NI KWANINI WATU WENGI WANASHINDWA KUMWELEWA MUNGU?

by Admin | 25 May 2023 08:46 am05

Je! Moyo wako upo kweli kwake?

Kuna kauli Bwana Yesu alisema kuhusiana na watu kumwelewa Mungu na uweza wake kwetu, alisema..

Mathayo 13:14  “Na neno la nabii Isaya linatimia kwao, likisema, Kusikia mtasikia, wala hamtaelewa; Kutazama mtatazama, wala hamtaona. 15  Maana mioyo ya watu hawa imekuwa mizito, Na kwa masikio yao hawasikii vema, Na macho yao wameyafumba; Wasije wakaona kwa macho yao, Wakasikia kwa masikio yao, WAKAELEWA KWA MIOYO YAO, WAKAONGOKA, NIKAWAPONYA”

Ametaja mambo makuu matatu,

  1. Kuona – Kwa macho
  2. Kusikia –kwa masikio
  3. Kuelewa – Kwa moyo

Hatua ya mwisho ambayo Mungu anatarajia, pindi anapomfundisha mtu, au kusema naye ni KUELEWA. Hivyo ataanza kwanza kwa kumwonyesha mambo kadha wa kadha, yatapita mbele yake, ataanza kusema na yeye kwa njia nyingi, aidha kwa wahubiri wake, au ndoto, au maono, au vitu vya asili, au kwa Neno lake, au kwa maisha yake mwenyewe.. Lakini  pamoja na njia zote hizo  bado mtu huyo anaweza asimwelewe Mungu, kama Moyo wako haupo kwake.

Jambo ambalo watu wengi hatujui, ni kwamba Mungu anazungumza na kila mmoja, Na kila mmoja anaonyeshwa maono mengi na Mungu, kila mtu ameshakutana na Mungu, aidha uso kwa uso au katika roho, haijalishi ni mwema au mwenye dhambi, Lakini ni wachache sana walioweza kuielewa sauti yake iliposema nao.

Ni kwasababu gani hawaielewi? Ni kwasababu inahitaji MOYO ili kuielewa, Na sio macho au sikio. Kama moyo wako haupo kwake, sahau kumwelewa Mungu anaposema na wewe kwa njia yoyote ile. Hata kama itakuja kwa dhahiri, bado hutamwelewa. Sauti yake kwako itakuwa ni ngurumo tu, kama ilivyokuwa kipindi kile Bwana Yesu alipokuwa anazungumza na makutano kuhusiana na ufalme wa mbinguni.

Yohana 12:28  “Baba, ulitukuze jina lako. Basi ikaja sauti kutoka mbinguni, Nimelitukuza, nami nitalitukuza tena. 29  Basi mkutano uliosimama karibu wakasikia, walisema ya kwamba kumekuwa ngurumo; wengine walisema, Malaika amesema naye.30  Yesu akajibu, akasema, Sauti hiyo haikuwako kwa ajili yangu, bali kwa ajili yenu”

Ni kwanini iwe hivyo kwao? Ni kwasababu kilichowapeleka kwa Yesu sio wokovu wa Roho zao, au upendo wao kwa Mungu, kilichowapeleka kwake, ni miujiza, uponyaji, uzuri, mwonekano, mazingira, basi, hakuna jipya. Wakishapata walichokuwa wanakitafuta hao wanaondoka zao kuendelea na mambo yao ya dhambi ya sikuzote.

Ndio maana hakukuwa na hata mmoja ambaye aliyeelewa mifano yote Yesu aliyokuwa anaisema mbele ya umati. Isipokuwa wanafunzi wake tu, pamoja na wachache waliomfuata baada ya pale kutaka kufafanuliwa.

Ndugu ikiwa leo unakwenda kanisani kutimiza tu ratiba, kutazama kwaya, kuangalia watu wamevaaje, hata ukiwepo humo unasinzia, unaangalia muda utatoka saa ngapi, ni kweli utakutana na Mungu, atasema na wewe, utamwona, utahisi uwepo wake, utanena hata kwa lugha, utasisimka moyo. Lakini kumwelewa, haitakaa iwezekane. Kwasababu Mungu hajifunui kwa watu ambao  mioyo yao haipo kwake.Hana utaratibu huo.

Na sio tu kanisani, hata mahali popote pale, iwe ni shuleni, kazini, nyumbani, barabarani, Mungu huwa anazungumza, anasema kwa njia mbalimbali tena kirahisi sana, Lakini hutaelewa ikiwa huna moyo wa dhati kwa Mungu wako.

Alisema hivi;;

2Nyakati 16:9 “Kwa maana macho ya Bwana hukimbia-kimbia duniani mwote, ili ajionyeshe mwenye nguvu kwa ajili ya hao, WALIOKAMILIKA MOYO KUELEKEA KWAKE…”

Alisema pia..

Mathayo 15:7  “Enyi wanafiki, ni vema alivyotabiri Isaya kwa habari zenu, akisema, 8  Watu hawa huniheshimu kwa midomo; Ila mioyo yao iko mbali nami”.

Yatupasa sasa tuondoe unafiki wa ndani, kwa kumaanisha kweli kweli kumpenda Mungu kwa moyo, ili sasa aanze kutufunulia sauti yake na kazi zake. Tukimfuata Kristo tujue kinachotupeleka kule ni Utakatifu na haki, na sio kwasababu tunashida tutimiziwe mahitaji yetu, hapo ndipo atapendezwa na sisi, na hatimaye, tutamwona kila inapoitwa leo.

Bwana akubariki.

Shalom.

Tafadhali shea na wengine ujumbe huu;

Pia Kwa maombezi/ Ushauri/ Maswali/ Whatsapp:
Tuandikie katika BOXI la Maoni hapo chini au
Piga namba hizi: +255693036618 au +255789001312 Jiunge na magroup yetu ya whatsapp kwa kubofya hapa > WHATSAPP-Group

Mada Nyinginezo:

YESU HAYUPO KATIKA MAZINGIRA YALEYALE TU SIKUZOTE, USIJISAHAU.

MWANANGU, NIPE MOYO WAKO;

Biblia inaposema “Wote tumetenda dhambi” si inamaanisha hakuna mtakatifu duniani?

Amri zilizo ndogo alizozizungumzia Yesu ni zipi?

NIFANYE NINI ILI NIKUBALIWE NA YESU?

Je! Mwendo wa Sabato ulikuwaje kibiblia?(Matendo 1:12)

Rudi nyumbani

DOWNLOAD PDF
WhatsApp

Source URL: https://wingulamashahidi.org/2023/05/25/ni-kwanini-watu-wengi-wanashindwa-kumwelewa-mungu/