Je kunena kwa Lugha mpya kukoje?

by Admin | 2 September 2019 08:46 pm09

Swali: Je hizi lugha ni zipi, na je! ni lazima kila mkristo aliyepokea Roho Mtakatifu anene kwa lugha mpya

JIBU: Hili ni moja ya jambo linalowachanganya wengi sana, Na nilinichanganya hata mimi pia kwa muda mrefu, na lingine linalofanana na hili ni juu ya uthibitisho halisi wa mtu kuwa amepokea Roho Mtakatifu ni upi?..

Lakini napenda ufahamu kuwa tukiweza kutofautisha kati ya hivi vitu viwili yaani “vipawa vya Roho Mtakatifu” na “Roho Mtakatifu” mwenyewe tutaweza kuondoa huu utata kwa sehemu kubwa sana.. Biblia inasema Kunena kwa lugha ni moja ya karama ya Roho Mtakatifu kama zilivyokarama nyingine, mfano Unabii, miujiza, uponyaji, ualimu, uinjilisti n.k. Lakini hatutaenda sana huko turudi kwenye msingi wa swali letu linalouliza juu ya Kunena kwa Lugha. Tukirudi nyuma kidogo kabla siku ile Bwana Yesu kupaa, aliorodhesha baadhi ya ishara ambazo zitaambata na wale wote waliomwamini na mojawapo ya ishara hizo alisema watanena kwa lugha mpya.

Marko 16:17 “Na ishara hizi zitafuatana na hao waaminio; kwa jina langu watatoa pepo; watasema kwa lugha mpya;

18 watashika nyoka; hata wakinywa kitu cha kufisha, hakitawadhuru kabisa; wataweka mikono yao juu ya wagonjwa, nao watapata afya”.

Sasa Neno “Lugha mpya”, ni Neno lisilo na mipaka (Halifungiki), yaani kwa ufupi Lugha yoyote usiyoijua wewe ukiinena kwako ni Lugha mpya, iwe ni ile iliyopo katika nchi yako, au nje ya nchi yako, au iwe ya ulimwengu huu au sio ya ulimwengu huu maadamu hauitambui bado kwako ni Lugha mpya. Hivyo ukisoma maandiko utaona ulikuwa ni mpango wa Roho Mtakatifu tangu zamani, kuwa utafika wakati atazungumza na watu wote wa ulimwenguni kwa lugha tofauti, unabii huo unaweza kuusoma katikaIsaya 28: 11 “La, bali kwa midomo ya watu wageni, na kwa lugha nyingine atasema na watu hawa;”Sasa utagundua kumbe lengo la kwanza Roho Mtakatifu kusema kwa lugha gheni katikati ya watu ni ili kuwavuta kwake wamwamini.

Hapa ni lazima atumie lugha za kibinadamu, Mfano dhahiri ni kile kilichotokea Siku ile ya Pentekoste, Walijikuta wote wanazungumza Lugha za mataifa mengine ya mbali na wale waliokuwa wanasikia wote walishikwa na butwaa na kusema hakika haya matendo makuu ya Mungu..Na kwa kitendo kile tu maelfu ya watu walivutwa Kwa Kristo.Na jambo hili liliendelea kwa muda mrefu sana.

Na pia kusudi la pili la lugha hizi Roho Mtakatifu kuziachia duniani ni ili kudhihirisha uwepo wake katikati ya waaminio, Hapa ndipo mtu anajikuta ananena lugha asiyoifahamu kwa uweza wa Roho wa Mungu..kuna Lugha za kimbinguni pia, ambazo hizo hazina matunda yoyote kwa watu wasioamini, na ndio maana Mtume Paulo alionya akasema ikiwa mtu atajikuta katika hali kama hii basi na anyamaze na anene na nafsi yake mwenyewe na Mungu wake kwa jinsi anavyojaliwa, vinginevyo ataonekana kama mwendawazimu kama akifanya hivyo katikati ya watu wasioamini, na Mungu sikuzote ni Mungu wa utaratibu. (1Wakorintho 14:28).

Fikiri mtu asiyeujua kabisa Ukristo, anaingia kanisani ghafla anashangaa watu wanaanza kuzungumza lugha zisizoeleweka…moja kwa moja atahisi amekutana na watu pengine ni wendawazimu au wanaabudu miungu..lakini akiingia na kusikia lugha yake pale inaongelewa katika ufasaha wote na anayeiongea sio hata wa jamii ya watu wake..Na maneno anayoongea ni ya kumtukuza Mungu..atashangaa sana na kuogopa kusema huu ni muujiza?..na hivyo atajua mahali pale kuna uwepo Fulani wa kiMungu na hivyo atatubu na kumgeukia Mungu. Na kusema kuwa kila mwaminio ni lazima anene kwa lugha mpya, kauli hiyo inapingana kabisa na maandiko.

Kumbuka kuwa mtu haneni lugha kama apendavyo yeye, au ajisikiavyo yeye bali ni kama vile Roho ANAVYOMJALIA MTU KUTAMKA (Soma Matendo 2:4), kama tu vile mtu asivyoamua kuona maono mpaka Mungu amwonyeshe na lugha ndio ziko hivyo hivyo..Vinginevyo mtu utakuwa ananena tu kwa akili zake, na ndivyo watu wengi walivyofanya leo hii, ambayo yanafanya tunaonekana kama watu waliorukwa na akili..

Kunena kwa lugha ni kipawa cha Mungu na Mungu anakigawa kwa jinsi apendavyo yeye mwenyewe, mmoja atampa lugha mpya, mwingine unabii, mwingine tena uponyaji, mwingine uongozi, wingine matendo ya miujiza, mwingine kufundisha n.k..lakini wote hatuwezi kuwa manabii, au wote waalimu au wote wenye kufanya matendo ya miujiza au wote wenye kunena kwa lugha au wote wachungaji.

1Wakorintho 12.27 “Basi ninyi mmekuwa mwili wa Kristo, na viungo kila kimoja peke yake.

28 Na Mungu ameweka wengine katika Kanisa, wa kwanza mitume, wa pili manabii, wa tatu waalimu, kisha miujiza, kisha karama za kuponya wagonjwa, na masaidiano, na maongozi, na aina za lugha.

29 Je! Wote ni mitume? Wote ni manabii? Wote ni waalimu? Wote wanatenda miujiza?

30 Wote wana karama za kuponya wagonjwa? WOTE WANENA KWA LUGHA? Wote wafasiri?.”

Na jambo lingine la muhimu la kufahamu ni kuwa mtu anaweza kuwa na ananena kwa lugha mpya lakini bado asiwe na Roho Mtakatifu ndani yake, kama tu vile mtu anaweza akawa ni nabii, akaona maono yote duniani, na asiwe nabii wa kweli, kama tu vile mtu anaweza akaponya magonjwa kwa karama Mungu aliyompa na kufanya miujiza mingi isiyokuwa ya kawaida na bado Kristo asimtambue.(Mathayo 7:21). 

Hivyo usijisifie karama, kwasababu Roho Mtakatifu sio karama yeye ni zaidi ya hicho, ikiwa utapenda kupata maelezo marefu juu ya uthibitisho fasaa unaomtambulisha mtu kuwa amepokea Roho Mtakatifu atanitumia ujumbe inbox, nikutumie somo lake.

Hivyo kwa kumalizia ikiwa wewe ni mmojawapo wa waliokirimiwa kipawa hichi Unaponena kwa lugha mwombe pia Mungu akupe kutafsiri, Sehemu hii inaonekana kwa wachache katika kanisa lakini ndio inayofaa zaidi, kuliko kunena tu maneno yasiyojulikana kanisani mbele ya watu, kwasababu hilo linaweza kuwa na manufaa tu kwako mwenyewe lakini lisiwe na msaada wowote kwa wengine.

Lakini kama litaambatana na tafsiri hilo linafaa sana na lina nguvu kwasababu linalijenga kanisa la Kristo kwa ujumla.

1Wakorintho 14:27 “Kama mtu akinena kwa lugha, wanene wawili au watatu, si zaidi, tena zamu kwa zamu, na mmoja na afasiri.

28 Lakini asipokuwapo mwenye kufasiri na anyamaze katika kanisa; aseme na nafsi yake tena na Mungu.”

Jivunie karama yako ikiwa inalijenga kanisa la Kristo, na sio kwa kujionyeshea kuwa ni hodari wa kunena, Mtume Paulo alijisifia zaidi ya mtu yoyote, lakini alisema ni heri anene maneno matano lakini yanalifaa kanisa kuliko kunena maneno Elfu kwa lugha.

Bwana akubariki.

[embedyt] https://www.youtube.com/watch?v=-v8ToQZwJho[/embedyt]


Mada zinazoendana:

JE! NI LAZIMA WATU WOTE WANENE KWA LUGHA?

JE! KARAMA NI UTHIBITISHO WA KUWA NA MUNGU?

JE! UMEPOKEA KWELI ROHO MTAKATIFU?

UPEPO WA ROHO.

ROHO MBAYA KUTOKA KWA BWANA.

SEHEMU ISIYO NA MAJI.


Rudi Nyumbani:

DOWNLOAD PDF
WhatsApp

Source URL: https://wingulamashahidi.org/2019/09/02/je-kunena-kwa-lugha-mpya-kukoje-na-hizi-lugha-ni-zipi-na-je-ni-lazima-kila-mkristo-aliyepokea-roho-mtakatifu-anene-kwa-lugha-mpya/