Hapa ana maana gani kusema hivi? ” Usiseme moyoni mwako,Ni nani atakayepanda kwenda Mbinguni? (yaani ni kumleta Kristo chini), “au,Ni nani Atakayeshuka kwenda Kuzimu? (yaani, ni kumleta Kristo juu,kutoka kwa wafu.). {Warumi10:6-7.}

by Admin | 2 September 2019 08:46 pm09

JIBU: Ukisoma kuanzia hiyo mistari wa kwanza wa kitabu cha Warumi Mlango wa 10, Utaona kuwa Mtume Paulo alikuwa anazungumza habari za juu ya Wayahudi ambao wanaamini katika kuhesabiwa haki kwa matendo ya sheria na wala sio kwa Imani.   Sasa Mtume Paulo alichokuwa anataka kuonyesha ni kwamba..Torati Musa aliyopewa na Mungu, imezungumza habari zote mbili yaani habari ya kuishi kwa sheria kwamba Mtu akiitenda sheria zilizoandikwa katika mbao zile ataishi katika hizo..Yaani Mtu akifanya maagizo yote ya torati basi atafanikiwa katika maisha yake.. Na pia torati hiyo hiyo mahali pengine pia imezungumzia kuhusu haki ipatikanayo kwa njia ya Imani kwamba..

Sheria za Mungu zikiandikwa ndani ya moyo wa mtu basi naye pia atabarikiwa zaidi..Kwasababu maana halisi ya agano jipya ni kuwa zile zile sheria za Mungu zinakuwa zinaandikwa ndani ya Moyo wa Mtu.   Sasa ukisoma Kitabu cha kumbukumbu utaona Mungu anaizungumzia hiyo Mtume Paulo aliyoinukuu.

Kumbukumbu 30: 11 “Kwa maana maagizo haya nikuagizayo leo, si mazito mno kwako, wala si mbali.

12 Si mbinguni, hata useme, Ni nani atakayetupandia mbinguni akatuletee, aje atuambie tusikie, tupate kuyafanya?

13 Wala si ng’ambo ya pili ya bahari, hata useme, Ni nani atakayetuvukia bahari, akatuletee, aje atuambie, tusikie, tupate kuyafanya?

14 Lakini neno li karibu nawe sana, li katika kinywa chako na moyo wako, upate kulifanya.

15 Angalia, nimekuwekea leo mbele yako uzima na mema, na mauti na mabaya”

Unaona Haki ipatikanayo kwa njia ya Imani kwamba sheria za Mungu zitakuwa karibu sana na mtu mahali alipo, hazipo mbinguni kwamba Bwana Yesu aende akatuchukulie atuletee katika gari la moto, au hazipo kuzimu kwamba Bwana Yesu azifuate atuletee katika mbao kama Musa alivyozileta katika mbao kwa wana wa Israeli ili wazishike.. Hapana sheria zake ataziandika ndani yetu (ndani ya mioyo yetu)..zipo karibu sana na sisi, hakuna haja ya kwenda milimani kuzitafuta kama alivyofanya Musa, wala hakuna haja ya kusubiria mtu atoke mbinguni au kuzimu kutufundisha…yeye Bwana ataziandika mioyoni mwetu kutufundisha mwenyewe..

Hiyo ndiyo maana ya huo mstari.. “Usiseme moyoni mwako,Ni nani atakayepanda kwenda Mbinguni? (yaani ni kumleta Kristo chini), “au,Ni nani Atakayeshuka kwenda Kuzimu? (yaani, ni kumleta Kristo juu,kutoka kwa wafu.) Lakini yanenaje? Lile neno li karibu nawe, katika kinywa chako, na katika moyo wako; yaani, ni lile neno la imani tulihubirilo”   Mtume Paulo alielezea vizuri zaidi juu ya agano hilo jipya katika kitabu cha 

Waebrania 8:8 “…Angalia, siku zinakuja, asema Bwana, Nami nitawatimizia nyumba a Israeli na nyumba ya Yuda agano jipya;

9 Halitakuwa kama agano lile nililoagana na baba zao, Katika siku ile nilipowashika mikono yao niwatoe katika nchi ya Misri. Kwa sababu hawakudumu katika agano langu, Mimi nami sikuwajali asema Bwana.

10 Maana hili ndilo agano nitakaloagana na nyumba ya Israeli Baada ya siku zile, asema Bwana; NITAWAPA SHERIA ZANGU KATIKA NIA ZAO, NA KATIKA MIOYO YAO NITAZIANDIKA; Nami nitakuwa Mungu kwao, Nao watakuwa watu wangu.

11 Nao hawatafundishana kila mtu na jirani yake, Na kila mtu na ndugu yake, akisema, Mjue Bwana; Kwa maana wote watanijua, Tangu mdogo wao hata mkubwa wao.

12 Kwa sababu nitawasamehe maovu yao, Na dhambi zao sitazikumbuka tena”

Ubarikiwe!


Mada Nyinginezo:

NOTI YA UFALME WA MBINGUNI

AMEFANYIKA BORA KUPITA MALAIKA!

JINSI EDENI ILIVYOKUWA.

MAVAZI YA NDANI NA YA NJE.

KAMA MWIZI USIKU WA MANANE:

MADHARA YA DHAMBI YA UASHERATI.


 

Rudi Nyumbani:

DOWNLOAD PDF
WhatsApp

Source URL: https://wingulamashahidi.org/2019/09/02/hapa-ana-maana-gani-kusema-hivi-usiseme-moyoni-mwakoni-nani-atakayepanda-kwenda-mbinguni-yaani-ni-kumleta-kristo-chini-auni-nani-atakayeshuka-kwenda-kuzimu-yaani-ni-kuml/