USIABUDU SANAMU.

by Admin | 23 May 2020 08:46 am05

Sanamu ni kitu chochote kile kinachotengenezwa chenye umbile aidha la malaika wa mbinguni, mwanadamu, mnyama, au mimea…Mwanadamu yoyote anayetengeneza kitu chochote chenye mifano ya hivyo vitu tayari kashatengeneza sanamu.

Sasa sio dhambi kutengeneza sanamu…ikiwa ina lengo lisilo la kiibada…kwamfano sanamu zilizopo makumbusho, hizo lengo lake ni la kumbukumbu, pia sanamu za Wanyama kama tembo, samaki,swala,watu n.k zilizopo sehemu za makumbusho au sehemu za maonyesho, au ambazo zinawekwa mahali kama nembo ya nchi au urembo wa mji sio dhambi…

Tatizo kubwa ni pale zinapotengenezwa kwa lengo la Ibada!…kwamba inapofikia hatua ya mtu kuamini kwamba sanamu ile ya tembo ina UUNGU ndani yake na hivyo inahitajika kuogopwa au kusujudiwa, kwamba Sanamu ya mtu yule ambaye alikuwa shujaa wa Taifa letu ina Uungu ndani yake, sanamu ile ya Mtakatifu aliyewahi kuishi Ina Uungu ndani yake, na hivyo inastahili kusujudiwa, na kupewa heshima fulani na hata kutukuzwa..Hilo ndio tatizo.

Sasa kuzitumikia na kuzisujudia sanamu kwa namna hiyo ndiko kunakoitwa IBADA ZA SANAMU. Na hizi ibada za sanamu zilianzia kwa wapagani, na shetani ameziingiza mpaka kwenye kanisa..na amewapofusha watu macho na kuwafanya wasione kabisa ukweli kuwa wanaabudu sanamu..

Kwamfano utaona sanamu ya mtakatifu fulani wa kwenye biblia labda tuseme Petro, au Paulo au Hana…imewekwa pale na inapewa heshima kana kwamba ni Paulo mwenyewe yupo ndani ya ile sanamu, inapewa heshima kana kama ni Petro mwenyewe yupo ndani ya ile sanamu kiasi kwamba mtu anaogopa hata kuikanyaga kwa bahati mbaya..kwasababu anahisi kabisa yule pale ni Petro, au Paulo amesimama…

Unakuta imewekwa sanamu ya Bwana Yesu pale, mtu anaogopa hata kuitazama usoni akihisi ni Bwana Yesu Mwenyewe yupo pale anamtazama,…hivyo inamfanya aende kwa adabu na staha na moyo wa ibada mbele ya ile sanamu, hatimaye kujinyenyekeza chini yake na hata kutaka kubarikiwa chini ya ile sanamu…HAYO NDIYO MACHUKIZO MBELE ZA MUNGU…Hiyo ndiyo sababu Bwana amesema Kwamba tusizichonge kabisa kama zitatupeleka katika kuzisujudia na kuzitumikia kwasababu zinamtia Mungu WIVU…Maana yake ni kwamba badala moyo wako uwe mbinguni Mungu aliko, na akili yako uipeleke mbinguni, na mawazo yako uyapeleke mbinguni mahali alipo…wewe unayapeleka kwenye ile sanamu iliyopo mbele yako, unayapeleka katika picha iliyopo mbele yako, hicho ndicho kinachomtia Mungu wivu.

Na inafika mbali Zaidi hadi wengine wanaziundia sala maalumu za kuombea, yaani wanafanya sanamu hizo kama nyezo au daraja la kuwasiliana na Mungu.

Kutoka 20:4 “Usijifanyie sanamu ya kuchonga, wala mfano wa kitu cho chote kilicho juu mbinguni, wala kilicho chini duniani, wala kilicho majini chini ya dunia.

5 Usivisujudie wala kuvitumikia; kwa kuwa mimi, Bwana, Mungu wako, ni Mungu mwenye wivu; nawapatiliza wana maovu ya baba zao, hata kizazi cha tatu na cha nne cha wanichukiao,

6 nami nawarehemu maelfu elfu wanipendao, na kuzishika amri zangu”.

Mungu wetu anataka tumwabudu katika roho na kweli…na si katika sanamu…

Yohana 4:20 “Baba zetu waliabudu katika mlima huu, nanyi husema ya kwamba huko Yerusalemu ni mahali patupasapo kuabudia

21 Yesu akamwambia, Mama, unisadiki, saa inakuja ambayo hamtamwabudu Baba katika mlima huu, wala kule Yerusalemu.

22 Ninyi mnaabudu msichokijua; sisi tunaabudu tukijuacho; kwa kuwa wokovu watoka kwa Wayahudi.

23 Lakini saa inakuja, nayo sasa ipo, ambayo waabuduo halisi watamwabudu Baba katika ROHO NA KWELI. Kwa maana Baba awatafuta watu kama hao wamwabudu.

24 Mungu ni Roho, nao wamwabuduo yeye imewapasa kumwabudu katika roho na kweli”

Umeona Mungu aabudiwi kupitia sanamu fulani, wala kilima fulani wala mtu fulani wala malaika fulani..yeye anaabudiwa katika roho na kweli…Laiti kama angekuwa anapenda tumwabudu kwa kumuuona…asingekuwa kama alivyo leo…angejidhihirisha duniani kote na wote tungeijua sura yake, na picha yake ingezagaa kila mahali, tungeiabudu na kuisujudia na wote tungekuwa na nakala ya picha hiyo…tungeiweka mpaka kama nembo ya Hela yetu..lakini hajayaruhusu hayo kwasababu anataka sisi tusimwabudu kupitia picha yake..anataka tumwabudu katika ROHO NA KWELI.

Hatumwoni lakini tunaamini yupo…Na hiyo Imani ya kwamba hatumwoni lakini tunaamini yupo, ndiyo ya thamani kwake…na ndiyo anayotaka tumwabudu nayo…

Kama ni picha ya Bwana Yesu au mtakatifu yoyote iwepo tu kama “lugha ya picha” na si chombo cha ibada wala kichukuacho sehemu ya hisia za mtu kana kwamba ndio kitu chenyewe halisi….Bwana anataka tukiweka sanamu/picha ya mtakatifu fulani tuichukulie ile picha kama vile tunavyoichukulia picha/sanamu ya mnyama iliyopo makumbusho…Hakuna mtu anayeweza kwenda mbele ya sanamu tembo na kuiogopa na kuipa heshima kana kwamba ni tembo halisi yupo pale, hakuna mtu anayeweza kuona sanamu ya simba akatetemeka na kukimbia, hakuna mtu anaweza kuona sanamu ya ng’ombe akaenda kukamua maziwa chini yake…Na sisi hatupaswi kwenda kukamua baraka kutoka kwenye sanamu ya mtakatifu Mariamu tulioitengeneza sisi au ya Bwana mwenyewe.

Shetani ameshalijua hilo, Hivyo alichokifanya ni kwenda kujipachika nyuma ya sanamu hizo, ili mumwabudu kisirisiri. Hivyo unapojihusisha na mojawapo ya ibada hizo ujue kabisa unamwabudu shetani.

2Wakorintho 6:16 “Tena pana mapatano gani kati ya hekalu la Mungu na sanamu? Kwa maana sisi tu hekalu la Mungu aliye hai; kama Mungu alivyosema, ya kwamba, Nitakaa ndani yao, na kati yao nitatembea, nami nitakuwa Mungu wao, nao watakuwa watu wangu.

17 Kwa hiyo, Tokeni kati yao, Mkatengwe nao, asema Bwana, Msiguse kitu kilicho kichafu, Nami nitawakaribisha.

18 Nitakuwa Baba kwenu, Nanyi mtakuwa kwangu wanangu wa kiume na wa kike,

Bwana atubariki na kutusaidia.

Tafadhali washirikishe na wengine habari hizi njema, na pia kama utapenda tuwe tunakutumia masomo haya kwa njia ya email yako au Whatsapp tutumie ujumbe kwenye box la maoni chini au piga namba hii +255 789001312

Mada Nyinginezo:

MAFUNDISHO YA MASHETANI

DANIELI: Mlango wa 3

Sabato halisi ni lini, Je! ni Jumapili au Jumamosi?, Ni siku gani itupasayo kuabudu?

Amin, nawaambia, Kizazi hiki hakitapita, hata hayo yote yatakapotimia..!!

CHUKIZO LA UHARIBIFU

UNYAKUO.

Rudi Nyumbani:

DOWNLOAD PDF
WhatsApp

Source URL: https://wingulamashahidi.org/2020/05/23/usiabudu-sanamu/