JINSI NEEMA YA MUNGU ILIVYOKUWA KUBWA KWA MKE WA LUTU.

by Admin | 24 February 2020 08:46 pm02

Siku zote Mungu akitaka kumuokoa mtu neema yake huwa anaizidisha sana kwa kiwango cha juu kiasi kwamba kwa nje ni rahisi kuona kama anatumia nguvu, au analazimisha ndivyo ilivyokuwa kwa Lutu na mke wake na watoto wake… Wale malaika wawili walipoona wanachelewa chelewa, wanakawia kawia waliwashika mikono yao na kuwavuta mpaka nje ya mji kwa nguvu kwa jinsi Mungu alivyowahurumia…

Mwanzo 19: 15 “Hata alfajiri ndipo malaika wakamhimiza Lutu, wakisema, Ondoka, mtwae mkeo na binti zako wawili waliopo hapa, usipotee katika maovu ya mji huu.

16 Akakawia-kawia; nao wale watu wakamshika mkono, na mkono wa mkewe, na mkono wa binti zake wawili, kwa jinsi Bwana alivyomhurumia, wakamtoa wakamweka nje ya mji.”

Lakini tendo hilo la kushikwa mikono halikuendelea milele walipofikishwa tu nje ya ule mji, wameshajua sasa yawapasayo kufanya jambo lililofuata waliambiwa..jiponyeni nafsi zetu msigeuke nyuma..Lakini Mke wa Lutu alijiharibia.

Mwanzo 19:17 “Ikawa walipomtoa nje, mmoja alisema, Jiponye nafsi yako usitazame nyuma, wala usisimame katika hilo bonde po pote; ujiponye mlimani, usije ukapotea”.

Ndugu, picha hii inatuonyesha kuwa wokovu ni tendo la neema kubwa sana, kiasi kwamba hakuna mtu anayeweza kujiokoa mwenyewe kwa nguvu zake…Na ndio maana Mungu aliona malaika hawatoshi kuja kutuokoa sisi na hukumu hiyo kubwa inayokuja huko mbele, badala yake akaamua kumtuma mwanawe kabisa , YESU KRISTO, ili aje kutuvuta sisi mbali na ile hukumu ya siku za mwisho na ziwa la moto…Yeye ndiye anayetushika mkono na kutuvusha kutoka katika ulee mji wa mauti na kutupeleka sehemu salama..

Lakini ikiwa ameshatuweka sehemu salama mbali na dunia, ni wajibu wa kila mmoja kuuthamini wokovu ule kwa kukimbia mbali zaidi na dhambi kama ilivyokuwa kwa Lutu na watoto wake..Ikiwa tulishaona mkono wa Mungu ulivyotuepua kutoka katika dhambi, hatupaswi kujilegeza tena, kusubiria tena neema itutoe kwenye dhambi tunazozitenda kwa uzembe wetu.. Tukishafikia hii hatua ni wakati wa kuziponya nafsi zetu…

Lakini embu tumtafakari mke wa Lutu ambaye ni mfano wa wale waliookolewa ambao mioyo yao bado ipo ulimwenguni, yeye alipogeuka nyuma alikuwa nguzo ya chumvi, unaweza kujiuliza ni kwanini awe nguzo ya chumvi na sio kitu kingine chochote labda tuseme nguzo ya mti, au ya chuma, au ya udongo?..Chumvi ni kiungo cha kipekee sana ambacho huwa kinadumu milele, yaani ukiihifadhi chumvi vizuri leo kwenye chupa mtu anatakaye kuja kuzaliwa miaka milioni moja mbele ataitumia na ikawa na ubora ule ule..

Na ndio maana Mungu sehemu nyingine alikuwa analifananisha Agano aliloingia na Daudi pamoja na wana wa Israeli kama agano la Chumvi, ikimaanisha kuwa ni agano la milele soma..

2Nyakati 13:5 “je! Haikuwapasa kujua ya kwamba Bwana, Mungu wa Israeli, alimpa Daudi ufalme juu ya Israeli milele, yeye na wanawe kwa agano la chumvi?”

Soma tena Hesabu 18:19..

Hivyo lile lilikuwa ni agano la kukataliwa milele kati yake na mke wa Lutu.. Hata sisi leo hii, ikiwa Bwana Yesu alishatuokoa, halafu tunauchezea wokovu wetu, leo tunaenda mbele, kesho tunarudi nyuma…hatuthamini ondoleo la dhambi tulilopewa siku ile tulipotubu bure, ..na wema wake wote Mungu aliotutenda, hatuoni kama kuokolewa kule ni jambo la bahati sana ambapo sio watu ulimwenguni wanaweza kupewa neema hiyo badala yake mguu mmoja kwa Kristo na mguu mwingine kwa shetani Tujue tu tupo hatarini kuwa MAWE YA CHUMVI katika roho..

Yaani Mungu kuingia na sisi agano la rohoni la milele kuwa hatukustahili kuokolewa na yeye, na matokeo yake ni kuwa safari yetu ya wokovu inakuwa imeishia pale pale, tunakuwa tumekufa,japo kwa nje tunaonekana tupo hai..Kumbuka hilo ni agano la milele, maana yake ni kuwa Mungu hatakaa akupokee wewe tena milele kwasababu ile nguvu ya kukuvuta kwake inakuwa haipo tena…utaendelea na ubaridi wako, mpaka siku unakufa ili uishie katika ziwa la moto..mifano hiyo ipo duniani leo hii, utakuta mtu alianza vizuri na Bwana, wengine hata walitokewa kabisa na malaika, wengine walisikia sauti ikizungumza nao, wengine wakaonyeshwa maono, wengine Mungu akawa anawapa chochote waombacho katika hatua za awali kabisa za wokovu wao, wengine wakaepushwa na hatari nyingi kimiujiza, wakajua kabisa sasa hapa safari imeanza..Lakini kwa tabia zao za kuyarudia rudia yale yale machafu ya nyuma kwa kipindi kirefu hiyo ikawafanya wageuke kuwa mawe ya chumvi..Ambao ndio hao leo hii huwezi kuamini hata kama walishawahi kumjua Kristo…

Wokovu sio jambo la kujaribu, na ndio maana biblia inatuambia..

Wafilipi 2:12 “………..utimizeni wokovu wenu wenyewe kwa kuogopa na kutetemeka.

2 Kwa maana ndiye Mungu atendaye kazi ndani yenu, kutaka kwenu na kutenda kwenu, kwa kulitimiza kusudi lake jema.

Ikiwa ni wewe mmojawapo ndugu yangu unayesoma haya, na ndani yako bado kuna kanuru kadogo ambacho kanakaribia kuzima… basi usikubali izime kabisa…ni vizuri ukatubu kwa kumaanisha kabisa mbele za Mungu sasahivi, na kuacha kwa moyo wako wote mambo maovu yote unayoyafanya kwa vitendo, na kumfuata Kristo, neema hii bado ipo juu yako na ndio maana unasikia ndani yako kuhukumiwa unaposoma haya,….huyo ni Roho Mtakatifu anakuvuta kwake tena, anza kugeuka na kupiga hatua mbele, usipoitii hiyo sauti itafika kipindi hutaisikia tena ndani yako, utakuwa ukipita mahali na kukutana na maneno kama haya utaishia kudhihaki na kukejeli, lakini sasa kuna hofu ndani yako kiasi kwamba unaogopa hata kusema neno lolote la kejeli, hiyo hofu ni ya thamani na ya muhimu sana, na ndio inayokuvuta utubu,

Hivyo Tubu leo acha kwenda disko, acha ulevi, mrudie mke/mume wako, acha wizi, acha rushwa, acha kila aina ya dhambi unayoifanya maishani mwako na wala usigeuke nyuma kama mke wa lutu..…hizi ni siku za mwisho..Siku yoyote unyakuo unapita, na hii dunia inakwenda kuwa jivu, Maisha yatasimama…kilichosalia kwako sasa ni nini kama sio kuyasalimika maisha yako kwa Bwana Yesu ayaokoe, naye atakupokea kwasababu anakupenda na kukuhurumia…dini yako ya kiislamu haitakupeleka popote, dini ya kikristo haitakupeleka popote, dhehebu lako mashuhuri halitakupeleka popote bali YESU KRISTO pekee ndiye atakayekupeleka sehemu salama..

Hivyo Ikiwa upo tayari leo hii kuanza tena upya na Bwana..

Basi uamuzi unaoufanya ni wa busara sana ambao hautakaa uujutie maisha yako yote kama ilivyokuwa hata kwetu sisi. Unachopaswa kufanya, hapo ulipo, chukua muda mchache ujitenge peke yako.

Kisha piga magoti, kisha fuatisha sala hii kwa Imani, ukijua kuwa Mungu yupo hapo karibu na wewe pembeni yako kukusikia..Kisha ukiwa sasa katika utulivu Sema sala hii kwa sauti.

EE MUNGU BABA, NAJA MBELE ZAKO, NIKIWA NINAJITAMBUA KUWA MIMI NI MKOSAJI NA NIMEKUTENDA DHAMBI NYINGI, NA KWAMBA NIMESTAHILI HUKUMU. LAKINI WEWE MUNGU WANGU ULISEMA KATIKA NENO LAKO KUWA WEWE NI MUNGU WA REHEMA UNAYEWAREHEMU MAELFU ELFU YA WATU WANAOKUPENDA WEWE. NA LEO HII NINAKUJA MBELE ZAKO NAHITAJI MSAMAHA WAKO NA MSAADA WAKO MUNGU WANGU, NINATUBU DHAMBI ZANGU ZOTE KWA KUMAANISHA NA KWA MOYO WANGU WOTE, NINAKIRI KUWA YESU KRISTO NI BWANA, NA YEYE NDIYE MWOKOZI WA HUU ULIMWENGUNI. HIVYO NAOMBA DAMU YA MWANAO TAKATIFU INISAFISHE UOVU WANGU WOTE SASA NIFANYIKE KUWA KIUMBE KIPYA KUANZIA LEO NA HATA MILELE.

ASANTE BWANA YESU KWA KUNIPOKEA NA KUNISAMEHE.

AMEN.

Sasa ikiwa umefuatisha sala hiyo kwa Imani ..Hatua iliyobakia kwako ni kuithitisha toba yako kwa Vitendo ikiwa ulikuwa unafanya mambo yote ambayo hayampendezi Mungu unayaacha na kujitenga nayo, Sasa Mungu akishaona umegeuka kwa vitendo basi toba yako anaipokea na atakuja ndani yako wakati huo huo na kufanya makao ya milele kwako. Vile vile unahitaji, kutafuta kanisa la kiroho ambalo utajumuika na wakristo wengine katika kumwambudu Mungu, na kujifunza biblia ili uukulie wokovu. Na vilevile ili upate ubatizo sahihi wa kuzamishwa katika maji mengi na kwa jina la YESU KRISTO kwa ajili ya ondoleo la dhambi zako.

Zingatia hayo na Bwana atakuwa pamoja na wewe daima. Ubarikiwe sana.

Tafadhali washirikishe na wengine habari hizi njema, na pia kama utapenda tuwe tunakutumia masomo haya kwa njia ya email yako au Whatsapp tutumie ujumbe au piga namba hii +255 789001312. jiunge na channel yetu Kwa kubofya hapa >> WHATSAPP


Mada Nyinginezo:

KAMA MUNGU ANABORESHA KAZI ZAKE, KWANINI WEWE USIBORESHE ZA KWAKO?.

USIKIMBILIE TARSHISHI.

NIFANYE NINI ILI NILITIMIZE KUSUDI LA MUNGU.

YEZEBELI ALIKUWA NANI

CHAGUA NI JIWE LIPI LITAKALO KUFAA KWA UJENZI.

MWAKA WA BWANA ULIOKUBALIWA.

Ni nani anayetawala dunia kati ya Mungu na shetani?

Rudi Nyumbani:

DOWNLOAD PDF
WhatsApp

Source URL: https://wingulamashahidi.org/2020/02/24/jinsi-neema-ya-mungu-ilivyokuwa-kubwa-kwa-mke-wa-lutu/