MWENDO UNAOSHANGAZA SANA!

by Admin | 2 September 2019 08:46 pm09

Tukisoma kitabu cha Mithali sura ya 30 tunamwona mtu mmoja aliyeitwa Aguri bin Yake akiandika mithali ambazo ni mahusia aliyompa mtu mmoja anayeitwa Ithieli. Kati ya mambo mengi aliyokutana nayo katika maisha yake kuna manne yaliyomshangaza sana nayo ni haya tunayoyasoma katika mstari wa 18,


Mithali 30:18 “Kuna mambo matatu yaliyo ya ajabu kwangu, Naam, kuna manne nisiyoyafahamu.

19 Mwendo wa tai katika hewa; Na mwendo wa nyoka juu ya mwamba; Mwendo wa merikebu katikati ya bahari; Na mwendo wa mtu pamoja na msichana.


Ukiisoma hii mistari kwa juu juu utaona unaweza usione jambo lolote la kushangaza, lakini ukiitafakari kwa undani utagundua kweli alivyoviona vinamshangao mkubwa sana katika mienendo yao. Hapo amevitaja vitu vine, Kwanza ni TAI, pili NYOKA, tatu MERIKEBU, na nne MTU pamoja na Mwanamke..


Aguri alitafakari kutembea kwao kukamshangaza sana, kwa mfano alimtazama Tai jinsi anavyoweza kwenda kwa kasi hewani, akaona japokuwa amepewa miguu lakini haitegemei miguu yake katika mwendo wake, leo hii hakuna mnyama yoyote wala ndege yeyote mwenye mwendo wa kasi kama Tai,Vile vile akamtazama Mnyama nyoka, ambaye nawe pia unamfahamu jinsi alivyo hana miguu, lakini nyoka kama koboko anakimbia karibia mara 2 zaidi ya mwendo ya wanadamu wengi..Hivyo Aguri akaona kumbe hata miguu sio nyenzo pekee ya kuamua mwendo wa kiumbe hai, kwamba bila hicho mambo hayawezi kwenda..


Akachunguza tena, Merikebu bahari akaona haina magurudumu kama vifaa vingine vya usafiri mfano ma gari, baiskeli, treni au pikipiki lakini inauwezo wa tembea tena kwa kasi tu..hata ingepewa matairi bado yasingeweza kumsaidia katika mwendo kasi wake, kama tu vile miguu isivyomsaidia Tai kutembea kwa kasi, na kama vile miguu isivyotumika kwa nyoka kukimbia kwa kasi, jongoo anayefanana na nyoka mwenye miguu mingi kuliko nyoka na kuliko Wanyama wengi lakini bado hawezi kukimbia..


Hivyo Aguri akamalizia kuchunguza na mwendo wa mwingine ambao ulimshangaza naamini zaidi ya yote nayo ni ni mwendo wa Mtu pamoja na msichana, hapo ukisoma katika tafsiri nyingi inaeleza kwa undani zaidi inasema jinsi mtu na msichana wanavyopendana, au mwenendo wao katika upendo.


Mara nyingi nimekutana na watu wakikosoa ndoa za wengine, labda utaona mmoja anasema mbona kulikuwa na wanawake wazuri kuliko Yule kwanini amemwoa yule bibi-kizee?, mwengine atasema kwanza alishakuwa na watoto huko nyuma ni kitu gani kilichomfanya ampendee, mwingine anatasema alikuwa ni kahaba maarufu anayejulikana mtaa mzima, imekuwaje huyu jamaa kampenda?, mwingine atasema Yule mwanaume hana mwelekeo, hana pesa Yule mwanamke kampendea nini?..Mwingine atakuwa kweli anayopesa lakini mwanamke /mwanamume Yule hakumpenda kwa ajili ya mali zake, Hayo ni maswali ambayo yapo kila mahali, Uliyempenda wewe mwingine atajiuliza ulimpendea nini?


Hilo ndio jambo linaloshangaza, kati ya wawili wapendanao. Kile kinachodhaniwa kuwa kingekuwa chanzo cha wao kuwa pamoja kinagundulika kuwa sio.


Na ndivyo ilivyo Kristo na kanisa lake..Kristo ndio Mume wa kanisa, ametuoa sisi tulio kanisa lake..


2 Wakoritho 11:2 “Maana nawaonea wivu, wivu wa Mungu; kwa kuwa naliwaposea mume mmoja, ili nimletee Kristo bikira safi.”


Yeye hakutazama kuwa sisi tulikuwa ni wachafu kiasi gani, au tulikuwa hatustahili kiasi gani?, Aliacha enzi yake na utajiri wake wote, na mamlaka yake, kuja duniani kutukomboa sisi, mambo ambayo hata malaika hawana majibu nayo, kwanini alitupenda… akatoa uhai wake kwa ajili yetu sisi tusiostahili..Ukatazama ni kitu gani kizuri alichokiona kwetu, huwezi kukiona, ukitazama ni faida gani basi ataipata kutoka kwetu huwezi kuiona, ametupenda tu kwasababu ametupenda…Huo ni mwendo wa ajabu sana.


Vivyo hivyo na Kanisa lake halisi linarudisha upendo wa namna hiyo hiyo kwake. Japo sasa hatumwoni kwa macho lakini tunampenda, wengi watajiuliza mbona huyo Yesu mnayemtumika hamumwoni? Jibu ni kwamba Upendo tulio nao kwake hautegemei macho kujidhihirisha, ni zaidi ya macho, na hata kama tutamwona kwa macho bado hatutategemea macho yetu kumpenda yeye..Kuna kitu ndani yetu kinachotufanya tutamani kuwa naye siku zote, hakielezeki kwa namna ya kibinadamu.


1Petro 1:8 “Naye mwampenda, ijapokuwa hamkumwona; ambaye ijapokuwa hamwoni sasa, mnamwamini; na kufurahi sana, kwa furaha isiyoneneka, yenye utukufu,”


Vile vile hatumpendi Bwana Yesu kwasababu ya utajiri wake,.Upendo wetu kwake ni zaidi ya hapo..


Hivyo wewe ndugu ambaye bado upo nje ya Kristo umeshajua ni kwasababu gani unaona ni ngumu kumtumikia Mungu usiyemwona au usiyetembea naye? ni kwasababu hujaingizwa bado kwenye pendo lake., Siku ukiingizwa hutahitaji macho ili kutembea naye, hutahitaji akupe kwanza kitu Fulani ndipo umpende..Kwani atajidhihirisha kwako kwa namna ya ajabu ambayo hata macho hayafikii hicho kilele.


Unasubiri nini? Yeye anasema “Onjeni mwone ya kuwa Bwana yu mwema; Heri mtu yule anayemtumaini.(Zaburi 34:8)”


Mkaribishe sasa maishani mwako aanze kutembea na wewe mwendo ambao hata watu wa nje watashangaa unawezaje kuwa naye katika hali zote, utafanyika kuwa Bibiarusi na utaingia kwenye pendo ambalo litakusangaza hata wewe ambalo hutatamani hata utoke.


Warumi 8: 38 “ Kwa maana nimekwisha kujua hakika ya kwamba, wala mauti, wala uzima, wala malaika, wala wenye mamlaka, wala yaliyopo, wala yatakayokuwapo, wala wenye uwezo,

39 wala yaliyo juu, wala yaliyo chini, wala kiumbe kinginecho chote hakitaweza kututenga na upendo wa Mungu ulio katika Kristo Yesu Bwana wetu”.


Ufunuo 22: 17 “Na Roho na Bibi-arusi wasema, Njoo! Naye asikiaye na aseme, Njoo! Naye mwenye kiu na aje; na yeye atakaye, na ayatwae maji ya uzima bure.”


Ubarikiwe.Tafadhali “Share” na kwa wengine..


Mada Nyinginezo:

JAWABU LA MAISHA YA MTU.

AYUBU 28 : HEKIMA NI NINI? NA UFAHAMU UNAPATIKANA WAPI?

MSTARI HUU UNA MAANA GANI? “YUKO MWENYE HAKI APOTEAYE KATIKA HAKI YAKE”?

DHAMBI ISIYO NA MSAMAHA.

MATUMIZI YA DIVAI.

WALIOITWA NI WENGI, ILA WATEULE NI WACHACHE.


Rudi Nyumbani:


DOWNLOAD PDF
WhatsApp

Source URL: https://wingulamashahidi.org/2019/09/02/mwendo-unaoshangaza-sana/