MWIMBIE BWANA ZABURI KATIKA NYAKATI ZA FURAHA.

by Admin | 6 November 2022 08:46 pm11

Biblia Inatufundisha kuomba pale tunapokuwa katika majaribu, au tunapokuwa katika hali ya kuhitaji jambo Fulani.

Mathayo 7:7 “Ombeni, nanyi mtapewa; tafuteni, nanyi mtaona; bisheni, nanyi mtafunguliwa;

8  kwa maana kila aombaye hupokea; naye atafutaye huona; naye abishaye atafunguliwa”.

Lakini pia haitufundishi tu kuomba bali pia inatufundisha KUIMBA NYIMBO WAKATI WA FURAHA!. (Hili ni jambo la muhimu kulijua).

Biblia inasema..

Yakobo 5:13 “Mtu wa kwenu amepatikana na mabaya? NA AOMBE. Ana moyo wa kuchangamka? NA AIMBE ZABURI”

Hapo anasema mtu wa kwenu akiwa amepatikana na mabaya basi aombe, labda kapatwa na maradhi, au kakumbana na majaribu mazito..katika hali hii, biblia imesema tuombe!! Na Mungu atatusikia na kutuokoa au kutuponya na misiba yetu..

Zaburi 107:

4 “Walitanga-tanga jangwani katika njia ya nyika; Hawakuona mji wa kukaa. 

5 Waliona njaa, waliona na kiu, Nafsi yao ilikuwa ikizimia ndani yao

 6 Wakamlilia Bwana katika dhiki zao, Akawaponya na shida zao”

Lakini pia biblia inasema ikiwa mtu ANA MOYO WA KUCHANGAMKA..Na AIMBE ZABURI..ambaye ana Maana yake kama mtu moyoni mwake anayo furaha, au kapata furaha…pengine kaona mkono wa Bwana ukimtetea, au Bwana kampa afya na kumwokoa na mabaya, Bwana  kampa amani, kampa utulivu n.k… mtu wa namna hii biblia imeshauri kuwa na “Aimbe zaburi” asikae tu kama alivyo!..

Sasa Zaburi ni nini?

Zaburi ni nyimbo maalumu za KUMTUKUZA MUNGU, KUMSIFU na KUMSHUKURU baada ya Bwana kututendea mema.. (Nyimbo hizi zinakuwa katika mfumo wa mashairi mazuri) mfano wa hizi ni zile Daudi alizokuwa anaziimba, kila baada ya kuuona wema wa Bwana!.

1Nyakati 16:7 “Ndipo siku hiyo Daudi alipoagiza kwanza kumshukuru Bwana, kwa mkono wa Asafu na nduguze.

 8 Mshukuruni Bwana, liitieni jina lake; Wajulisheni watu matendo yake.

 9 Mwimbieni, MWIMBIENI KWA ZABURI; Zitafakarini ajabu zake zote. 

10 Jisifuni kwa jina lake takatifu; Na ufurahi moyo wao wamtafutao Bwana”

Kila tunapomshukuru Bwana au tunapomsifu kwa Nyimbo hizi za Zaburi, tunajipandishia thamani zetu mbele za Mungu, na tunaithibitisha mioyo yetu mbele za Mungu.

Unajua ni kwanini Daudi alipata kibali sana Mbele za Mungu?.. Sababu mojawapo ni desturi yake hiyo ya kumwimbia Mungu Zaburi..(na ndio maana hata kitabu chake kikaitwa kitabu cha Zaburi).

Zaburi 57:7 “Ee Mungu, moyo wangu u thabiti, Moyo wangu u thabiti. NITAIMBA, NITAIMBA ZABURI, 

8 Amka, utukufu wangu. Amka, kinanda na kinubi, Nitaamka alfajiri.

 9 Ee Bwana, nitakushukuru kati ya watu, NITAKUIMBIA ZABURI KATI YA MATAIFA.

 10 Maana fadhili zako ni kubwa hata mbinguni, Na uaminifu wako hata mawinguni.

 11 Ee Mungu, utukuzwe juu ya mbingu, Na juu ya nchi yote uwe utukufu wako”

Kwahiyo ni muhimu kufahamu kuwa KUOMBA ni muhimu lakini pia KUIMBA ni muhimu sana (Hususani Zaburi)..Mambo haya mawili yanakwenda pamoja!.. haijalishi sauti yako ikoje, wewe mwimbie Mungu, kwasababu Mungu katuumba ili tumtukuze yeye na kumsifu, pasipo kujalisha sauti zetu.

1Wakorintho 14:15 “Imekuwaje, basi? Nitaomba kwa roho, tena nitaomba kwa akili pia; MTAIMBA kwa roho, TENA NITAIMBA kwa akili pia”

Lakini pia ni muhimu kujua kuwa Nyimbo za Zaburi lengo lake ni kumtukuza Mungu na kumshukuru, na kumwimbia na sio mipasho. Siku hizi za mwisho utaona mtu baada ya kufanyiwa wema na Mungu, ndio wakati wa yeye kuimba nyimbo ambazo anakuwa hana tofauti na watu wa kidunia ambao wanasemana kwa nyimbo!, huo ni udunia!. Na mtu wa namna hii asitegemee atapokea chochote kutoka kwa Bwana, haijalishi ananukuu zaburi kutoka kwenye biblia.

Siku zote ni lazima Nia zetu za kumwimbia Bwana ziwe takatifu mbele zake, na tusifanane na watu wa kidunia.. Hakuna mahali popote Daudi alimwimbia Sauli zaburi za kujionyesha kama yeye kakubaliwa mbele za Mungu zaidi ya Sauli, lakini kinyume chake utaona siku zote Daudi alimwombea rehema Sauli na zaidi sana alimheshimu hata kufikia hatua ya kumwita Sauli Masihi wa Bwana (yaani mpakwa mafuta wa Bwana), mtu ambaye usiku na mchana alikuwa anaitafuta roho yake.

Na sisi ni lazima tufanane na Daudi, tunamwimbia Mungu wetu Zaburi, huku fahamu zetu na akili zetu zikiwa zinamwelekea yeye(Bwana), na si zinawaelekea wale wanaotutesa, au kutuudhi, au kushindana nasi..huku tukiwaombea wote wanaopingana nasi kama Bwana Yesu, Mwalimu mkuu alivyotuelekeza katika…Mathayo 5:43

Mathayo 5:43 “ Mmesikia kwamba imenenwa, Umpende jirani yako, na, Umchukie adui yako;

44  lakini mimi nawaambia, Wapendeni adui zenu, waombeeni wanaowaudhi,

45  ili mpate kuwa wana wa Baba yenu aliye mbinguni; maana yeye huwaangazia jua lake waovu na wema, huwanyeshea mvua wenye haki na wasio haki?”

Bwana Yesu azidi kutubariki sote na kutusaidia.

Maran atha!

Tafadhali shea na wengine ujumbe huu;

Pia Kwa maombezi/ Ushauri/ Maswali/ Whatsapp:
Tuandikie katika BOXI la Maoni hapo chini au
Piga namba hizi: +255693036618 au +255789001312

Mada Nyinginezo:

IFAHAMU HUZUNI NA FURAHA YA MALAIKA.

JE! NINAWEZA KUPOTEZA FURAHA YA WOKOVU?

Furaha ni nini?

Je ni kweli kila nafsi itaonja mauti kulingana na (Zaburi 89:48)?

OLE WAO WANAOJITAHIDI KUMFICHA BWANA MASHAURI YAO.

Rudi nyumbani

DOWNLOAD PDF
WhatsApp

Source URL: https://wingulamashahidi.org/2022/11/06/mwimbie-bwana-zaburi-katika-nyakati-za-furaha/