IJUE SIRI YA UTAUWA.

by Admin | 31 March 2022 08:46 am03

Maandiko yanasema..

1Timotheo 3:16 “Na bila shaka SIRI YA UTAUWA NI KUU…”.

Utauwa, maana yake ni UUNGU!.. Hivyo maandiko yanaposema.. “Siri ya Utauwa ni kuu”..maana yake ni kwamba “Siri ya Uungu ni kuu (yaani ni pana sana na ya kipekee)”.

Na Uungu (Utauwa)..unaozungumziwa hapo ni “Uungu wa Mungu”. Maana yake yeye ni nani, yupoje, anaonekanaje, anatendaje kazi, n.k

Sasa Mtume Paulo, kwa neema za Mungu, alipewa kuijua sehemu ndogo ya Uungu wa Mungu..na pasipo mashaka yoyote ya ufunuo huo alioupokea, akaiandika hivi..

1Timotheo 3:16 “Na bila shaka SIRI YA UTAUWA NI KUU. Mungu alidhihirishwa katika mwili, Akajulika kuwa na haki katika roho, Akaonekana na malaika, Akahubiriwa katika mataifa, Akaaminiwa katika ulimwengu, Akachukuliwa juu katika utukufu”.

Hebu tuviangalie kwa ufupi, hivyo vipengele 6 vya siri hiyo ya Uungu wa Mungu, ambavyo Mtume Paulo alifunuliwa kwa uweza wa Roho.

 1. MUNGU ALIDHIHIRISHWA KATIKA MWILI.

Sasa ni wakati gani Mungu alidhihirishwa katika Mwili?..bila shaka yoyote, ni kupitia Bwana Yesu Kristo.. kwahiyo kumbe Bwana Yesu alikuwa ni Mungu katika mwili?.. Hakika hiyo ilikuwa ni siri ya kipekee.. Kumbe yule aliyekuwa anazungumza na akina Petro, alikuwa ni Mungu mwenyewe, kumbe yule aliyekuwa anaongea na mafarisayo alikuwa ni Mungu mwenyewe, kumbe yule aliyepandishwa msalabani alikuwa ni Mungu mwenyewe!.. Hiyo ilikuwa ni Siri kubwa sana.

Mtume Yohana naye aliiona siri hiyo kwa sehemu na kusema..

Yohana 1:1 “Hapo mwanzo kulikuwako Neno, naye Neno alikuwako kwa Mungu, naye Neno alikuwa Mungu…..

14 Naye Neno alifanyika mwili, akakaa kwetu; nasi tukauona utukufu wake, utukufu kama wa Mwana pekee atokaye kwa Baba; amejaa neema na kweli.”

Umeona?, Tito naye aliiona hiyo siri kwa sehemu katika ..Tito 2:13 “tukilitazamia tumaini lenye baraka na mafunuo ya utukufu wa Kristo Yesu, Mungu mkuu na Mwokozi wetu” ..Na baadhi ya Mitume wa Bwana Yesu kama Tomaso, na  Manabii kama Isaya, walionyeshwa siri hiyo kwa sehemu. (Soma Yohana 20:28 na Isaya 9:6). Na zaidi sana Bwana mwenyewe, aliigusia siri hiyo katika Yohana 14:8-11.

 2. AKAJULIKANA KUWA NA HAKI KATIKA ROHO

Bila shaka hakuna mwingine aliyepata kibali, cha mambo ya rohoni kuliko Bwana Yesu, hakuna mtu aliyewahi kufanya miujiza mikubwa kuliko Bwana Yesu. Kwa mara ya kwanza pepo wameanza kutolewa kwa kukemewa na Bwana Yesu Kristo, Kwa mara ya kwanza wafu wanafufuliwa kwa kutamkiwa neno tu!, na idadi kubwa ya watu likuwa inaponywa kupitia jina lake..Hivyo katika roho hakuna mwingine aliyejulikana kuwa na Haki (yaani kupata kibali), kuliko Yesu.

 3. AKAONEKANA NA MALAIKA.

Ni wazi kuwa Malaika wanawaona watu wote, lakini hawawajui watu wote, Malaika wala shetani hawajui kilichopo ndani ya moyo wa wanadamu, siri hiyo ipo kwa Mungu tu!, na kwa mtu mwenyewe.

Vile vile Malaika hawajui sura ya mtu atakayezaliwa mwaka ujao..anayejua ni Mungu tu!.. Hivyo Malaika walikuwa hawamjua Masihi (ambaye ni Mungu katika mwili) atakuwaje kuwaje, na Zaidi sana walizijua sifa chache tu, lakini si zote..

Lakini siku ilipofika ya kuzaliwa kwake walimwona..na alipoishi na kuifanya kazi ya Mungu ndipo walimwelewa Zaidi.. Ndio likatimia hilo neno.. “akaonekana na Malaika”. Malaika wakamwona Mungu katika mwili.

 4. AKAHUBIRIWA KATIKA MATAIFA.

Ni nani mwingine aliyehubiriwa katika mataifa na anayehubiriwa sasa?.. bila shaka si mwingine Zaidi ya Bwana wetu Yesu Kristo.

Marko 16:15 “Akawaambia, Enendeni ulimwenguni mwote, mkaihubiri Injili kwa kila kiumbe”.

 5. AKAAMINIWA KATIKA ULIMWENGU.

Yesu Kristo ndiye peke yake ndiye anayeongoza kwa kuaminiwa na watu wengi duniani kuliko mtu mwingine yoyote, dini karibia zote (za uongo na za ukweli) pamoja na shetani mwenyewe na mapepo yake wanaamini kuwa Yesu katumwa kutoka mbinguni. Dini hizo zinaweza zisimkiri wazi, lakini zinaamini kuwa Bwana Yesu katoka mbinguni.

Yohana 12:42 “Walakini hata katika wakuu walikuwamo wengi waliomwamini; lakini kwa sababu ya Mafarisayo hawakumkiri, wasije wakatengwa na sinagogi”.

Na zaidi sana siku ya Mwisho, kila goti litapigwa na kila ulimi utakiri, kuwa Yesu Kristo ni Bwana.

Wafilipi 2:10 “ili kwa jina la Yesu kila goti lipigwe, la vitu vya mbinguni, na vya duniani, na vya chini ya nchi;

11 na kila ulimi ukiri ya kuwa YESU KRISTO NI Bwana, kwa utukufu wa Mungu Baba”.

 6. AKACHUKULIWA JUU KATIKA UTUKUFU.

Yohana 3:13 “Wala hakuna mtu aliyepaa mbinguni, ila yeye aliyeshuka kutoka mbinguni, yaani, Mwana wa Adamu”.

Kwa hoja hizi sita ni wazi kuwa Bwana Yesu ndiye siri ya Mungu, na ndiye Mungu mwenyewe aliyejidhihirisha katika mwili.

Sasa unaweza kuuliza kwanni Mtume Paulo auandike ufunuo huu kwetu, kwa uongozo wa Roho?.

Ni ili sisi tuzidi kuwa na Imani na Bwana Yesu, ili sisi tuzidi kumwamini, na kumtumainia?.. Je!, kwa kusikia kuwa Yesu ndiye Mungu, huoni inatuongezea Faraja sisi?, inatuongezea ujasiri na kuamini kuwa hakuna chochote kitakachoharibika, maadamu tunaye Mungu?..Hivyo Siri hiyo ni kwa faida yetu.

Lakini jukumu tulilonayo sisi, sio kusoma Habari hizi kama gazeti, bali kama Neno hai lenye kuleta mabadiliko ndani yetu.. Huu ni wakati wa kumwamini Bwana Yesu, na kubatizwa na kupokea Roho Mtakatifu, na vile vile kujitenga na dunia, na kukusanyika Pamoja na watakatifu wengine, huku tukiingoja ile ahadi tuliyoahidiwa ya mbingu mpya na nchi mpya.

Maran atha!

Tafadhali shea na wengine ujumbe huu;

Pia Kwa maombezi/ Ushauri/ Maswali/ Whatsapp:
Tuandikie katika BOXI la Maoni hapo chini au
Piga namba hizi: +255693036618 au +255789001312. Jiunge na magroup yetu ya whatsapp kwa kubofya hapa > WHATSAPP-Group


Mada Nyinginezo:

Ni SIRI gani Paulo aliyokuwa anaimaanisha katika Waefeso 5:32?

MPINGA-KRISTO

AKETIYE MAHALI PA SIRI PAKE ALIYE JUU.

Na alaaniwe ampigaye mwenzake kwa siri.

NG’OMBE MWEKUNDU ALIYEZALIWA ISRAELI, ANAFUNUA NINI?

Rudi nyumbani

DOWNLOAD PDF
WhatsApp

Source URL: https://wingulamashahidi.org/2022/03/31/ijue-siri-ya-utauwa/