Je shetani ana uwezo wa kujua mawazo ya mtu?

by Admin | 21 December 2021 08:46 pm12

Jibu: Hii ni moja ya hoja ambayo ni muhimu sana mkristo yeyote kuijua.

Ukweli ni kwamba shetani hawezi kuingia kwenye ufahamu wa mtu na kujua anachokifikiri au kukiwaza au kukipanga.

Huo uwezo hana, na hajawahi kuwa nao. Na sio yeye peke yake bali hata malaika hawana huo uwezo, wala wanadamu hawana huo uwezo.

Ni Mungu peke yake na mtu mwenyewe ndio wenye Nywila (password) ya kuingia ndani ya mawazo yako.

Maana yake ni kwamba kile unachokiwaza sasahivi ni wewe peke yako ndiye unayekijua na Mungu, shetani hakijui, wala malaika wala mwanadamu mwenzako.

Labda wewe ndio uamue kuwafunulia yaliyopo ndani yako.

Sasa swali hili; kama ni hivyo inakuwaje shetani anaonekana kama anajua mambo yetu hata yale ya siri?.

Jibu ni kwamba, anajua mambo yetu kwa kuzisoma fahamu zetu.

Hata wewe unaweza kumsoma mtu na kujua anachowaza kwa wakati huo, kama una utashi wa kutosha, lakini hiyo haijamaanisha kwamba umeingia katika ubongo wake na kuyaona mawazo yake kama Tv. Hapana!

Vivyo hivyo na shetani, ana uwezo mkubwa wa kumsoma mwanadamu na hata kujua anachowaza.. kwasababu amekabiliana na mwanadamu kwa miaka mingi, tangu Edeni anazijua tabia za wanadamu, hivyo ni rahisi pia kuyasoma mawazo yao lakini si kuingia ndani ya mawazo yao.

Kama vile wewe mtu mzima unavyoweza kuyasoma mawazo ya mtoto mdogo na kujua kila kitu anachokifikiri kwa wakati huo na shetani ni hivyo hivyo.

Lakini pamoja na kwamba shetani ana uwezo wa kuyasoma mawazo ya mtu, lakini bado anapata shida sana kuyasoma na kuwaelewa mawazo ya watu waliozaliwa mara ya pili kwa Roho.

Maandiko yanasema kuwa hali ya mtu aliyezaliwa mara ya pili ni kama upepo, haujulikani unapoanzia wala unapoishia.

Yohana 3:8 “Upepo huvuma upendako, na sauti yake waisikia, lakini hujui unakotoka wala unakokwenda; kadhalika na hali yake kila mtu aliyezaliwa kwa Roho”.

shetani anapata wakati mgumu sana kuyasoma mawazo ya mtu aliyezaliwa mara ya pili.

Kwasababu atadhani yale majaribu aliyomjaribu nayo jana, yatamfanya leo asiendelee na wokovu, kinyume chake anashangaa ndio kwanza anasonga mbele.

Au anategemea vile vitisho alivyomtisha navyo jana usiku, vitamfanya leo sidhubutuu kuendelea kuhubiri, au kuendelea na shughuli zake za kawaida, kinyume chake anaona yule mtu anaendelea kuhubiri kwa raha au anaendelea na shughuli zake.

Anategemea ule uchumi alioutikisa jana, utamfanya huyu mtu leo awe katika dimbwi kubwa la mawazo na hata kukufuru kinyume chake anamwona hata hawazi.

Kila anachojaribu kukifanya ili kumtikisa mtu aliyezaliwa mara ya pili, anakutana na matokeo tofauti na anayoyategemea.

Mtu aliyezaliwa mara ya pili anakuwa hatabiriki katika upeo wa shetani na mapepo yake. Tofauti na mtu ambaye hajazaliwa mara ya pili ambapo akitishiwa na wachawi kidogo tu ndani ya nyumba yake, tayari kashatishika kiasi kwamba shetani na mapepo yake wanajua kesho huyo mtu hatalala tena kwenye hiyo nyumba..Na kweli kesho yake halali tena huko ndani.

Mtu na namna hiyo shetani anakuwa anaweza kumsoma kirahisi na vile vile anakuwa anampangia maisha.

Swali ni je! Mimi na wewe tumezaliwa mara ya pili kwa Roho?. Kama bado basi tufahamu kuwa maneno haya yafuatayo yanatuhusu.

Yohana 3:3 “Yesu akajibu, akamwambia, Amin, amin, nakuambia, Mtu asipozaliwa mara ya pili, hawezi kuuona ufalme wa Mungu”.

Maran atha!

Tafadhali washirikishe na wengine habari hizi njema,

Kwa maombezi/Ratiba za ibada/ Ushauri/ Maswali.
Piga namba hizi: +255693036618 au +255789001312

pia kama utapenda uyapate mafundisho haya kwa njia ya Whatsapp au email basi tutumie ujumbe kwenye namba hizo hizo.


Mada Nyinginezo:

UKIOKOKA,HIZI FIKRA ZIKIJA NDANI YAKO, ZIKATAE.

YESU ANA KIU NA WEWE.

JISHUSHE ILI MUNGU AKUHUDUMIE.

Tofauti kati ya ndoto na Maono ni ipi?

JINSI MUNGU ATAKAVYOTOA THAWABU ZAKE, NA VIGEZO ATAKAVYOTUMIA. (Sehemu ya 4)

Rudi nyumbani

DOWNLOAD PDF
WhatsApp

Source URL: https://wingulamashahidi.org/2021/12/21/shetani-anajua-mawazo/