Jiepushe na tamaa ya Mali/kupenda fedha.

by Admin | 28 August 2020 08:46 pm08

Kwa namna ya kawaida fedha haina ubaya wowote, ni nyezo ambayo Mungu aliiruhusu iwepo na itumiwe ili kuendesha kushughuli zote za kijamii.

Mhubiri 19:19 “…Na fedha huleta jawabu la mambo yote”.

Lakini kitendo cha kupenda fedha, hicho ndicho Mungu amekikatazata, na katika biblia kimekemewa sana, ikiwa wewe ni mtoto wa Mungu, na roho ya kupenda fedha ipo ndani yako, basi upo hatarini sana, kuzama katika maovu mengi..biblia inasema hivyo..

1Timotheo 6:10 “Maana shina moja la mabaya ya kila namna ni kupenda fedha; ambayo wengine hali wakiitamani hiyo wamefarakana na Imani, na kujichoma kwa maumivu mengi.”

Ndio maana biblia inawaasa sana watoto wa Mungu na kuwaambia..

Waebrania 13:5 “Msiwe na tabia ya kupenda fedha; mwe radhi na vitu mlivyo navyo; kwa kuwa yeye mwenyewe amesema, Sitakupungukia kabisa, wala sitakuacha kabisa”.

Mungu ametoa ahadi ya kuwahudumia watoto wake, kiasi kwamba hawatapungukiwa kabisa, hawatakosa kabisa ikiwa tu watakuwa watulivu katika shughuli zao.

Mtu mwenye tabia ya  kupenda fedha ni rahisi kuhonga, ili upate fursa Fulani,ni rahisi kufanya biashara haramu kisa tu ameona  zinamwingizia  fedha nyingi, mwingine atakuwa radhi hata kujiuza mwili wake kisa fedha, wengine wanakwenda kwa waganga, wengine wapo tayari kuikana imani,..n.k.n.k. hapo ndipo unajua ni kwanini biblia inasema kupenda fedha ni shina la mabaya yote ulimwenguni. Wengine wapo tayari hata kuua watu, ili walipwe au waibe.

Mithali 1:19 “Ndivyo zilivyo njia za kila mwenye tamaa ya mali; Huuondoa uhai wao walio nayo”.

Na dalili mojawapo ambayo biblia inasema itatutambulisha kuwa tunaishi katika siku za mwisho, ni kuibuka kwa wimbi kubwa la watu wanaopenda fedha.

2Timotheo 3:1 Lakini ufahamu neno hili, ya kuwa siku za mwisho kutakuwako nyakati za hatari.

2 Maana watu watakuwa wenye kujipenda wenyewe, wenye kupenda fedha, wenye kujisifu, wenye kiburi, wenye kutukana, wasiotii wazazi wao, wasio na shukrani, wasio safi,”

Mpaka sasa, imefikia hatua huduma za rohoni kutolewa kwa fedha,

1Timotheo 6: 5 “na majadiliano ya watu walioharibika akili zao, walioikosa kweli, huku wakidhani ya kuwa utauwa ni njia ya kupata faida”.

Hiyo yote ni matokeo ya wanadamu kupenda fedha..Bwana Yesu alisema..

Mathayo 6:24 “Hakuna mtu awezaye kutumikia mabwana wawili; kwa maana atamchukia huyu, na kumpenda huyu; ama atashikamana na huyu, na kumdharau huyu. Hamwezi kumtumikia Mungu na mali”.

Shetani alijua hapa ndipo wanadamu wengi wanapoweza kunaswa, hivyo, akatumia  njia hiyo hiyo kumjaribia pia Yesu, akamwambia nitakupa milki zote za ulimwenguni, nitakupa fedha zote na majumba yote ikiwa utanisujudia tu. Lakini Bwana Yesu alimkemea akamwambia utamsujudia Bwana Mungu wako tu.. Kwasababu alijua kupenda fedha ni kuupenda ulimwengu.

1Yohana 2:15 “Msiipende dunia, wala mambo yaliyomo katika dunia. Mtu akiipenda dunia, kumpenda Baba hakumo ndani yake”.

Kama hiyo haitoshi Wenye mali, bado biblia inawapa nafasi ndogo sana ya kuurithi ufalme wa mbinguni;

Mathayo 19:23 “Yesu akawaambia wanafunzi wake, Amin, nawaambieni, ya kwamba itakuwa shida tajiri kuingia katika ufalme wa mbinguni.

24 Nawaambia tena, Ni rahisi zaidi ngamia kupenya tundu ya sindano, kuliko tajiri kuingia katika ufalme wa Mungu”.

Vifungu vipo vingi sana kwenye biblia vinavyozungumzia hatari za kupenda fedha., hatuwezi kuviweka vyote hapa, lakini kwa hivyo vichache  kama na wewe ni mmojawapo, basi geuka haraka sana, uridhike na vile Mungu anavyokupa, kwasababu biblia inasema..

Mhubiri 5:10 “Apendaye fedha hatashiba fedha, Wala apendaye wingi hatashiba maongeo. Hayo pia ni ubatili”.

Na pia inasema.

Zaburi 37:16 “Kidogo alicho nacho mwenye haki ni bora Kuliko wingi wa mali wa wasio haki wengi”.

Chuma kidogo kidogo utafanikiwa..

Mithali 13:11 “Mali iliyopatikana kwa haraka itapunguka; Bali yeye achumaye kidogo kidogo atazidishiwa”.

Lakini kama wewe hujaokoka, ukweli ni kwamba hii roho ya kupenda fedha haiwezi kuondoka ndani yako, hata iweje,  itaondoka, ikiwa tu utamruhusu Bwana Yesu aingie ndani yako aibadilishe Nia yako..

Akishakubadilisha hapo ndipo  Roho ya kuridhika na ya utulivu itaingia ndani yako, na hapo hapo Mungu ataanza kukufundisha njia sahihi na yenye Baraka ya kukusanya..mpaka mwisho wa siku atakufikisha pale anapotaka uwepo. Na zaidi ya yote utaurithi uzima wa milele.

Hivyo kama upo tayari leo hii kutubu dhambi zako, unahitaji kuokoka, uamuzi huo utakuwa ni wa busara sana basi, fungua hapa kwa ajili ya kuongozwa sala ya Toba >>> KUONGOZWA SALA YA TOBA

Bwana akubariki.

Tafadhali washirikishe na wengine habari hizi njema, na pia kama utapenda tuwe tunakutumia masomo haya kwa njia ya email yako au Whatsapp tutumie ujumbe kwenye namba hii +255 789001312

Mada Nyinginezo:

MKUMBUKE MKE WA LUTU.

UNAWAFAHAMU MANABII WA UONGO?

USIPOWATAMBUA YANE NA YAMBRE, KATIKA KANISA LA KRISTO, UJUE UMEPOTEA.

YONA: Mlango 1

UNYAKUO.

UTAWALA WA MIAKA 1000.

EPUKA MUHURI WA SHETANI

Rudi Nyumbani:

DOWNLOAD PDF
WhatsApp

Source URL: https://wingulamashahidi.org/2020/08/28/jiepushe-na-tamaa-ya-mali-kupenda-fedha/