AMEFANYIKA BORA KUPITA MALAIKA!

by Admin | 27 April 2019 08:46 pm04

Luka 24:1 ‘‘Hata siku ya kwanza ya juma, ilipoanza kupambazuka, walikwenda kaburini, wakiyaleta manukato waliyoweka tayari.

2 Wakalikuta lile jiwe limevingirishwa mbali na kaburi,

3 Wakaingia, wasiuone mwili wa Bwana Yesu.

4 Ikawa walipokuwa wakifadhaika kwa ajili ya neno hilo, tazama, watu wawili walisimama karibu nao, wamevaa nguo za kumeta-meta;

5 nao walipoingiwa na hofu na kuinama kifudifudi hata nchi, hao waliwaambia, Kwa nini mnamtafuta aliye hai katika wafu?

6 Hayupo hapa, amefufuka. Kumbukeni alivyosema nanyi alipokuwa akaliko Galilaya,

7 akisema, Imempasa Mwana wa Adamu kutiwa mikononi mwa wenye dhambi, na kusulibiwa, na kufufuka siku ya tatu’’.

Waebrania 1:4 ' amefanyika bora kupita malaika, kwa kadiri jina alilolirithi lilivyo tukufu kuliko lao'.Mambo yote yalimalizika siku ile Bwana aliyokata roho, pale aliposema IMEKWISHA!!..Hapo ndio ilikuwa mwisho wa mambo yote, ni sawa na mwanafunzi aliyemaliza mtihani wake wa mwisho wa kuhitimu siku ile anapoweka kalalmu yake chini ..Siku hiyo ndio mwisho wa mambo yake yote yahusuyo shule.

Na Bwana katika siku ile ya Ijumaa, ndio ulikuwa mwisho wa Majaribu yake yote, mwisho wa kazi yake yote, Hivyo mwisho wa majaribu yake ndio ulikuwa mwanzo wa ukombozi wetu! NA Heshima yetu sisi..Haleluya. Siku ile alimaliza yote aliyopaswa kufanya, maumivu, dhiki, taabu, uchungu na kila kitu! Ndio vilikuwa mwisho pale…akaweka rekodi ulimwenguni ya kuwa mwanadamu aliyeishi mpaka kufa bila kutenda dhambi hata moja!..Na kuthibitisha mbele za Mungu kuwa mwanadamu anaweza kuishi pasipo dhambi, Maisha yake yote mpaka kufa, Na ndio maana maandiko yanasema ‘amefanyika bora kupita malaika.

Waebrania 1:4 ‘ amefanyika bora kupita malaika, kwa kadiri jina alilolirithi lilivyo tukufu kuliko lao’.

Ikiwa na maana kuwa Hakuna malaika yoyote ambaye alishawahi kuwa mkamilifu kama yeye.

Wengi hatujui kuwa malaika nao walijaribiwa kama tunavyojaribiwa sisi, na wapo walioshinda na wapo walioshindwa, walioshinda ndio hao wapo mbinguni sasa, na walioshindwa ndio hao ambao wapo upande wa shetani..Kwahiyo miongoni mwa walioshinda pia wametofautiana ngazi, wapo waliofanya vizuri Zaidi ya wengine..sisi wanadamu hatuwajui ni yupi aliyefanya vizuri Zaidi ya mwingine, pengine tutajua tukishafika huko juu, tutakapopewa miili ya utukufu ya kufanana na wao. Sasa miongoni mwa hao waliofanya vizuri,

 hakuna aliyefanya vizuri Zaidi ya Bwana wetu Yesu Kristo.

Na kwasababu Mungu hana upendeleo, yeyote aliyefanya vizuri ndiye atakayepewa thawabu kubwa Zaidi. Kwahiyo kwasababu Bwana alifanya vizuri kuliko malaika wote wa mbinguni basi,Mungu akampa Jina ambalo, hakuna mtu aliyewahi kuwa nalo tangu ulimwengu kuumbwa, na Zaidi ya yote akapewa vitu vyote vya mbinguni na vya duniani..Akakabidhiwa mamlaka yote ya mbinguni na duniani juu ya watu wote..kwamba kila goti lipigwe mbele zake. Utasema ni wapi kwenye biblia jambo hilo lipo..soma.

Wafilipi 2: 5 ‘’Iweni na nia iyo hiyo ndani yenu ambayo ilikuwamo pia ndani ya Kristo Yesu;

6 ambaye yeye mwanzo alikuwa yuna namna ya Mungu, naye hakuona kule kuwa sawa na Mungu kuwa ni kitu cha kushikamana nacho;

7 bali alijifanya kuwa hana utukufu, akatwaa namna ya mtumwa, akawa ana mfano wa wanadamu;

8 tena, alipoonekana ana umbo kama mwanadamu, alijinyenyekeza akawa mtii hata mauti, naam, mauti ya msalaba.

9 Kwa hiyo tena Mungu alimwadhimisha mno, akamkirimia Jina lile lipitalo kila jina;

10 ili kwa jina la Yesu kila goti lipigwe, la vitu vya mbinguni, na vya duniani, na vya chini ya nchi;

11 na kila ulimi ukiri ya kuwa YESU KRISTO NI Bwana, kwa utukufu wa Mungu Baba’’.

Na kwasababu sisi tuliomwamini ni ndugu zake, hivyo hawezi kutuacha chini, ni lazima nasi pia tutamiliki naye, malaika watakuwa chini yetu, kwasababu yeye yupo juu ya malaika wote sharti na sisi tuliokolewa tuwepo naye..Ni sawa na kijana apambane mpaka aipate nafasi ya uraisi, ndugu zake kwa namna moja au nyingine watafika tu ikulu mahali anapokaa..mama yake na baba yake watamtembelea hata ikiwezekana kulala kule,na hiyo ni kwasababu tu wale ni ndugu zake! na si kingine kingine..

Kadhalika na Bwana Yesu kwa Haki yake ambayo imemfanya kupewa mamlaka yote ya mbinguni na duniani, na kupewa enzi yote na kuketi katika kile kiti cha enzi, sasa sisi ndugu zake (ambao ni wanadamu na si malaika) hawezi kututupa, kwa namna moja au nyingine tutafika tu pale alipo haleluya!! Ndio maana kuna umuhimu sana wa kuwa ndugu wa damu wa Bwana wetu Yesu Kristo nikimaanisha ndugu wa kuzaliwa mara ya pili.

Kwasababu hakuna njia yoyote ya kumkaribia yeye kama hatutazaliwa mara ya pili kwa damu yake!! Kumbuka si kwa damu ya mwanadamu bali kwa damu yake, sio kwa mapenzi ya mwili bali kwa mapenzi yake..wengi wanatenda mema na kufanya mambo mazuri na kusema kwa matendo yangu haya lazima nitamwona Mungu, ndugu yangu usidanganyike…

Unaweza ukatenda matendo mazuri kuliko mkristo yeyote duniani na bado usimkaribie Mungu hata kidogo…kwanini iwe hivyo? Jibu ni rahisi ni kwasababu wewe sio ndugu wa damu wa yule mhusika, kwahiyo matendo yako mazuri ni bure!.

Ndugu yangu kama wewe ni muislamu unasoma ujumbe huu, au mkristo ambaye bado hujayajua vizuri mamlaka Bwana Yesu aliyopewa na vigezo vya kuwa mrithi pamoja naye, na unasema moyoni ninasaidia masikini, ninawaheshimu wazazi, sidhulumu, sifanyi hichi sifanyi kile, ukijidanganya kuwa kwa mambo hayo tu upo karibu na Mungu na huku umemweka Kristo nyuma

Hujazaliwa mara pili katika damu yake, napenda nikuambie ndugu yangu UNAPOTEZA MUDA!!!! Matendo yako ni mazuri lakini hayatakusaidia huko mbeleni. Huko mbeleni ni UNDUGU ndio utakaojalisha kwanza na kisha ndio matendo yafuate!..Ni sawa na kwenda kumfanyia boss wako mema yote unayoyajua duniani na kumpendeza kwa viwango vyote ukitumai kuwa siku moja atakurithisha kampuni lake!!…hilo katika akili yako lifute, kwasababu hawezi kuacha kumrithisha mtoto wake (damu yake) akurithishe wewe?..hata kama mwanawe hana tabia nzuri kama za kwako, hata kama wewe ni mchapa kazi kuliko yeye, siku moja huyo mtoto atakuja kuwa boss wako tu…kwanini?? Kwasababu ya uhusiano wa kidamu uliopo kati ya yule mtoto na baba yake!!.

Na ufalme wa Mbinguni ndio upo hivyo hivyo, ndio maana ufalme wa mbinguni unaitwa URITHI, sio UTAHIFISHWAJI, hapana bali URITHISHWAJI, wanarithishwa WANA WA MUNGU tu. Kumbuka pia ufalme wa mbinguni haukuanza siku ile Bwana Yesu aliposulibiwa, ufalme wa mbinguni ulikuwepo kabla hata ya dunia kuumbwa, ni kitu kinachoendelea, kwahiyo kitakachotokea ni urithishwaji, Na wana wa Mungu ndio watakaourithi, na wana wa Mungu ni wale wote waliomwamini Yesu Kristo na kumpokea kwa kuzaliwa mara ya pili.

Yohana 1:12 ‘Bali wote waliompokea aliwapa uwezo wa kufanyika watoto wa Mungu, ndio wale waliaminio jina lake;

Kwahiyo ndugu yangu, siku ya leo (SIKU YA BWANA KUFUFUKA). Ni siku ya muhimu sana,Bwana anapowatembelea wengi duniani kuwapa wokovu asikupite na wewe. Kama hujazaliwa mara ya pili, huu ni wakati mzuri wa kufanya hivyo…Utauliza unazaliwaje mara ya pili?…Biblia imetupa majibu, kuwa hatuwezi kurudi tena kwenye matumbo ya mama zetu na kuzaliwa tena!!..Kuzaliwa mara ya pili ni lugha ya rohoni, yenye maana ya kufanyika upya kwa Maisha yako ya kiroho, yaani kugeuzwa na kuwa mwingine katika mwelekeo wako wa kiimani.

Hiyo ndio maana ya kuzaliwa mara ya pili. Tunasema Taifa ya Tanganyika lilizaliwa mwaka 1961, haimaanishi liliingia tumboni kwa mama yake na kuzaliwa hapana! Bali ni lugha tu inayomaanisha, kuwa lilifanyika upya kidemokrasia na kuwa taifa huru linalojitegemea mwaka huo. Na katika Imani ya kikristo ndio hivyo hivyo, unapofanyika upya kifikra kwa nguvu za kiMungu, unakuwa umezaliwa mara ya pili. Na zipo hatua chache za kufanyika upya huko…

Yohana 3:1 ”Basi palikuwa na mtu mmoja wa Mafarisayo, jina lake Nikodemo, mkuu wa Wayahudi.

2 Huyo alimjia usiku, akamwambia, Rabi, twajua ya kuwa u mwalimu, umetoka kwa Mungu; kwa maana hakuna mtu awezaye kuzifanya ishara hizi uzifanyazo wewe, isipokuwa Mungu yu pamoja naye.

3 Yesu akajibu, akamwambia, Amin, amin, nakuambia, MTU ASIPOZALIWA MARA YA PILI, HAWEZI KUUONA UFALME WA MUNGU.

4 Nikodemo akamwambia, Awezaje mtu kuzaliwa, akiwa mzee? Aweza kuingia tumboni mwa mamaye mara ya pili akazaliwa?

5 Yesu akajibu, Amin, amin, nakuambia, MTU ASIPOZALIWA KWA MAJI NA KWA ROHO, HAWEZI KUUINGIA UFALME WA MUNGU.

6 Kilichozaliwa kwa mwili ni mwili; na kilichozaliwa kwa Roho ni roho.

7 Usistaajabu kwa kuwa nilikuambia, Hamna budi kuzaliwa mara ya pili”.

Kwahiyo hatua za kufuata ili uwe umezaliwa mara ya pili baada ya kumwamini Bwana Yesu Kristo kuwa ni mkombozi wa ulimwengu, na kuwa yeye ndiye aliyeshinda kila kitu, na kukabidhiwa mamlaka yote ya mbinguni na duniani, hatua inayofuata ni kwenda kubatizwa katika maji mengi na kwa jina lake (Yesu Kristo), kuwa kwako kama ishara ya kufa na kufufuka na Kristo, (huko ndio kuzaliwa kwa maji Bwana alikokuzungumzia) na baada ya kubatizwa Bwana Mwenyewe atakupa kipawa cha Roho wake Mtakatifu ndani yako atakayekusaidia kushinda dhambi, na kukuongoza katika kuijua kweli yote ya maandiko, na kukulinda, (Huko ndiko kuzaliwa kwa Roho).

Sasas ukikamilisha hatua hizo tatu, yaani kuamini, kubatizwa kwa maji, na kubatizwa kwa Roho Mtakatifu…Utakuwa tayari umezaliwa mara ya pili, umefanyika kiumbe kimpya , nawe unakuwa ni mwana wa Mungu, mrithi wa Mungu.ya kale yote yamepita, Tazama yamekuwa mapya,(2 Wakoritho 5:17) Unakuwa ni NDUGU wa Bwana WETU YESU KRISTO, wa Damu kabisa…Unakuwa mrithi wa ahadi za Mungu, hakuna atakayeweza kukushtaki kuanzia wakati huo, wala hakuna atakayeweza kukutenga na upendo wake…

Ndugu Kwasasa hatuujui vizuri kwa mapana na marefu urithi huo, tunajua kwa sehemu tu! Lakini baada ya maisha haya kuisha, ndipo tutakapomfurahia Mungu, tutamjua kwa mapana na marefu utajiri aliotupa na heshima aliyotuheshimu nayo, kwa kupitia mwanawe mpendwa YESU KRISTO.

Ni maombi yangu kuwa katika msimu huu wa pasaka, Utatambua maana yake katika maisha yako, na pia utafanya maamuzi Mema na ya Busara na Bwana akusaidie.

Mawasiliano: +255693036618

Na pia kama utapenda masomo haya yawe yanakufikia kila siku kwa njia ya Whatsapp  Pia unaweza ukapata mafundisho haya Kwa njia ya Whatsapp yako, jiunge na channel yetu Kwa kubofya hapa >> WHATSAPP


Mada Zinazoendana:
BASI MUNGU AKAMUADHIMISHA SANA.
MBINGUNI YUPO NANI SASA?
MAUTI YA PILI NI NINI?
KUOTA UNAJIFUNGUA.
LAKINI WAKATI WA TAABU WATASEMA, SIMAMA UKATUOKOE.
UAMINIFU NI KIGEZO KIKUBWA CHA KUTUMIWA NA MUNGU.
Nifanyeje niwe mwombaji mzuri, wa masafa marefu?

Rudi Nyumbani

DOWNLOAD PDF
WhatsApp

Source URL: https://wingulamashahidi.org/2019/04/27/amefanyika-bora-kupita-malaika/