Nini maana ya “kila tendo lisilotoka katika imani ni dhambi?”

by Admin | 4 November 2020 08:46 am11

Jibu: Tusome mstari huo kuanzia juu kidogo.

Warumi 14:21  “Ni vyema kutokula nyama wala kunywa divai wala kutenda neno lo lote ambalo kwa hilo ndugu yako hukwazwa.

22  Ile imani uliyo nayo uwe nayo nafsini mwako mbele za Mungu. Heri mtu yule asiyejihukumu nafsi yake katika neno lile analolikubali.

23  Lakini aliye na shaka, kama akila, amehukumiwa kuwa ana hatia, kwa maana hakula kwa imani. NA KILA TENDO LISILOTOKA KATIKA IMANI NI DHAMBI”

Tukirudi juu Zaidi katika Mstari wa 14, Neno la Mungu linasema..

Warumi 14:14  “Najua, tena nimehakikishwa sana katika Bwana Yesu, ya kuwa hakuna kitu kilicho najisi kwa asili yake, lakini kwake yeye akionaye kitu kuwa najisi, kwake huyo kitu kile ni najisi”

Katika mistari hii, biblia ilikuwa inazungumzia juu ya vyakula..Na katika agano jipya, biblia imesema hakuna chakula chochote kilicho najisi.. Kwasababu kinachomwingia mtu mdomoni hakimtii unajisi, bali kile kimtokacho moyoni mwake ndicho kinachomtia mtu unajisi..Ni Bwana wetu Yesu ndiye aliyetupa ufunuo huo, ambao ni kweli kabisa..kasome Mathayo 15:16-20.

Kwahiyo katika agano jipya, nguruwe sio najisi, Kambale sio najisi, hata wanaokula nyoka hawapati unajisi wowote.

Lakini kwasababu ufunuo huo umekuwa mgumu kueleweka kwa wengi, kwamba vyakula vyote vimetakaswa.. Hivyo bado wanabaki kuamini kuwa vipo baadhi vilivyo najisi, kama nguruwe, Kambale, na vingine baadhi…. Sasa hawa ndio biblia inawataja kuwa “DHAIFU WA IMANI” (Warumi 14:1), haijalishi wao watajiona wana Imani kiasi gani, lakini biblia imewataja kuwa ni dhaifu wa Imani. Na miongoni mwao wapo Wakristo na wasio wa Kristo.

Sasa kwasababu biblia ni kitabu cha Hekima, imetufundisha jinsi ya kuenenda na hawa watu,

Kwanza: hatupaswi kuyahukumu mawazo yao (Maana yake kuwalazimisha waamini tunachoamini sisi, ikiwemo pia kushindana nao hatupaswi kushindana nao).

Pili: hatupaswi kuutumia ujuzi huo tulionao sisi kuwafanya wamkosee Mungu, au wamwache Kristo au kumchukia.

Maana yake ni kwamba labda umemhubiria Muislamu, akamwamini na kumpokea Kristo, lakini bado akawa anaamini kuwa nguruwe ni najisi. Na wewe kwasababu una UJUZI wa kujua kuwa hakuna kilicho najisi, hupaswi kwenda kula nguruwe mbele yake..au kumlazimisha ale nguruwe, ukifanya hivyo mwisho wa siku utamhuzunisha na kumfanya arudi nyuma au auchukie ukristo moja kwa moja..Na tukimkosesha mtu mmoja kwaajili ya chakula biblia inasema tunamtenda Kristo dhambi (Ndio hapo biblia inasema ni heri nisilie nyama kabisa kama itamkosesha ndugu yangu)..

1Wakoritho 8:11 “Na yule aliye dhaifu aangamizwa kwa ujuzi wako, naye ni ndugu ambaye Kristo alikufa kwa ajili yake.

12  Hivyo, mkiwatenda dhambi ndugu zenu na kuitia jeraha dhamiri iliyo dhaifu, mnamtenda dhambi Kristo.

13  Kwa hiyo, chakula kikimkwaza ndugu yangu, hakika sitakula nyama hata milele, nisije nikamkwaza ndugu yangu”

kwasababu hata asipokula hivyo vyakula tunavyokula sisi haviwafanyi wao wasiende mbinguni. Wasipokula nguruwe Maisha yao yote au Kambale, na wakawa wamempokea Kristo, watafika mbinguni tu.. Hivyo hatupaswi kutumia UJUZI wetu kuiharibu kazi ya Mungu ya wokovu.

Ndivyo biblia inavyosema katika..

Warumi 14: 1  “Yeye aliye DHAIFU WA IMANI, mkaribisheni, walakini msimhukumu mawazo yake.

2  Mtu mmoja anayo imani, anakula vyote; lakini yeye aliye dhaifu hula mboga.

3  Yeye alaye asimdharau huyo asiyekula, wala yeye asiyekula asimhukumu huyo alaye; kwa maana Mungu amemkubali.

4  Wewe u nani unayemhukumu mtumishi wa mwingine? Kwa bwana wake mwenyewe yeye husimama au huanguka. Naam, atasimamishwa, kwa kuwa Bwana aweza kumsimamisha”

Sasa kwa huyu mtu ambaye ni DHAIFU WA IMANI, ambaye moyoni mwake “anaamini kabisa kwamba kula nguruwe ni dhambi, au kula chakula Fulani ni dhambi”.. mtu huyu akaacha kufanya hicho kitu anachokiamini na kwenda kula nguruwe au chakula kingine chochote ambacho anajua sio sawa kulingana na anachokiamini moyoni mwake. Huyo mtu ni wazi kuwa baada ya kula, moyoni mwake ATASIKIA HALI YA KUHUKUMIWA. Sasa hiyo hali ya kuhukumiwa anayoisikia maana yake ni kwamba, amefanya kitu kinyume na anachokiamini, Hapo tayari kafanya tendo ambalo halijatokana na kile anachokiamini, na hivyo ANATENDA DHAMBI!!…Hiyo ndio maana ya “KILA TENDO LISILOTOKA KATIKA IMANI NI DHAMBI”,

Lakini kama macho yake yalifumbuka na kupata ufunuo kuwa “ni kweli hakuna kilicho najisi” na kwa ufunuo huo akaenda kula chakula ambacho hapo kwanza alikuwa anakiona ni najisi..Ni wazi kuwa mtu huyo baada ya kula hatasikia kuhukumiwa moyoni mwake, kwasababu amefanya kitu akiwa na uhakika kwamba hamtendi Mungu dhambi, na hivyo atakuwa kafanya jambo lile kwa Imani, na kwake hiyo haitahesabika kuwa ni dhambi.

Hivyo ndugu unayesoma ujumbe huu, ambaye ni mkristo, kama unaamini kuwa bado kuna vyakula najisi, na hivyo dhamiri yako inakushuhudia kwamba hupaswi kula, basi usivile lakini hakikisha unaushikilia utakatifu wote na kukaa katika maagizo ya Mungu.

Na kama wewe haupo katika Imani ya kikristo (maana yake ni Muislamu au mtu wa Imani nyingine), fahamu kuwa Yesu anakupenda na alikufa kwaajili yako..Njoo kwa Yesu na heshima yako hiyo hiyo uliyonayo, yeye atakuongezea nyingine juu ya hiyo itakayodumu milele, …njoo kwa Yesu na ustaarabu wako huo huo, hatakupokonya, badala yake atakuongezea na mwingine mwingi udumuo milele…njoo kwa Yesu na maadili yako hayo hayo, na kujisitiri kwako huko huko, atakuongezea na mwingine mwingi…Njoo kwa Yesu ukiwa huli nguruwe hivyo hivyo, wala hatakuambia uanze kuzila nguruwe..anachokihitaji ni roho yako na si tumbo lako, akuokoe akupe uzima wa milele bure!..Kwasababu yeye ndiye aliyetumwa kuukomboa ulimwengu, wala hakuna mwingine.

Hivyo kama umeamua leo kumpokea hatua inayofuata ni rahisi sana, hapo ulipo piga magoti, kisha fuatilisha sala hii  kwa kufungua hapa >>> SALA YA TOBA

Bwana akubariki sana.

Tafadhali washirikishe na wengine habari hizi njema, na pia kama utapenda tuwe tunakutumia mafundisho ya Neno la Mungu ya mara kwa mara kwa njia ya email yako au Whatsapp basi tutumie ujumbe kwenye namba hii +255 789001312


Mada Nyinginezo:

SIKUKUU 7 ZA KIYAHUDI ZINAFUNUA NINI KWETU?

KUOTA UNAKULA CHAKULA.

CHAKULA CHA ROHONI.

Katika Mathayo 15:21-28, Yesu alikuwa na maana gani alipomwambia huyu Mama kwamba chakula cha watoto hawapewi mbwa?

Mstari huu una maana gani? “Tupa chakula chako usoni pa maji; Maana utakiona baada ya siku nyingi”. (Mhubiri 11:1)

Rudi Nyumbani:

DOWNLOAD PDF
WhatsApp

Source URL: https://wingulamashahidi.org/2020/11/04/nini-maana-ya-kila-tendo-lisilotoka-katika-imani-ni-dhambi/