MZAZI, JALI MAISHA YA KIROHO YA MTOTO WAKO.

by Admin | 15 November 2020 08:46 pm11

Kuna pepo moja lililowasumbua sana mitume wa Yesu, hilo halikuwa sawa na pepo mengine waliyokutana nayo, walihangaika nalo mchana kutwa lakini hawakufua dafu mpaka alipokuja Bwana Yesu mwenyewe kulikemea na kulitoa.

Lakini leo hatutazungumzia juu ya pepo hilo kwasababu habari yenyewe tunaijua, ila katika habari hiyo lipo jambo ambalo ni vizuri sisi tukajifunza, husasani kwa wazazi au walezi, wanaoishi na watoto wadogo. embu tusome tena alichokifanya Yesu kisha, tuende kwenye ujumbe wenyewe..

Marko 9:20 “Wakamleta kwake; hata alipomwona, mara yule pepo alimtia kifafa; naye akaanguka chini, akagaa-gaa, akitokwa na povu.

21 Akamwuliza babaye, AMEPATWA NA HAYA TANGU LINI? Akasema, TANGU UTOTO.

22 Na mara nyingi amemtupa katika moto, na katika maji, amwangamize; lakini ukiweza neno lo lote, utuhurumie, na kutusaidia”.

Sasa katika habari hiyo, usidhani Yesu alikuwa hajui matatizo ya huyo mtoto ndio maana akamwuliza vile, Kumbuka Yesu alikuwa anajua kila kitu wala alikuwa hana haja ya mtu kumuadhithia chochote, biblia inatuambia hivyo katika  Yohana 16:30, Lakini  aliuliza vile kwa lengo la kutaka watu wote wajue matatizo ya Yule mtoto yalianzia wapi, na ndio maana akamuuliza vile yule mzazi “Amepatwa na haya tangu lini?”.

Ndipo yule mzee akamjibu na kusema,  “amepatwa na haya tangu utotoni”. Ulishawahi  kuutafakari vizuri huu mstari, tangu utotoni? ..Hiyo ni kutuonyesha kuwa kuna mapepo ambayo, agenda yao kuu, ni watoto. Kwasababu yanajua yakianzia katika msingi, baadaye yatakuwa ni magumu kutoka.

Inashangaza leo hii kuona wazazi hawajali maisha ya kiroho ya watoto wao, wanaona kama wao ni watoto tu, shetani hawezi kuwashambulia, hawajui kuwa wanapaswa kulindwa kwasababu shetani huwa hatambui cha mtoto au cha mzee, lengo lake ni kuharibu. Kama alimuingia Nyoka ambaye ni mnyama tu, ataachaje kumwingine mtoto ambaye ni mwanadamu? ndio target yake kubwa?

Mzazi, anamruhusu mtoto wako mdogo atezame tv masaa 24 wakati wote hata zile programu ambazo haziendani na umri wake anamwacha azitazame, anamwacha asikilize miziki ya kidunia, tena Zaidi ya yote unafurahi anapocheza,  lakini nyimbo za tenzi hata moja haujui, Mzazi mwingine hata hampeleki mtoto wake Sunday school ili afundishwe njia ya kikristo angali akiwa mdogo, yeye anachojua ni kumnunulia mtoto wake nguo nzuri tu, kumtafutia nursery nzuri ya kusoma, anajali vya mwilini vya mwanawe anapuuzia na vile vya rohoni. Hata kumwombea mtoto wake anashindwa.

Nachotaka nikuambie ni kuwa tusipowawekea msingi mzuri watoto wetu, shetani atatusaidia kuwawekea wake, kama alivyofanya kwa mtoto wa huyu mzee tunayesoma habari zake.  Lile pepo lina haki ya kuwa gumu kutoka kwasababu tayari lilikuwa na msingi tangu utotoni. Na ukiangalia lengo la hilo pepo si lingine zaidi ya kumwangamiza tu, mara litake kumtupa kwenye maji, kwa bahati nzuri pengine watu wanamuona wanamuokoa, mara litake kumtupa kwenye moto, lakini Mungu anafungua rehema zake anaepukika.

Leo hii utaona kumenyanyuka kundi kubwa la watoto ambao wanaonyesha tabia ambazo hazieleweki chanzo chake ni nini, na wewe unaweza ukadhani ni yeye anafanya kumbe ni pepo ambalo tayari lilishamvaa tangu utotoni ndio linaonyesha tabia hizo ndani yake.

Wazazi ndio wanapaswa waanze kubadilika, ndio watoto wabadilike.  Wewe kama mzazi, kama hutaonyesha kujali maisha ya kiroho ya mtoto wako, usidhani mtoto atabadilika mwenyewe au atakuwa na tabia njema huko mbeleni.

Mithali 22:6 “Mlee mtoto katika njia impasayo, Naye hataiacha, hata atakapokuwa mzee”

SASA UTAYAZUIAJE MAPEPO YA UHARIBIFU KAMA HAYO YASIMWINGIE MWANAO?

Kwanza ni kwa kutumia kiboko: Biblia inasema hivyo, …Pale unapoona kuna tabia Fulani ambayo sio nzuri, mfano kiburi, anatukana, hana nidhamu, hapo hapo hupaswi kuiacha hiyo tabia imee, mpaka hilo pepo liumbike ndani yake.. Utalitoa hilo kwa kiboko.

Mithali 23:13 “Usimnyime mtoto wako mapigo; Maana ukimpiga kwa fimbo hatakufa.

14 Utampiga kwa fimbo, Na kumwokoa nafsi yake na Kuzimu”.

Pili Ni  kwa kumfundisha kanuni za imani: Unamfundisha biblia, unamfundisha nyimbo za kikristo, unamfundisha kusali, unamfundisha hata kukariri  vifungu vya biblia, hata kama hataelewa sasahivi lakini vitabaki moyoni mwake kama hazina itakayokuja kumsaidia baadaye. Na  hakikisha pia unampelekea kwenye mafundisho ya watoto kanisani.

Tatu  Unamwombea; Mara kwa mara unahakikisha unamfunika mwanao, kwa damu ya Yesu Kristo, unatenga muda mrefu wa kumuombea.

Na Nne unamzuia kufanya/kutazama mambo ambayo hayapasi: Si lazima kila unachokitazama wewe, mtoto naye akitazame, magemu anayoyacheza mtoto si yote yanamaudhui mazuri, vilevile nguo unazomvisha mtoto si zote ni njema. Hivyo jifunze kumchagulia mtoto vinavyomfaa.

Ukizingatia hayo, basi mapepo kama hayo ambayo ni hatari na sugu, hayatamkuta mwanao. Kumbuka biblia inasema shetani ni kama simba angurumaye, akitafuta mtu ammeze, hivyo usipuuzie haya maagizo, mjenge mwanao, mjenge mdogo wako, mjenge mtoto yoyote auishiye naye.

Na Bwana atakubariki.

Tafadhali washirikishe na wengine habari hizi njema, na pia kama utapenda tuwe tunakutumia mafundisho ya Neno la Mungu ya mara kwa mara kwa njia ya email yako au Whatsapp basi tutumie ujumbe kwenye namba hii +255 789001312


Mada Nyinginezo:

TUMEFANYIKA KUWA WANA WA MUNGU!

AGENDA KUBWA YA SHETANI KWA KANISA HILI LA LAODIKIA.

KILEMBA CHA NEEMA, JE! UMEMVIKA MWANAO?

RUDI KUMPA MUNGU UTUKUFU.

Rudi Nyumbani:

DOWNLOAD PDF
WhatsApp

Source URL: https://wingulamashahidi.org/2020/11/15/mzazi-jali-maisha-ya-kiroho-ya-mtoto-wako/