KUOTA UNAANGUKA .

by Admin | 11 March 2020 08:46 pm03

Kuota unaanguka chini maana yake ni nini?


Ndoto hii huwa inachukua maumbile tofautitofauti, wengine wanaota wanaanguka kutoka kwenye ghorofa refu sana, wengine kutoka kwenye mti mrefu, wengine kwenye shimo lisilokuwa na mwisho, wengine wanaota wanaanguka kutoka angani. Wengine wanaangukia kwenye maji n.k.

Maadamu kiini cha ndoto ni Kuanguka kutoka sehemu fulani, basi ujue ndoto hiyo ni tahadhari kubwa  kwako kutoka kwa Mungu, kwani Biblia inasema..

Ayubu 33:14 “Kwa kuwa Mungu hunena mara moja, Naam, hata mara ya pili, ajapokuwa mtu hajali. 

15 Katika ndoto, katika maono ya usiku, Usingizi mzito uwajiliapo watu, Katika usingizi kitandani; 

16 Ndipo huyafunua masikio ya watu, Na kuyatia muhuri mafundisho yao, 

17 Ili amwondoe mtu katika makusudio yake, Na kumfichia mtu kiburi; 

18 YEYE HUIZUIA NAFSI YAKE ISIENDE SHIMONI, Na uhai wake usiangamie kwa upanga. 

19 Yeye hutiwa adabu kwa maumivu kitandani mwake, Na kwa mashindano yaendeleayo daima mifupani mwake”;

Unaona huo mstari wa 15 unasema  Mungu kumbe anaweza kuzungumza na mtu mara moja, katika ndoto na asipojali atazungumza naye hata mara mbili..ili tu amzuie nafsi yake isiende shimoni. Hivyo fahamu kuwa ndoto hiyo ni Mungu anazungumza na wewe kukuonya.

Ni vizuri kujua katika biblia inapozungumza kuanguka inamlenga  ibilisi mwenyewe kwasababu yeye peke yake ndio anayetajwa akianguka kutoka mbinguni..Bwana Yesu alisema..

 “…Nilimwona Shetani, akianguka kutoka mbinguni kama umeme(Luka 10:18)..

Sasa inaposema alimwona shetani akianguka inamaanisha kuwa hapo mwanzo alikuwa sehemu sahihi lakini kuna wakati ulifika alifanya mambo fulani yasiyofaa ndio yakamfanya atoke katika ile sehemu yake na aanguke chini kwa kasi sana kama umeme.. na hicho si kingine Zaidi ya dhambi ya uasi..

Hivyo tendo la kuanguka ni tendo linalofunua uasi.. Shetani alipoasi ndipo alipoanguka chini, Vivyo hivyo na mtu yeyote leo hii anapomuasi Mungu, ni ishara kuwa anaanguka kutoka katika uwepo wa Mungu na mwisho wake unaenda kuwa mbaya  kama ulivyokuwa kwa shetani.

Kwahiyo ikiwa unaota unaanguka chini, tena mahali ambapo hufiki, basi ujue hiyo ni tahadhari kwako, kuwa unaanguka kutoka katika neema ya Mungu, mrudie Mungu wako kabla mlango wa neema haujafungwa.. Yaangalie Maisha yako, na matendo yako, unaona kabisa hayaendani na njia ya wokovu..unaona kabisa hata Kristo akirudi leo hii utaachwa kutokana na njia zako na mienendo yako.

Kwa kuwa Mungu anakupenda na anaona mwisho wako utakavyokuwa kama wa shetani, ndio maana anakuonyesha ndoto kama hiyo, anachotaka kwako ni  utubu dhambi zako, umgeukie yeye. Ukitubu leo kwa kumaanisha atakuokoa, na kukusafisha kabisa..Anachohitaji kwako ni moyo wa kumaanisha, kabisa, Hivyo kama kweli umemaanisha kufanya hivyo leo basi ujue uamuzi unaoufanya ni mzuri..Usijiangalie wewe ni muislamu, au mkristo ikiwa Kristo hajaumbika ndani ya Maisha yako, haijalishi wewe ni nani, umepotea tu na hata ukifa leo huwezi kwenda mbinguni..

Hivyo kama unapenda Yesu leo awe mwokozi wako, na kiongozi wa Maisha yako basi

Basi uamuzi unaoufanya ni wa busara sana ambao hautakaa uujutie maisha yako yote kama ilivyokuwa hata kwetu sisi. Unachopaswa kufanya, hapo ulipo, chukua muda mchache ujitenge peke yako. Biblia inasema saa ya wokovu ni sasa, hivyo usingojee Kesho, haitakuwa yako..

Sasa ukishajitenga sehemu yako mwenye, piga magoti, kisha fuatisha sala hii kwa Imani, ukijua kuwa Mungu yupo hapo karibu na wewe pembeni yako kukusikia..Kisha ukiwa sasa katika utulivu Sema sala hii kwa sauti.

EE MUNGU BABA, NAJA MBELE ZAKO, NIKIWA NINAJITAMBUA KUWA MIMI NI MKOSAJI NA NIMEKUTENDA DHAMBI NYINGI, NA KWAMBA NIMESTAHILI HUKUMU. LAKINI WEWE MUNGU WANGU ULISEMA KATIKA NENO LAKO KUWA WEWE NI MUNGU WA REHEMA UNAYEWAREHEMU  MAELFU ELFU YA WATU WANAOKUPENDA WEWE. NA LEO HII NINAKUJA MBELE ZAKO NAHITAJI MSAMAHA WAKO NA MSAADA WAKO MUNGU WANGU, NINATUBU DHAMBI ZANGU ZOTE KWA KUMAANISHA NA KWA MOYO WANGU WOTE, NINAKIRI KUWA YESU KRISTO NI BWANA, NA YEYE NDIYE MWOKOZI WA HUU ULIMWENGUNI. HIVYO NAOMBA DAMU YA MWANAO TAKATIFU INISAFISHE UOVU WANGU WOTE SASA NIFANYIKE KUWA KIUMBE KIPYA KUANZIA LEO NA HATA MILELE.

ASANTE BWANA YESU KWA KUNIPOKEA NA KUNISAMEHE.

AMEN.

Sasa ikiwa umefuatisha sala hiyo kwa Imani ..Hatua iliyobakia kwako ni kuithitisha toba yako kwa Vitendo ikiwa ulikuwa unafanya mambo yote ambayo hayampendezi Mungu unayaacha na kujitenga nayo,

Sasa Mungu akishaona umegeuka kabisa kwa vitendo basi toba yako anaipokea na atakuja ndani yako wakati huo huo na kufanya makao ya milele kwako. Vile vile unahitaji, kutafuta kanisa la kiroho ambalo utajumuika na wakristo wengine katika kumwambudu Mungu, na kujifunza biblia ili uukulie wokovu. Na vilevile ili upate ubatizo sahihi wa kuzamishwa katika maji mengi na kwa jina la YESU KRISTO kwa ajili ya ondoleo la dhambi zako.

Ubarikiwe sana

Unaweza pia kujiunga na kundi letu la mafundisho Whatsapp, au kuwasiliana nasi kwa link hii

Group la whatsapp Kwa mgawanyo bora wa masomo download App hapa>> App wingu la mashahidi

Mada Nyinginezo:

NIFANYE NINI ILI NILITIMIZE KUSUDI LA MUNGU.

NINI TUNAJIFUNZA KWA MWANA MPOTEVU NA NDUGUYE?

CHAGUA NI JIWE LIPI LITAKALO KUFAA KWA UJENZI.

DHIKI KUU INAKUJA NA UNYAKUO UPO KARIBU.

MAPIGO YA VITASA SABA, NA SIKU YA BWANA.

Rudi Nyumbani:

DOWNLOAD PDF
WhatsApp

Source URL: https://wingulamashahidi.org/2020/03/11/kuota-unaanguka/