Ni SIRI gani Paulo aliyokuwa anaimaanisha katika Waefeso 5:32?

Ni SIRI gani Paulo aliyokuwa anaimaanisha katika Waefeso 5:32?

Jibu: Labda tuanze kusoma kuanzia juu kidogo..

Waefeso 5:31 “Kwa sababu hiyo mtu atamwacha baba yake na mama yake, ataambatana na mkewe na hao wawili watakuwa mwili mmoja.

32 SIRI HIYO NI KUBWA; ILA MIMI NANENA HABARI YA KRISTO NA KANISA.

33 Lakini kila mtu ampende mke wake kama nafsi yake mwenyewe; wala mke asikose kumstahi mumewe”

Siri Paulo aliyoimaanisha hapo, sio nyingine Zaidi ya hiyo aliyoitaja hapo kwamba “WAWILI WATAKUWA MWILI MMOJA”. Hiyo ndiyo SIRI yenyewe.. Na kwanini iwe siri?, ni kwasababu ni jambo gumu kueleweka au kufafanulika kwamba watu wawili tofauti wenye miili miwili tofauti wamekutana halafu wanakuwa mwili mmoja, na ilihali ni watu wawili tofauti wenye miili miwili tofauti.. afadhali angesema “watakuwa nafsi moja au watakuwa wamoja”.. kidogo ingeweza kuwa rahisi kueleweka, lakini kuwa mwili mmoja? Hapo ni lazima kuna siri katikati yake.

Tunaona pia Bwana Yesu alilisisitiza tena jambo hilo hilo katika injili ya Marko.

Marko 10:7 “Kwa sababu hiyo mtu atamwacha babaye na mamaye, ataambatana na mkewe;

8 NA HAO WAWILI WATAKUWA MWILI MMOJA; HATA WAMEKUWA SI WAWILI TENA, BALI MWILI MMOJA”

Kwahiyo hiyo ni SIRI kubwa sana.

Lakini biblia imetupa uvumbuzi wa siri hiyo, ni kwa jinsi gani, wawili wanakuwa mwili mmoja na si roho moja.

Na uvumbuzi huo tunaupata pale Mwanzo, Mungu alipowaumba Adamu na Hawa.. Biblia inasema

Mwanzo 2:21 “Bwana Mungu akamletea Adamu usingizi mzito, naye akalala; kisha akatwaa ubavu wake mmoja, akafunika nyama mahali pake,

22 na ule ubavu alioutwaa katika Adamu Bwana Mungu akaufanya mwanamke, akamleta kwa Adamu.

23 Adamu akasema, SASA HUYU NI MFUPA KATIKA MIFUPA YANGU, na NYAMA KATIKA NYAMA YANGU, basi ataitwa mwanamke, kwa maana ametwaliwa katika mwanamume.

24 Kwa hiyo mwanamume atamwacha baba yake na mama yake naye ataambatana na mkewe, nao watakuwa mwili mmoja”.

 Hapo katika mstari wa 23, tunaona Adamu hakusema huyu ni “roho katika roho yangu” wala “nafsi katika nafsi yangu”..bali alisema huyu “ni nyama katika nyama yake”.. akimaanisha mwili wa mwanamke yule ni mwili wake…kwasababu katwaliwa kutoka kwake.

Kwahiyo mtu yeyote anayekwenda kuoa au kuolewa, yule aliyejiungamanisha naye, tayari wanakuwa mwili mmoja, kwasababu wote asili yetu ni Adamu. Na kama wanakuwa mwili mmoja maana yake, Baraka zote wanashiriki pamoja, na vile vile laana zote wanashiriki pamoja na mambo yote mazuri au mabaya, ya mwilini au rohoni wanakuwa wanashiriki pamoja.

Ndio maana kuna hatari kubwa sana ya kutoka nje ya ndoa na kuzini, au kufanya uasherati.. kwasababu yule unayezini naye, au unayefanya naye uasherati, kiroho unajiunganisha naye na kuwa mwili mmoja bila wewe kujijua, maandiko yanasema hivyo..

1Wakorintho 6:13 “…………….Lakini mwili si kwa zinaa, bali ni kwa Bwana, naye Bwana ni kwa mwili………………….

15 Je! Hamjui ya kuwa miili yenu ni viungo vya Kristo? Basi nivitwae viungo vya Kristo na kuvifanya viungo vya kahaba? Hasha!

16 Au hamjui ya kuwa YEYE ALIYEUNGWA NA KAHABA NI MWILI MMOJA NAYE? MAANA ASEMA, WALE WAWILI WATAKUWA MWILI MMOJA”

Hivyo kahaba au mtu yeyote unayefanya naye uasherati, kama kuna Laana amezibeba katika maisha yake, wewe unayeshiriki naye, nawe pia unazibeba, kama ana roho na mapepo unaposhiriki naye uzinzi huo, yale mapepo nawe pia yanapata hifadhi ndani yako, (mnayashiriki pamoja) kwasababu tayari mmekuwa mwili mmoja.

Ndio maana moja ya amri za Mungu ni USIZINI! Kwasababu uzinzi una madhara makubwa sana kiroho na kimwili.

Wagalatia 5:19 “ Basi matendo ya mwili ni dhahiri, ndiyo haya, UASHERATI, uchafu, ufisadi,

 20 ibada ya sanamu, uchawi, uadui, ugomvi, wivu, hasira, fitina, faraka, uzushi

21 husuda, ulevi, ulafi, na mambo yanayofanana na hayo, katika hayo nawaambia mapema, kama nilivyokwisha kuwaambia, ya kwamba watu watendao mambo ya jinsi hiyo hawataurithi ufalme wa Mungu”.

Bwana azidi atubariki.

Marna tha!

Tafadhali washirikishe na wengine habari hizi njema,

Kwa maombezi/Ratiba za ibada/ Ushauri/ Maswali.
Piga namba hizi: +255693036618 au +255789001312

pia kama utapenda uyapate mafundisho haya kwa njia ya Whatsapp au email basi tutumie ujumbe kwenye namba hizo hizo.


Mada Nyinginezo:

WALIPO WAWILI AU WATATU KWA JINA LANGU

WALIPO WAWILI AU WATATU KWA JINA LANGU

Noeli ni nini, na je! Neno hili linapatikana katika biblia?

JISHUSHE ILI MUNGU AKUHUDUMIE.

Tofauti kati ya uchafu wa mwilini na rohoni ni  ipi?

Rudi nyumbani

Print this post

About the author

Admin administrator

Subscribe
Notify of
guest
0 Comments
Inline Feedbacks
View all comments