NA UPEPO WA KUSI ULIPOANZA KUVUMA KIDOGO,

by Admin | 10 June 2020 08:46 am06

Na upepo wa kusi ulipoanza kuvuma kidogo, wakidhani ya kuwa wamepata waliyoazimu.


Shalom jina la Bwana wetu Yesu Kristo libarikiwe.

Si kila dalili nzuri inayoonekana mbele yetu, itatuletea mwisho mwema, Kama hatutakaa chini kutaka kutafuta mashauri ya Mungu, tuwe na uhakika kuwa kuna uwezekano mkubwa sana wa kupotea..Kama vile biblia inavyotuambia katika…

Mithali 14:12 “Iko njia ionekanayo kuwa sawa machoni pa mtu, Lakini mwisho wake ni njia za mauti”.

Tukiiangalia mfano ile safari ya Mtume Paulo kutoka Yerusalemu kwenda Rumi kama mfungwa, haikuwa safari ya kawaida, kama sio neema ya Mungu tu kuwa pamoja na Paulo basi asingenusurukia mtu yeyote kwenye ile safari waliyosafiri yeye pamoja na wafungwa wengine, pamoja na maasakari wote na manahodha wote..Lakini hiyo yote ilisababishwa na wengi wao kuyadharau mashauri ya Mungu na kuyafuata mawazo yao wenyewe na akili zao wenyewe zinavyowatuma.

Kwani walipofika kwenye kisiwa kimoja kinachoitwa bandari nzuri, walitulia pale kwa muda wakingoja hali iwe shwari kidogo kisha waanze safari tena, Lakini ghafla kukaanza kuvuma upepo mzuri sana unaovutia ujulikanao kama upepo wa Kusi , Upepo huu ukivuma basi manahodha huwa wanafurahi kwasababu ni upepo rafiki kwa kusafiria baharini, na zaidi ya yote unawafanya safari yao kuwa nyepesi Zaidi na isiyogharimu.. Lakini Mtume Paulo kwa kuonywa na Roho aliwaambia wasisafiri, kwani mbeleni alionyeshwa watakumbana na madhara makubwa ambayo sio tu ya kupoteza shehena na merikebu bali yatahatarisha pia na maisha yao… Jambo hilo Yule Akida wa askari wala hakulizingatia, kwani aliyasikiliza zaidi mashauri ya mabaharia ambao wao kila siku wapo vilindini wenye uzoefu wa mambo hayo, pengine akajisemea moyoni huyu mfungwa maskini anatueleza nini..

Lakini biblia inatuambia walipoondoka tu kwenye kisiwa kile, hawakufikia hata mbali ule upepo wa kusi uligeuka na kuwa upepo wa Tufani wa aina nyingine ujulikanao kama Eurakilo.

Matendo 27:13 “Na upepo wa kusi ulipoanza kuvuma kidogo, wakidhani ya kuwa wamepata waliyoazimu kupata, wakang’oa nanga, wakasafiri karibu na Krete pwani kwa pwani.

14 Baada ya muda mchache ukavuma upepo wa nguvu wa namna ya tufani, uitwao Eurakilo,

15 merikebu iliposhikwa, na kutoweza kushindana na upepo, tukaiacha tukachukuliwa”.

Tufani ya namna hii ikikukumba ukiwa katikati ya bahari basi kupona hapo ni jambo ambalo haliwezekani, tufani za namna hii huwa zinakwenda kuathiri mpaka makazi ya watu nchi kavu, sasa jiulize kwa wale waliokuwa baharini ilikuwaje?..Na ndio maana ukisoma pale utaona jinsi safari ile ilivyowagharimu sana maisha,baada ya merikebu kuvunjwa, Kama sio mwenye haki mmoja kuwepo kwenye ile meli asingepona mtu kabisa..

Hayo ni mambo ambayo tunapaswa tujifunze katika maisha, tunaweza tukawa tunauzoefu mwingi wa kimaisha, tunaweza tukawa na ujuzi Fulani wa mambo, lakini tusipokaa chini na kuyatafuta mapenzi ya Mungu katika maisha yetu, badala yake tukawa tunagemea akili zetu tu, ziamue kila jambo..tufahamu kuwa Eurakilo ipo mbele yetu..siku moja itatuangamiza tu.. Haijalishi hapo mwanzo zilishatusaidia mara ngapi, ipo siku tutanasika tu.

Tunaweza tukasema mbona jambo hili au shughuli hii, inauelekeo wa kunifikisha ninapotaka kufika? Ndugu je kabla hujaliendea ulishawahi kumshirikisha kwanza Mungu? Kama ni mapenzi yake au la?

Madhara ya kutomshirikisha Mungu njia zetu ni Mengi sana.. Na mojawapo ni ghafla tu tutajikuta tumepotea, tukiangalia kumbe ni mambo Fulani yalituponza mpaka tukafikia pale.

Hivyo maandiko haya matatu yakiwapo akilini mwetu, basi kuna uwezekano mkubwa wa kuufikia mwisho mwema..

  1. Mithali 14:12 “Iko njia ionekanayo kuwa sawa machoni pa mtu, Lakini mwisho wake ni njia za mauti”.

Na hili..

  1. Zaburi 119:9 “Jinsi gani kijana aisafishe njia yake? Kwa kutii, akilifuata neno lako”.

Na la mwisho ni hili…

  1. Mithali 16:3 “Mkabidhi Bwana kazi zako, Na mawazo yako yatathibitika”.

Bwana atubariki na kutuongoza katika njia zetu katika Jina la Yesu Kristo.

Tafadhali washirikishe na wengine habari hizi njema, na pia kama utapenda tuwe tunakutumia masomo haya kwa njia ya email yako au Whatsapp tutumie ujumbe kwenye box la maoni chini au piga namba hii +255 789001312

Mada Nyinginezo:

IKO NJIA IONEKANAYO KUWA SAWA MACHONI PA MTU.

SIRI YA KUFANIKIWA KWA MTUME PAULO.

Amin, nawaambia, Kizazi hiki hakitapita, hata hayo yote yatakapotimia..!!

NJONI, NUNUENI MLE NA MNYWE.

ZIKIMBIE TAMAA ZA UJANANI! NA MTU YEYOTE ASIUDHARAU UJANA WAKO.

MAPIGO YA VITASA SABA, NA SIKU YA BWANA.

Rudi Nyumbani:

DOWNLOAD PDF
WhatsApp

Source URL: https://wingulamashahidi.org/2020/06/10/na-upepo-wa-kusi-ulipoanza-kuvuma-kidogo/