NA NENO LA BWANA LILIKUWA ADIMU SIKU ZILE.

by Admin | 9 July 2020 08:46 pm07

Kuna wakati Israeli ilikuwa inapitia majira tofauti tofauti, Si kila wakati Mungu alikuwa anazungumza nao, ana kwa ana au kwa kupitia manabii au waamuzi, hapana Kuna wakati Mungu alikuwa hasemi chochote kabisa kwa kipindi fulani, Lakini hiyo haikumaanisha kuwa Mungu amewaacha au hafuatilii mienendo yao kabisa, bali ni jinsi tu yeye, alivyopenda na anafanya hivyo wakati mwingine ili tu kupima uaminifu wa watu wake.

Kipindi kimojawapo kilikuwa ni kile cha Nabii Samweli, na kingine ni kipindi cha kati ya Nabii Malaki hadi wakati wa Yohana mbatizaji ambapo inakadiriwa ni Zaidi ya miaka 300. Sasa kwa mfano tukirudi katika kipindi cha Samweli, tunaona ulifika wakati biblia inasema Neno la Bwana lilikuwa ni adimu sana, na kulikuwa hakuna mafunuo Dhahiri, hii ikiwa na maana kuwa Mungu hakuwa anajifunua moja kwa moja kwa watu wake, aidha kwa kupitia manabii au makuhani, au kitu chochote tusome..

1Samweli 3:1 “Basi, mtoto Samweli akamtumikia Bwana mbele ya Eli. Na neno la Bwana lilikuwa adimu siku zile; hapakuwa na mafunuo dhahiri.”

Unaona, sasa matokeo yake ni kuwa watu wengi walipoona hivyo, kwanini Mungu hasemi chochote, hazungumzi chochote, hapigi popote, wakadhani kuwa hawatazamwi mienendo yao na matendo yao, hapo ndipo baadhi ya watumishi wake wakaanza kupoa na kukengeuka mpaka kufikia hatua ya kufanya mambo ya ajabu madhabahuni pake…Kama vile tu ilivyo leo..

Mfano ukisoma pale utaona kulikuwa na Watoto wawili wa Kuhani aliyeitwa Eli, ambaye wa kwanza aliitwa Hofni, na wa pili aliitwa Finehasi, hawa walifikia hatua ya kuidharau sadaka ya Bwana,kwa kuchukua kiwango ambacho hawajaamuriwa kwa nguvu na Zaidi ya yote walikuwa wanazini na wanawake ambao walikuwa wanatumika katika nyumba ya Bwana.. Hofu ya Mungu ilikuwa imeshaondoka ndani yao, kwasababu tu waliona Mungu hafanyi lolote, wala hachukui hatua yoyote kwao..

Lakini siku ya siku ilipofika ya Mungu kuanza kusema tena Dhahiri..Hapo ndipo walipojua Mungu tangu zamani alikuwa anawatazama, na kuwalipa mema wale waliostahili mema, na mabaya wale waliostahili mabaya..

Siku moja kijana Samweli alipokuwa amelala usiku Bwana alimtokea na kumwambia..

1Samweli 3:11 “Bwana akamwambia Samweli, Angalia, nitatenda tendo katika Israeli, ambalo kila atakayelisikia masikio yake yatamwasha.

12 Siku hiyo nitayatimiza maneno yale yote niliyoyasema juu ya Eli katika habari za nyumba yake, tangu mwanzo hata mwisho.

13 Kwa maana nimemwambia ya kwamba nitaihukumu nyumba yake milele, kwa ajili ya ule uovu alioujua; kwa kuwa wanawe walijiletea laana, wala yeye hakuwazuia.

14 Na kwa hiyo nimeapa juu ya nyumba ya Eli, ya kwamba uovu wa nyumba ya Eli hautasafika kwa dhabihu wala kwa sadaka hata milele”.

Ujumbe huo ulikuwa ni mzito sana hata kwa Samweli ambaye haumuhusu, itakuwaje kwa wale wahusika?, Ukifuatilia Habari ile utaona ndani kipindi kifupi sana, zaidi ya watu elfu 80 walikufa kwa kupigwa na Mungu.. ikiwemo wale wana wawili wa Eli.

Hata sasa, upo wakati utaonekana kama Bwana amekaa kimya (Nikimaanisha kwa mapigo, yanaonekana kama adimu), lakini hilo lisitufanye tudhani kuwa haoni yanayoendelea katika kanisa lake..Tujue kuwa lipo kusudi analitekeleza na mojawapo ndio hilo la kuwapima walio waaminifu ni wapi …

Lakini wakati utafika, ambao utakuja kwa ghafla, atazungumza hukumu zake, lakini atakapozungumza safari hii ujue kuwa sikio lako litawasha . Leo hii unapata ujasiri wa kuvaa nusu uchi kanisani, unadhani Mungu kuwa kimya, inainajisi madhabahu yake ni kwamba anapendezwa na wewe, unashiriki meza ya Bwana halafu ukitoka hapo unakwenda kuzini, unadhani Mungu hakuoni.

wewe ni mchungaji lakini kuzini na washirika wako mfano wa Hofni na Finehasi ni kitu cha kawaida kwako, kwa kuwa huoni kitu chochote kikitokea katika Maisha yako, sasa unadhani ndivyo itakavyokuwa hivyo siku zote.

Unafanya mambo ya ajabu madhabahuni pa Mungu, wala huogopi, unafanya comedy, na siasi, ili upendwe na watu ukijiona wewe ni mjanja, nataka nikuambie wakati utafika wa mwenye madhabahu kuzungumza..

Wengine wanasema tunaishi chini ya neema, Mungu hawezi kuwaadhibu watu aliowakomboa kwa damu ya mwanawe.. Ndugu, Kasome Habari za Hanania na Safira na mke wake, halafu useme lile ni agano la kale au jipya?..Watu wale walikufa kwa kutotimiza tu viapo vyao kwa Mungu vya kumtolea sadaka, jiulize wewe ambaye ni mzinzi, halafu unashiriki meza ya Bwana, utakuwaje?

Tufahamupo hukumu za Mungu, basi tuchukue tahadhari kabla mabaya hayajatukuta mimi na wewe. Nyakati hizi ni za nyakati za hatari.

Maran Atha!

Tafadhali washirikishe na wengine habari hizi njema, na pia kama utapenda tuwe tunakutumia masomo haya kwa njia ya email yako au Whatsapp tutumie ujumbe kwenye box la maoni chini au piga namba hii +255 789001312


Mada Nyinginezo:

KIFO CHA REINHARD BONKEY KINAACHA UJUMBE GANI KWETU?

USHAURI KWA MWANAMKE WA KIKRISTO.

Je! msalaba kaburini una umuhimu wowote?

https://wingulamashahidi.org/2020/07/03/kutomzuia-kutombana-mtoto-wako-ni-dhambi/

Rudi Nyumbani:

DOWNLOAD PDF
WhatsApp

Source URL: https://wingulamashahidi.org/2020/07/09/na-neno-la-bwana-lilikuwa-adimu-siku-zile/