HATARI! HATARI! HATARI!

by Admin | 1 August 2022 08:46 am08

Unajua ni kwanini Bwana Yesu alisema  “Jiangalieni basi jinsi msikiavyo?” (Luka 8:18)

Alijua kuwa kuna hatari kubwa sana ya mtu aliyesimama kupotea kwa kile tu anachokisikia ikiwa hakitokani na yeye.. Hivyo si kila jambo ni la kulisikiliza na kuliweka moyoni, Zama hizi ni zama za uovu.

Mambo haya makuu matatu, kuwa nayo makini sana siku hizi za mwisho.

  1. Maono
  2. Ndoto
  3. Mafunuo

Ikiwa Maisha yako yote unayoishi ni kutegemea tu maono unayoonyeshwa, au ndoto, au mafunuo, na huku umeliweka Neno la Mungu nyuma basi ujue, hatari ya kupotea ni kubwa sana..tena sana. Haijalishi yatakuwa yanatoka kwa Mungu au kwa shetani, kama unaliweka Neno la Mungu nyuma..Bado hatari ya kupotea ni kubwa sana kuliko unavyodhani ndivyo ilivyo.. Najua inaweza ikawa ni ngumu kupokea lakini ukweli ndio huo.

Leo tupo wakati ambapo mtu atakuambia nimepelekwa kuzimu, nikaonyeshwa hiki, na kile, nimeonyeshwa watu wanaokula pipi za ivory, na soda za cocacola wapo kuzimu, nimeonyeshwa mabinti wote, walioingia katika ndoa bila ubikira, wanazini, waume zao ni wale wakwanza waliozini nao, kabla hawajaokoka hao ndio wanapaswa wakaolewe nao, hivyo wakiolewa na wengine wanazini..Nimeonyeshwa watu wote wanaosali siku ya jumapili wapo jehanamu, nimeambiwa na Yesu watu wote wanaoota ndoto wanapaa wajiandae na moto, nimeambiwa, kama umeokoka, unapaswa urudishe madeni yote uliyowahi kuwatapeli watu huko nyuma hata kama huna uwezo huo, usipofanya hivyo ni ziwa la moto, kama unakwenda beach kuogelea ni kuzimu, kama upo katika ndoa na unatumia uzazi wa mpango ujue ni motoni moja kwa moja…n.k n.k. Ni mengi mno..

Mambo kama haya embu tujaribu kudhania kuwa ni kweli yanatoka kwa Mungu..Lakini nikikuuliza swali ni nini kimekupa uhakika kuwa kinatoka kwa Mungu, utanipa jibu gani? Utasema ni kwasababu mpendwa yule kaonyeshwa au mimi nimeonyeshwa?? Au ninamwamini sana yule? Unadhani hilo tu linatosha?

Je! Ikitokea mwingine akakamwambia watu wote wenye Ngozi nyeusi, wanayo laana ya Hamu, hivyo wasipokombolewa kwa kupitishwa kwenye kemikali maalumu ya kuchubuliwa Ngozi zao, hawataingia mbinguni..Je! hilo nalo utalithibitisha vipi?

Ndugu ukiishi kwa Neno la Mungu, ni elimu tosha, ni ushuhuda tosha..hata kama mtu akikuambia nimeonyeshwa mashoga  wote wapo motoni, wewe uliye na Neno, hutashangaa kana kwamba ni jambo jipya, kwasababu Neno linakuambia hivyo..Hata kama asingekuletea maono hayo.

1Wakorintho 6:9 “Au hamjui ya kuwa wadhalimu hawataurithi ufalme wa Mungu? Msidanganyike; waasherati hawataurithi ufalme wa Mungu, wala waabudu sanamu, wala wazinzi, wala wafiraji, wala walawiti,

10 wala wevi, wala watamanio, wala walevi, wala watukanaji, wala wanyang’anyi”.

Hivyo hapo hujaishi kwa maono yako, bali kwa Neno la Mungu, basi upo salama.. Hatari inakuja ni pale mtu unapotegemea  tu shuhuda, na kuziamini moja kwa moja bila hata ya kuzipima..ndugu  utatoka nje ya mpango wa Mungu, utachanganywa, utaishi kwa hofu na wasiwasi, na presha kubwa, kwasababu huyu atakuambia hivi yule vile, yatachanganyikana ya ukweli na uongo..matokeo yake utashindwa kujua ni wapi umesimama..Na mtu wa namna hii ni rahisi sana kuanguka dhambini. Na ndio maana kuna umuhimu mkubwa sana wa kuijua biblia.. SOMA BIBLIA.

Yohana 8:32 “tena mtaifahamu kweli, nayo hiyo kweli itawaweka huru”.

Kuwa makini na shuhuda unazozisikiliza mitandaoni (youtube)..Kuwa makini na watu unaowafuatilia mitandaoni. Usipoijenga Imani yako katika Neno la Mungu, shetani atakusaidia kujenga Imani yako katika misingi yake mwenyewe.

Usiniamini mimi, wala usimuamini mtu yeyote, iamini biblia yako, hiyo inatosha..Utakuwa salama.

Mwingine atakuambia Bwana ameniambia leta nywele zako, na kucha zako, weka kwenye kitambaa chekundu, tuombe Pamoja, ukimuuliza misingi hiyo ameitolea wapi, atakuambia nimefunuliwa, na usipofanya hivyo huwezi kufunguliwa.. Hii ni Hatari kubwa sana! ..Kataa kusikiliza hayo mafunuo.

Mwingine atakuambia, pasipo kuniamini mimi, huwezi kwenda katika unyakuo, kataa

1Timotheo 4:1 “Basi Roho anena waziwazi ya kwamba nyakati za mwisho wengine watajitenga na imani, wakisikiliza roho zidanganyazo, na mafundisho ya mashetani;”

Usiwe mwepesi wa kuamini Neno lolote usilolithibitisha katika maandiko,

Bwana atusaidie..

Tafadhali shea na wengine ujumbe huu;

Pia Kwa maombezi/ Ushauri/ Maswali/ Whatsapp:
Tuandikie katika BOXI la Maoni hapo chini au
Piga namba hizi: +255693036618 au +255789001312

Mada Nyinginezo:

MAFUNDISHO YA MASHETANI

USIPOTEZWE NA MANENO YA MANABII WA UONGO.

Amin, nawaambia, Kizazi hiki hakitapita..

KUONGOZWA SALA YA TOBA

USIISHI KWA NDOTO!

MIHURI SABA

Je Malaika Mikaeli ndiye Yesu mwenyewe?

Rudi nyumbani

DOWNLOAD PDF
WhatsApp

Source URL: https://wingulamashahidi.org/2022/08/01/hatari-hatari-hatari/