BWANA ANASAMEHE.

by Admin | 2 January 2024 08:46 pm01

Jina la Bwana na Mwokozi Mkuu YESU KRISTO lihimidiwe, karibu tujifunze biblia, Neno la Mungu wetu lililo hai, ambalo ndilo taa na mwanga wa njia yetu ya kwenda mbinguni (Zab.119:105).

Moja ya hubiri kubwa na kongwe la shetani, ni kuwahubiria watu kuwa “MUNGU HASAMEHI na ANACHUKIA WATU”.

Fundisho hili ni silaha kubwa sana ya kumfanya mtu asijaribu kumtafuta Mungu, au hata kama alikuwa ameshaanza hatua za kuutafuta uso wa Mungu, basi akate tamaa njiani. Anajua mtu akifahamu kuwa anaweza kusamehewa na Mungu basi hatampata tena, na yeye anataka watu waendelee kudumu katika dhambi ili hatimaye waukose uzima wa milele kama yeye alivyoukosa.

Sasa sifa moja kuu ya MUNGU aliyeumba mbingu na nchi, ni MSAMAHA. Maana yake “anatoa msamaha hata kwa mtu asiyestahili kusamehewa”.. Na hii ndio sifa ya kwanza inayomfanya yeye (MUNGU) kutisha!..na wala si tu yale matendo ya miujiza aliyoyafanya kule Misri, au anayoendelea kuifanya hata sasa, ambayo kimsingi tunadhani hayo ndiyo yanayomfanya Mungu atishe.

Muujiza Mkuu na wa kwanza unaomfanya Mungu kutisha, ni KUSAMEHE NDAMBI, na KUZIONDOA KABISA NDANI YA MTU.

Zaburi 130:3 “Bwana, kama Wewe ungehesabu maovu, Ee Bwana, nani angesimama?

4 Lakini kwako kuna msamaha, ILI WEWE UOGOPWE”.

Je! Unajihisi wewe ni mwenye dhambi, na unahisi dhambi yako haifutiki??…fahamu kuwa MUNGU kuna msamaha, na sio tu msamaha bali pia na ondoleo la dhambi, kiasi kwamba baada ya kusamehewa Mungu anaondoa mpaka msingi wa hiyo dhambi, kiasi kwamba wakati mwingine haitakuwa na nguvu juu yako.

Je unahisi mauaji uliyoyafanya hayawezi kusameheka?, je unahisi mawazo uliyowaza au unayowaza hayana msamaha?, je unahisi tendo ulilolifanya na tena umelirudia mara nyingi nyingi halina msamaha?..kama hayo mawazo yapo ndani yako basi fahamu kuwa ni adui ndiye anayekuambia hivyo.

Yote uliyoyafanya yanasameheka ikiwa utataka Bwana akusamehe!. Unachopaswa kufanya ni kutubu tu kwa kumaanisha kuacha hayo unayoyafanya, Ikiwa utatubu kweli kwa kumaanisha, basi kwa IMANI amini kuwa Mungu kashakusamehe, hauhitaji kutokewa na Malaika na akamwambie kwamba umesamehewa, wewe Amini tu, kwasababu ndivyo biblia inavyotufundisha kwamba “tuenende kwa Imani na si kwa kuona” (2Wakorintho 5:7).

Na ukishaamini namna hiyo, basi Mungu kashakusamehe lile kosa au yale makosa uliyoyafanya hata kama uliyafanya kwa kurudia rudia mara 100, tayari atakusamehe deni yako yote. Lakini kumbuka msamaha si ondoleo!.. Mtu anaweza kukusamehe tusi ulilomtukana, lakini kama ile roho ya kutukana haijaondoka ndani yako basi unaweza kurudia tena kesho na kesho kutwa kumtukana matusi yale yale.

Kwahiyo ili lile kosa lisijirudie rudie tena katika maisha yako, linahitaji kuondolewa kwa mizizi yake ndani yako. Sasa kanuni ya kuondoa mzizi wa dhambi ndio shetani amewafumba watu macho wasiione.

Lakini ashukuriwe Mungu kwasababu ipo wazi katika maandiko.

Tusome,

Matendo 2:37 “Walipoyasikia haya wakachomwa mioyo yao, wakamwambia Petro na mitume wengine, Tutendeje, ndugu zetu?

38  Petro akawaambia, TUBUNI MKABATIZWE KILA MMOJA KWA JINA LAKE YESU KRISTO, MPATE ONDOLEO LA DHAMBI ZENU, nanyi mtapokea kipawa cha Roho Mtakatifu”.

Hapa Petro anawaonyesha hawa Makutano, kanuni ya KUONDOA MZIZI wa dhambi ndani yao, baada ya wao KUTUBU dhambi,  kwamba WAKABATIZWE KWA JINA LAKE YESU KRISTO. Kama ishara ya kuuvua utu wa kale na kuuvaa utu upya, na kwa ishara hiyo ya maji basi ule mzizi wa dhambi utaondoka ndani yao, zile dhambi za kujirudia rudia zitakoma, kwahiyo mtu wa Mungu anabaki huru mbali na dhambi.

Na tena Mungu wetu kwa upendo wake anatuongezea na zawadi ya Roho Mtakatifu, ndani yetu kama Muhuri wa Mungu kwa kile tulichokitubia.

Je bado umezishikilia dhambi zako? Kwanini usiungame leo kwa kutubu na kubatizwa?. Na kumbuka ungamo sahihi ni lile la kutubu kwa kumaanisha, na ubatizo sahihi ni ule wa maji mengi na kwa jina la BWANA YESU KRISTO, Kutubu kusikotoka moyoni, na ubatizo usio sahihi haviwezi kuleta matokeo yoyote kwa mtu.

Bwana akubariki.

Ikiwa utahitaji msaada katika kuongozwa sala ya Toba, au ubatizo basi waweza wasiliana nasi na tutakusaidia katika hilo.

Maran atha!

Tafadhali shea na wengine ujumbe huu;

Pia Kwa maombezi/ Ushauri/ Maswali/ Whatsapp:
Tuandikie katika BOXI la Maoni hapo chini au
Piga namba hizi: +255789001312 au +255693036618

Mafundisho mengine:

NINI MAANA YA KUTUBU

TAFUTA MSAMAHA HALISI, NA SI MSAMAHA TU!

BABA UWASAMEHE

UMEONDOLEWA DHAMBI?

KUTUBU SIO KUOMBA REHEMA.

Rudi nyumbani

DOWNLOAD PDF
WhatsApp

Source URL: https://wingulamashahidi.org/2024/01/02/bwana-anasamehe/