MKUMBUKE MKE WA LUTU.

MKUMBUKE MKE WA LUTU.

Mkumbuke Mke wa Lutu..

Luka 17:28 “Na kadhalika, kama ilivyokuwa katika siku za Lutu, walikuwa wakila na kunywa, walikuwa wakinunua na kuuza, wakipanda na kujenga;

29 lakini siku ile Lutu aliyotoka Sodoma kulinyesha moto na kibiriti kutoka mbinguni vikawaangamiza wote.

30 Hivyo ndivyo itakavyokuwa siku ile atakayofunuliwa Mwana wa Adamu.

31 Katika siku ile, aliye juu ya dari, na vyombo vyake vimo ndani ya nyumba, asishuke ili kuvitwaa; na kadhalika, aliye shambani asirejee nyuma.

32 MKUMBUKENI MKEWE LUTU.

33 Mtu ye yote atakaye kuiponya nafsi yake, ataiangamiza; na ye yote atakayeiangamiza ataiponya”.

Ni wazi kuwa kizazi tunachoishi kinafananishwa na kile cha Sodoma na Gomora, kadhalika kinafananishwa pia na kizazi cha Nuhu, Na ni kwanini ni hichi na sio kizazi kingine?. Ni kwasababu yale mambo yaliyokuwa yanafanyika kule wakati ule ndio yanayofanyika sasa na zaidi hata ya pale, Kumbuka Jambo kuu lililopelekea Miji ya Sodoma na Ghomora kuteketezwa ni tabia ya ulawiti na ushoga, tafsiri ya neno lenyewe Sodoma ni Ulawiti, Hivyo wakati ule hiyo roho ya kuingiliana kwa watu kinyume na maumbile ilikuwa imekithiri jambo ambalo lilianza tena kuonekana likijirudia kwa kasi sana mwanzoni mwa karne ya 20 na kuendelea mpaka sasa.

Roho hii imekithiri katika karne hizi 2 kuliko vizazi vingine vyote vya nyuma vilivyotangulia. Mpaka sasa hivi vitendo hivyo vimehalalishwa kisheria, kwamba vimepewa haki ya kuitwa ndoa kama ndoa nyingine halali, Kama Bwana Yesu alivyotabiri siku hizo watu watakuwa wakioa na kuolewa. Sasa Kuoa na kuolewa kwenyewe kunakozungumziwa hapo sio ndoa za mke na mume hapana, bali ni ndoa za mume na mume, na mke na mke. Mambo ambayo tunayaona sasahivi yakihalalishwa hata katika nyumba zinazojiita ni za ibada.

Sasa madhara ya haya mambo ni nini?

Madhara yake ni kupelekea jamii nzima kuathiriwa na adhabu hata watu wanaoonekana kutokuwa na hatia wanashiriki adhabu yao. Kwamfano tukitazama katika kipindi cha Nuhu, makosa ya wanadamu yaliwasababisha hata wanyama wasiokuwa na hatia kuangamizwa, ilisabababisha nchi na mimea isiyokuwa na hatia kuharibiwa, ilisababisha watoto wachanga wasiotenda hayo makosa kuteketezwa pia. Kadhalika na katika kipindi cha Lutu vivyo hivyo Na ndivyo itakavyotokea hata katika kizazi hiki cha siku za mwisho, wataathirika hata na watu wengine na viumbe vingine visivyokuwa na makosa (visivyostahili hayo madhara).

Lakini kabla Bwana hajaleta maangamizi huwa anatuma kwanza wajumbe wa kuwaonya watu wajitenge na kizazi hicho, Na ndio tunakuja kuona katika wakati wa Nuhu waliotii sauti ya Mungu ni watu wachache (yaani watu 8 tu! kati ya mamilioni), Kadhalika katika wakati wa Lutu waliotii ni watu 4 tu lakini Yule wanne (ambaye leo tutajifunza habari zake) alilikuja kuangamia, na kupelekea watu 3 tu kupona kati ya maelfu na mamilioni waliokuwa mijini.

Siku zote tunajua ni jambo la kawaida kwa mwanadamu kufuata au kuamini kitu kinachopendwa na watu wengi, hata kama ni cha kipuuzi kiasi gani, kikiwa kimekubaliwa na wengi basi ni rahisi kupata wafuasi wengi pasipo hata kupata ukinzani.kwamfano jamii nyingi za zamani watu walikuwa na hofu ya kumiliki televisheni katika manyumba yao wakiogopa kuwa zinaweza kuharibu maadili ya familia au jamii zao, lakini kwa jinsi zinavyozidi kuongezeka na kuaminiwa na wengi, zinakuja kuwa ni kitu cha kawaida kadri muda ulivyozidi kuendelea hata wale wachache waliokuwa wanazitilia mashaka wanaanza kuona kama ulikuwa ni ushamba kuogopa kumiliki televisheni, 

Kadhalika pia zamani mtoto mdogo kumiliki simu ya mkononi wengi iliwashangaza sana, kuona kama mtoto ataharibikiwa, lakini kutokana na simu kuwa nyingi na wazazi wanaowawaruhusu wanao kuzitumi kuongezeka, inapelekea hata wale wazazi waliokuwa wanazipinga zisimilikiwe na watoto wao, wajione kama walikuwa washamba na wanahofu ya bure tu!, hii inakuja kutokana na presha ya watu wengine, hivyo husababisha yale madhara yalikuwa yanadhaniwa mwanzo kumezwa na mabadiliko ya kijamii.

Mfano mwingine ni kuwasili kwa fasheni, zamani ilikuwa mwanamke akionekana amevaa suruali alijulikana kama ni kahaba Fulani hivi, lakini kwa siku zilivyozidi kwenda na wavaaji kuongezeka, suruali zikaanza kuonekana kuwa ni kitu cha kawada sana kwa wanawake, hata wale wachache waliokuwa wanazipiga vita wanaanza kujiona kuwa walikuwa ni washamba..Na ndivyo ilivyo hata kwa ushoga, zamani ilikuwa hata kutamkwa hilo neon tu, ilikuwa ni aibu lakini leo hi kutokana na kwamba mambo haya yanazidi kuongezeka hata Eneo linalojiita la Kanisa mada hizo zinazungumziwa na kupewa kipaumbele na kuhalalishwa, limekuwa ni jambo la kawaida hata wale waliokuwa wanapinga mwanzoni, wanaanza kujiona kama walikuwa watu wa itikadi kali…Kwahiyo roho hii ya kubadilika kutokana na mikumbo ya watu wengi imeendelea mpaka sasa katika kanisa la Mungu..

Sasa mambo haya ndivyo yalivyokuwa katika zama za Lutu, Na Mungu kwa kumuhurumia Lutu na familia yake akamwambia atoke, lakini kabla ya wao kutoka walipewa nafasi ya kwenda kuwahubiria ndugu zao pia , lakini biblia inasema walionekana kama wanacheza mbele zao (mwanzo 19:24), Hivyo ikawalazimu watoke wao tu.

Tukizidi kusoma habari ile tunaona, Mkewe Lutu alikuja kugeuka nyuma na kuwa nguzo ya chumvi.

Kwanini Mke wa Lutu ageuke nyuma na anamwakilisha nani Sasa?

Mke wa Lutu anamwakilisha MKRISTO ambaye alishaokolewa huko nyuma, kumbuku Mke wa Lutu mwanzoni aliitika kabisa wito wa kutoka Sodoma, kwa kuyatambua maovu yote yaliyokuwa yanatendeka kule, kwamba wale watu walikuwa wanastahili hukumu , kwa kujua hilo aliamua kabisa kuyaacha mambo ya Sodoma na kuondoka, Lakini baadaye katikati ya safari alianza kujiona anavutiwa na mambo ya nyuma kuliko ya mbele, akianglia mbele haoni majumba, mali, wala raha, akiangalia nyuma anaona fahari, mali, starehe, karamu, mashamba, n.k. Hivyo akaanza kushawishika kidogokidogo kuyafikiria na kuyatamani aliyoyoaacha nyuma Hivyo matokeo yake akageuka, akaangamia na kuwa jiwe la chumvi.

Mke wa Lutu alidanganyika kama vile kanisa linavyodanganyika leo, pengine aliambiwa maneno haya na wale watu aliowahubiria huko nyuma;…,

aah! Ni nyie tu wanne Mungu aliowaona ndio watakatifu kuliko watu wote hapa Sodoma!, Vipi kuhusu watoto,? Unataka kusema watoto wasio na hatia Mungu atawaangamiza pia?, Na vipi kuhusu viongozi wetu wa kidini tulio nao huku, wao nao wataangamizwa, nyie ni bora kuliko wao? Na majengo yetu, na masinagogi yetu Mungu ataanzia wapi kuyaangamiza?..

Kwa kosa gani kubwa hivyo mji wote uteketezwe?..Nyie ni lazima mtakuwa mmesikia roho zidanganyazo..ambazo haziwatakii mema, zinawataka muache mali zetu mkimbilie milimani na kufa huko!…Vipi kuhusu mifugo kwani nayo imemkosea nini Mungu, hata iangamizwe? Mungu ni wa haki bwana, hawezi kufanya hivyo vitu….wapo wengi waliojaribu kama nyie wakapotea, embu tulieni hapa, muwe kama sisi acheni hizo itikadi zenu kali rudini kwenu, msije mkawa vichaa.

Ndivyo mke wa Lutu alivyodanganyika wakati akiwa katikati ya safari yake kwa kuyatafakari hayo maneno, akagundua kweli inawezekana ni upuuzi anaoufanya, kwamba hakuna kitu kama hicho, Mungu hawezi kuleta madhara kama yale kwa idadi kubwa ya watu kama ile,ni kweli vipi kuhusu mali zetu, vipi kuhusu mifugo yetu, vipi kuhusu ndugu zetu na watoto, vipi kuhusu viongozi wa kidini n.k…Kwa ushawishi mwingi kama huo Mke wa Lutu akageuka nyuma moja kwa moja na kuangamia milele.Na ndio maana Bwana alisema “Mkumbukeni mkewe Lutu”

Mkumbuke Mke wa Lutu

Ulikuwa mkristo mzuri zamani ulipoamini, macho yako yalikuwa yapo mbinguni, hukujali ulimwengu unakuchukuliaje, ulijua kabisa unaishi katika siku za mwisho na siku yoyote ghadhabu ya Mungu itamwagwa juu ya nchi, ulikuwa tayari kuacha sigara, pombe, uasherati, anasa, disco, ulawiti, usagaji, pornography, mustarbation, mizaha, matusi, vimini, suruali, mapambo yote ya kikahaba n.k. na zaidi ya yote ulikuwa umeshajumuika na wenzako katika safari ya kuukimbia ulimwengu.. Lakini ulifika wakati ukaanza kuona kama safari yako ni ngumu na ni wachache tu mpo, ukaanza kukumbuka mafundisho ya ya mashetani uliyohubiriwa huko nyuma..yaliyokuwa wanakuambia: Yesu haji leo wala kesho, ukakumbuka pia mtu mmoja alishawahi kukwambia dunia haiwezi kuangamizwa Mungu hawezi kuangamiza watu wasiokuwa na hatia, hawezi kuangamiza watoto wadogo, hawezi kuteketeza viongozi wetu wa kidini, kwani ni nyie tu kikundi kichache kinachojiona kitakatifu ndio mtakao okoka,? Mungu haoni wengine? Mungu ni Mungu wa upendo, Na zaidi ya yote unaacha uzuri wako, unaacha kujipa raha kama kijana unaenda kuwa mshamba,..utakumbuka kuna mwingine alikwambia kuna watu waliopita njia kama yako na mwisho wake ukawa ni matatizo, utakumbuka kuna kiongozi wa kidini alikuambia uzichunguze hizo roho…watakambia hizo ni roho za shetani zinazowafanya mtoke katika hali ya kawaida na kuwa katika hali ya kutazamia mambo yasiyokuwepo ya uongo n.k..

Sasa hapo na wewe unashawishika na kuyatazama mambo ya nyuma, ndugu/dada usigeuka nyuma maana kabla ya kurudi nyuma utakuwa umeshakuwa JIWE LA CHUMVI. Biblia inasema.

2Petro 2: 20 “Kwa maana wale waliokwisha kuyakimbia machafu ya dunia kwa kumjua Bwana na Mwokozi Yesu Kristo, kama wakinaswa tena na kushindwa, hali yao ya mwisho imekuwa mbaya kuliko ile ya kwanza.

21 Maana ingekuwa heri kwao kama wasingaliijua njia ya haki, kuliko kuijua, kisha kuiacha ile amri takatifu waliyopewa.

22 Lakini imetukia kwao sawasawa na ile mithali ya kweli, Mbwa ameyarudia matapiko yake mwenyewe, na nguruwe aliyeoshwa amerudi kugaa-gaa matopeni”.

Ndugu yangu mkumbuke MKE WA LUTU. Kumbuka dunia ya leo hii imejaa maovu ya kila namna, hivyo usitazame wimbi la watu wengi wanafanya nini, usitazame kwasababu vijana wote wanafanya anasa na wewe ufanye, kwasababu wanawake wote wanavaa vimini na wewe uvae kwasababu watu wote wanazini na wewe uzini, Biblia ilishatabiri katika siku za mwisho watakatifu watakuwa wachache, na upendo wa wengi utapoa, kama zilivyokuwa katika siku za Nuhu na siku za Lutu, Hivyo ukiwa wewe ni mkristo na umeacha mambo ya ulimwengu huu, zidi kujitakasa, maana siku si nyingi Mungu atauteketeza huu ulimwengu kabisa na watakaopona ni watakatifu ambao watakuwa ni wachache sana, mimi na wewe tuwe miongoni mwao….

2Petro 3: 3 “Mkijua kwanza neno hili ya kwamba katika siku za mwisho watakuja na dhihaka zao watu wenye kudhihaki, wafuatao tamaa zao wenyewe,

4 na kusema, Iko wapi ahadi ile ya kuja kwake? Kwa maana, tangu hapo babu zetu walipolala, vitu vyote vinakaa hali iyo hiyo, tangu mwanzo wa kuumbwa.

5 Maana hufumba macho yao wasione neno hili ya kuwa zilikuwako mbingu tangu zamani, na nchi pia, imefanyizwa kutoka katika maji, na ndani ya maji, kwa neno la Mungu;

6 kwa hayo dunia ile ya wakati ule iligharikishwa na maji, ikaangamia.

7 Lakini mbingu za sasa na nchi zimewekwa akiba kwa moto, kwa neno lilo hilo, zikilindwa hata siku ya hukumu, na ya kuangamia kwao wanadamu wasiomcha Mungu.

8 Lakini, wapenzi, msilisahau neno hili, kwamba kwa Bwana siku moja ni kama miaka elfu, na miaka elfu ni kama siku moja.

9 Bwana hakawii kuitimiza ahadi yake, kama wengine wanavyokudhani kukawia, bali huvumilia kwenu, maana hapendi mtu ye yote apotee, bali wote wafikilie toba.

10 Lakini siku ya Bwana itakuja kama mwivi; katika siku hiyo mbingu zitatoweka kwa mshindo mkuu, na viumbe vya asili vitaunguzwa, na kufumuliwa, na nchi na kazi zilizomo ndani yake zitateketea.

11 Basi, kwa kuwa vitu hivi vyote vitafumuliwa hivyo, imewapasa ninyi kuwa watu wa tabia gani katika mwenendo mtakatifu na utauwa,

12 mkitazamia hata ije siku ile ya Mungu, na kuihimiza; ambayo katika hiyo mbingu zitafumuliwa zikiungua, na viumbe vya asili vitateketea na kuyeyuka?”

Ubarikiwe.

Tafadhali “share” ujumbe huu kwa wengine na Mungu atakubariki.

Pia unaweza ukapata mafundisho haya Kwa njia ya Whatsapp yako, jiunge na channel yetu Kwa kubofya hapa >> WHATSAPP

Group la whatsapp


Mada Nyinginezo:

MAANA YA KUISHI NA MKE KWA AKILI.

TABIA YA KIPEKEE USIYOIJUA KUHUSU NENO LA MUNGU.

OKOA BADALA YA KUANGAMIZA!

ULE MSALABA UNAOWEKWA KWENYE KABURI, NA ILE IBADA INAYOFANYWA VINA UMUHIMU WOWOTE KWA MKRISTO?


Rudi Nyumnani

Print this post

About the author

Admin administrator

Subscribe
Notify of
guest
3 Comments
Newest
Oldest Most Voted
Inline Feedbacks
View all comments
Yohana petro
Yohana petro
1 year ago

Amen! Masomo ni mazuri sana Hakika tunapata ufahamu wa kimungu wa Kulijua neno la Mungu na Kuliishi.

Danieli
Danieli
1 year ago

Watumishi Mungu awabariki sana kwa somo zuri nimejifunza kitu hapa ni marufuku kurudi nyuma mbele kwa mbeli hadi kieleweke hata watuseme watutukane watutenge watudharau Yesu ni Bwana na mwakozi wa milele