali Mungu aliyachagua mambo mapumbavu ya dunia awaaibishe wenye hekima; tena Mungu alivichagua vitu dhaifu vya dunia ili aviaibishe vyenye nguvu;

28 tena Mungu alivichagua vitu vinyonge vya dunia na vilivyodharauliwa, naam, vitu ambavyo haviko, ili avibatilishe vile vilivyoko;

29 mwenye mwili awaye yote asije akajisifu mbele za Mungu”.

Bwana alilinyanyua kabila la Benyamini, anaweza kufanya kwako au kwa mwingine yeyote.. Mwamini Mungu, wala usijidharau.

Maran atha!

Tafadhali shea na wengine ujumbe huu;

Pia Kwa maombezi/ Ushauri/ Maswali/ Whatsapp:
Tuandikie katika BOXI la Maoni hapo chini au
Piga namba hizi: +255693036618 au +255789001312


Mada Nyinginezo:

Bwana Yesu alikuwa kabila gani?

Ni kwa namna gani Yesu ni Simba wa Yuda?

Kwanini Bwana Yesu alitokea katika ukoo wa Yuda?

Amri zilizo ndogo alizozizungumzia Yesu ni zipi?

NA ABARIKIWE KILA AKUBARIKIYE, NA ALAANIWE KILA AKULAANIYE.

Rudi nyumbani

DOWNLOAD PDF
WhatsApp

Source URL: https://wingulamashahidi.org/2022/03/26/kabila-la-benyamini/