SEMA KWA LUGHA NYINGINE.

by Admin | 12 October 2022 08:46 am10

Jina la Bwana na Mwokozi wetu Yesu Kristo libarikiwe, karibu tujifunze na kuyatafakari maandiko pamoja.

Leo napenda tujifunze juu ya lile tukio maarufu lililotokea siku ile ya Pentekoste, ambapo tunasoma Roho Mtakatifu alishuka juu ya Wanafunzi wa Bwana Yesu 11, pamoja na wanafunzi wengine wengi, jumla yao ni watu 120 (Matendo 1:15).

Ilipotimia siku ya Pentekoste tunasoma kuwa Watu wote walishukiwa na “Ndimi zilizogawanyikana kama ndimi za moto”.

Matendo 2:1  “Hata ilipotimia siku ya Pentekoste walikuwako wote mahali pamoja.

2  Kukaja ghafula toka mbinguni uvumi kama uvumi wa upepo wa nguvu ukienda kasi, ukaijaza nyumba yote waliyokuwa wameketi.

3  Kukawatokea ndimi zilizogawanyikana, kama ndimi za moto uliowakalia kila mmoja wao”

Napenda tuyafakari hayo maneno kabla hatujaendelea mbele.

Neno la Kwanza ni “Ndimi”.. Ndimi ni wingi wa neno “ulimi”, Na mtu anapozungumzia Ulimi, anamaanisha “lugha”... Kwamfano tukitaafsiri neno “lugha mama” kwenda kwenye lugha ya kiingereza itakuwa ni “Mother tongue” na tafsiri ya “tongue” kwa Kiswahili ni “ulimi”.. Hivyo badala ya kusema “lugha mama” pia ni sahihi kusema “ulimi mama” (ni kitu kimoja).

Kwahiyo hapo biblia iliposema kuwa zilitokea “ndimi za moto” ilimaanisha kuwa ni “lugha za moto”.. Lakini haiishi hapo, biblia inaendelea kusema kuwa “zilikuwa ni ndimi zilizogawanyikana” maana yake ni kuwa zilikuwa ni “lugha zilizogawanyikana/tofautitofauti”.. kila mmoja alishukiwa na lugha yake tofauti na ya mwenzake.. Na lugha hizo hazikuwa za kimbinguni, bali za duniani kama vile Kiswahili, kiarabu, kihindi, kichina, kisukuma n.k

Matendo 2:4  “Wote wakajazwa Roho Mtakatifu, wakaanza kusema kwa lugha nyingine, kama Roho alivyowajalia kutamka.

5  Na walikuwako Yerusalemu Wayahudi wakikaa, watu watauwa, watu wa kila taifa chini ya mbingu.

6  Basi sauti hii iliposikiwa makutano walikutanika, wakashikwa na fadhaa, kwa kuwa kila mmoja aliwasikia wakisema kwa lugha yake mwenyewe.

7  Wakashangaa wote, wakastaajabu wakiambiana, Tazama, hawa wote wasemao si Wagalilaya?

8  Imekuwaje basi sisi kusikia kila mtu lugha yetu tuliyozaliwa nayo?

9  Warparthi na Wamedi na Waelami, nao wakaao Mesopotamia, Uyahudi na Kapadokia, Ponto na Asia, 10  Frigia na Pamfilia, Misri na pande za Libia karibu na Kirene, na wageni watokao Rumi, Wayahudi na waongofu,

11  Wakrete na Waarabu; TUNAWASIKIA HAWA WAKISEMA KWA LUGHA ZETU MATENDO MAKUU YA MUNGU.

12  Wakashangaa wote wakaingiwa na shaka, wakiambiana, Maana yake nini mambo haya?

Mstari wa 11, biblia inasema… “TUNAWASIKIA HAWA WAKISEMA KWA LUGHA ZETU MATENDO MAKUU YA MUNGU”.

Kumbe Wanafunzi hawa waliojazwa Roho Mtakatifu, walikuwa wananena matendo makuu ya Mungu.. Kumbe walisikika wakiyatangaza matendo makuu ya Mungu, na si mambo mengine..

Sasa mfano wa matendo hayo ni yapi?

Ndio kama yale ya Mungu kupasua bahari na wana wa Israeli kupita salama, ndio kama yale ya Mana kushushwa kutoka mbinguni kwa miaka 40, ndio kama yale ya Bwana kuziangusha kuta za Yeriko, ndio kama yale ya Eliya kushusha moto n.k n.K (Hayo ndio matendo ambayo mitume walisikika wakiyatangaza kwa lugha nyingine)…Na watu waliposikia wakikumbushwa matendo makuu hayo ya Mungu, tena kwa lugha za ndani kabisa..mioyo yao iliwaka, kutaka kumrudia Mungu na kutaka kujua zaidi.

Hebu tengeneza picha unamwona mzungu aliyetoka Ulaya anazungumza lugha yako ya kikabila tena ile ya ndani kabisa, ambayo hata wewe pengine huipati vizuri, na ukizingatia yeye ni mgeni kabisa, na hajawahi kufika huko kijijini kwenu.. halafu maneno anayoyasema ni ya kumtukuza Mungu, kwa matendo makuu aliyoyafanya katika biblia.

Bila shaka utaduwaa na kushangaa!! Na kujiuliza maswali mengi, na jibu la mwisho utakalolipata ni kusema “huu ni muujiza” na zaidi sana hata kile mzungu huyo anachokisema kitakuja kwa uzito kwako, tofauti na kama angeongea kwa lugha yake ile ile ya kiingereza.

Ndicho kilichotokea siku ya Pentekoste,  wanafunzi walisikika wakimtangaza Mungu kwa lugha mbalimbali, hivyo watu wakashangaa na kutenga muda kuwasikiliza, na siku hiyo wakaongezeka waongofu elfu 3.

Na sisi hatuna budi wakati mwingine, tuzungumze kwa lugha nyingine.. Kuzungumza kwa lugha nyingine si lazima kuwe kwa lugha ambayo huijui!, hapana! Hata kwa lugha yako hiyo hiyo lakini Bwana aibadilishe itoke kwa namna nyingine, ambayo italeta mageuzi kwa wale watakaokusikiliza.

Na si lazima kuwe kunena tu, bali hata KUIMBA, Bwana akabadilishe lugha na sauti yako iwe na uvuvio wa Roho ambao utawabadilisha watu wasikiao, na si katika kuimba tu, bali hata katika KUOMBA!. Bwana akabadili lugha yako, na kuwa lugha nyingine kusudi maombi yakolee munyu, mbele zake.

1Wakorintho 14:15 “Imekuwaje, basi? Nitaomba kwa roho, tena nitaomba kwa akili pia; mtaimba kwa roho, tena nitaimba kwa akili pia”.

Na si katika kuomba, na kuimba tu, bali hata katika MAISHA YETU YA KAWAIDA YA MAZUNGUMZO. Lugha zetu zinapaswa zibadilishwe.

Tukiwa watu wa lugha mbaya, maandiko yanasema tunaziharibu tabia zetu njema !(1Wakorintho 15:33). Na lugha mbaya ndizo zinazotukosesha kibali, lakini kauli mbaya huuwasha moto (Yakobo 3:6).

Siku ya leo ni siku ya kuomba BWANA AIBADILISHE LUGHA YAKO..Na kuwa lugha nyingine ya kuwafaa watu na kufaa mbele za Mungu.

Ikiwa bado hujaokoka, Bwana Yesu hawezi kuibadilisha lugha yako.. lakini leo hii ukiamua kumpokea Yesu maishani mwako kwa kumaanisha kabisa kwa dhati,  basi Bwana atakupa lugha mpya.. Na hivyo utakuwa mtu mwingine wa kuzaa matunda siku zote..

Basi ikiwa umeshampokea Yesu, au leo hii umeshafanya maamuzi ya kumpokea Yesu na kutubu dhambi zako, basi pata muda jitenge binafsi mahali pa utulivu, na kisha piga magoti kwa utulivu na uombe na mwombe Bwana akupe kipawa hicho cha lugha mpya, naye ni mwaminifu atakupa, na tangu siku hiyo utaona mabadiliko makubwa sana katika maisha yako..

Bwana akubariki.

Tafadhali shea na wengine ujumbe huu;

Pia Kwa maombezi/ Ushauri/ Maswali/ Whatsapp:
Tuandikie katika BOXI la Maoni hapo chini au
Piga namba hizi: +255693036618 au +255789001312

Mada Nyinginezo:

JE! UMEPOKEA KWELI ROHO MTAKATIFU?

Je Mungu ana njia ngapi za kuzungumza?

NINI TOFAUTI KATI YA MATENDO YA SHERIA NA MATENDO YA IMANI?

IFAHAMU HUZUNI NA FURAHA YA MALAIKA.

NYAKATI AMBAZO NI LAZIMA TUKUTANE NAZO TU.

Rudi nyumbani

DOWNLOAD PDF
WhatsApp

Source URL: https://wingulamashahidi.org/2022/10/12/sema-kwa-lugha-nyingine/