Nchi ya “Kabuli” ndio nchi gani kwasasa, na kwanini iliitwa hivyo? (1Wafalme 9:13).

by Admin | 7 December 2023 08:46 am12

Jibu: Tusome,

1 Wafalme 9:12 “Naye Hiramu akatoka Tiro kuitazama hiyo miji Sulemani aliyompa; wala haikumpendeza.

13 Akasema, Miji gani hii uliyonipa, ndugu yangu? Akaiita NCHI YA KABULI, hata leo”.

Nchi hiyo iliitwa “Nchi ya Kabuli” na sio “Nchi ya Kaburi”.Kuna tofauti ya “Kabuli” na “Kaburi”.

Maana ya “kaburi” ni shimo la kuzikia mtu aliyekufa, lakini “Kabuli” maana yake ni “isiyofaa kitu”. Kwahiyo hapo inaposema Nchi ya Kabuli, maana yake ni nchi isiyofaa kitu.

Sasa kwanini nchi hiyo iliitwa hivyo na huyu Hiramu?. Na ni funzo gani tunapata?.

Kipindi Sulemani anaijenga nyumba ya Mungu pamoja na nyumba yake mwenyewe, aliingia makubaliano na Mfalme wa Tiro kwamba Mfalme wa Tiro atampa Sulemani Malighafi za ujenzi (Miti ya Mierezi na mawe pamoja na malighafi nyingine baadhi, 1Wafalme 5:17-18), kwa makubaliano ya kwamba Mfalme Sulemani atampa Hirimu, mfalme wa Tiro ardhi kama malipo.

Sasa baada ya Sulemani kukamilisha ujenzi wa nyumba hizo mbili, ambapo alitumia miaka 20 (1Wafalme 9:10), aliazimu kumlipa Hirimu malipo yake.

Hivyo Sulemani akaamua kumpa Mfalme wa Tiro miji 20, (maana yake kila mji mmoja kwa mwaka mmoja aliotumikiwa). Zaidi ya hayo Sulemani alimpa Hiramu mwaka kwa mwaka kori nyingi za mafuta na ngano.

1Wafalme 5:10 “Basi Hiramu akampa Sulemani miti ya mierezi na miti ya miberoshi kadiri alivyotaka. 

11 Sulemani akampa Hiramu kori ishirini elfu za ngano, chakula cha watu wake, na kori ishirini za mafuta safi. Ndizo Sulemani alizompa Hiramu mwaka kwa mwaka”.

Lakini tunasoma Hiramu, Mfalme wa Tiro hakupendezwa na miji hiyo 20 iliyokuwa kaskazini mwa Israeli (Galilaya, mpakani na Tiro), na biblia haijataja sababu za yeye kutopendezwa na miji hiyo, huenda pengine aliona si mizuri na yeye alitegemea kupewa miji mingine mizuri yenye kupendeza, ambayo huenda ipo katikati ya Israeli.

Na kwasababu hakupendezwa nayo, aliipokea tu hivyo hivyo, na kuiita “miji isiyo na faida” yaani “Kabuli”

Lakini yote katika yote biblia haijaelezea kwa kina sababu ya Sulemani kufanya vile, au sababu ya Hiramu, Mfalme wa Tiro kutopendezwa nayo na hata kuiita nchi ya Kabuli (Maana yake isiyofaa kitu).

Ni nini tujajifunza kupitia habari hiyo na miji hiyo?.

Tunachoweza kujifunza ni kuwa tunapotenda wema “tusitegemee malipo kutoka kwa wanadamu, bali kutoka kwa Mungu”. Malipo ya wanadamu siku zote yana mapungufu mengi.

Mfalme huyu wa Tiro, alikuwa ni mtu mwema sana kuliko wafalme wote waliowahi kutokea Tiro, na zaidi sana alikuwa ni rafiki yake Mfalme Daudi, baba yake Sulemani, na hata alivyosikia kuwa Sulemani anataka kumjengea Mungu nyumba alifurahi sana na kumtukuza Mungu wa Israeli, (1Wafalme 5:7) hivyo akamtia nguvu Sulemani kwa sehemu kubwa sana, lakini pamoja na hayo alitazamia kupewa thawabu nyingi (malipo mengi) kutoka kwa Sulemani, kwasababu alijua Sulemani alikuwa Tajiri sana, Zaidi ya wafalme wote duniani, lakini kinyume chake akapewa vichache tofauti na alivyotegemea, hivyo moyo wake ukauma!, lakini Laiti kama angetegemea vichache ni wazi kuwa asingeumia kwa vile alivyopewa badala yake angeshukuru na thawabu yake ingezidi kuwa kubwa mbele za Mungu.

Hivyo na sisi hatupaswi kutegemea malipo kutoka kwa watu, pale tunapotenda wema bali tunapaswa tuwe na nia ya kiasi, ili wakati wa Bwana ukifika tupate thawabu kulingana na kile tulichokitenda.

Bwana atubariki.

Maran atha.

Pia Kwa maombezi/ Ushauri/ Maswali/ Whatsapp:
Tuandikie katika BOXI la Maoni hapo chini au
Piga namba hizi: +255789001312 au +255693036618 Jiunge na magroup yetu ya whatsapp kwa kubofya hapa > WHATSAPP-Group

Mafundisho mengine:

Miji ya Tiro na Sidoni ni miji gani kwasasa?

Kwanini Herode aliwakasirikia watu wa Tiro na Sidoni? (Matendo 12:20)

Je! Sulemani alienda mbinguni?

Je Mungu anaketi katika giza? (1Wafalme 8:12)

VITABU VYA BIBLIA: Sehemu ya 14 (Yoeli, na Obadia).

Rudi nyumbani

DOWNLOAD PDF
WhatsApp

Source URL: https://wingulamashahidi.org/2023/12/07/nchi-ya-kabuli-ndio-nchi-gani-kwasasa-na-kwanini-iliitwa-hivyo-1wafalme-913/