EZEKIELI, ITABIRIE MIFUPA MIKAVU.

by Admin | 22 December 2021 08:46 am12

Je! Ule Unabii wa mifupa mikavu una maana gani kwetu?


Ezekieli alionyeshwa maono,ambayo yalimshangaza sana, maono yenyewe yalihusu mifupa ya watu ambao walionekana kama walishakufa  kipindi kirefu sana nyuma, na inavyoelekea yalikuwa ni mauaji ya halaiki, (watu wengi waliouawa kwa wakati mmoja).Kwasababu mifupa hiyo ilikuwa mingi sana katika bonde kavu.

Hivyo alipopitishwa kwenye bonde hilo, alisikia sauti ya Mungu ikimuuliza Ezekieli Je! Mifupa hii inaweza kuwa hai tena?, Ezekieli akajibu wewe Bwana wajua, yaani wewe ndiye unayejua kama yaweza kuwa hai tena au la.

Lakini kama tunavyosoma Habari muda huo huo aliambiwa aitabirie uhai, na alipofanya vile  alishuhudia uumbaji wa Mungu kwa mara nyingine tena. Jinsi mifupa ilivyopata mishipa,  mara nyama, mara uhai na kutembea na kuongea tena..

Tusome.

EZEKIELI: MLANGO 37

1 Mkono wa Bwana ulikuwa juu yangu, naye akanichukua nje katika roho ya Bwana, akaniweka chini, katikati ya bonde; nalo limejaa mifupa;

2 akanipitisha karibu nayo pande zote; na tazama, palikuwa na mifupa mingi katika ule uwanda! Nayo, tazama, ilikuwa mikavu sana.

3 Akaniambia, Mwanadamu, je! Mifupa hii yaweza kuishi? Nami nikajibu, Ee Bwana MUNGU, wajua wewe.

4 Akaniambia tena, Toa unabii juu ya mifupa hii, uiambie, Enyi mifupa mikavu, lisikieni neno la Bwana.

5 Bwana MUNGU aiambia mifupa hii maneno haya; Tazama, nitatia pumzi ndani yenu, nanyi mtaishi.

6 Nami nitatia mishipa juu yenu, nami nitaleta nyama iwe juu yenu, na kuwafunika ngozi, na kutia pumzi ndani yenu, nanyi mtaishi; nanyi mtajua ya kuwa mimi ndimi Bwana.

7 Basi nikatoa unabii kama nilivyoamriwa; hata nilipokuwa nikitoa unabii, palikuwa na mshindo mkuu; na tazama, tetemeko la nchi, na ile mifupa ikasogeleana, mfupa kwa mfupa mwenziwe.

8 Nikatazama, kumbe! Kulikuwa na mishipa juu yake, nyama ikatokea juu yake, ngozi ikaifunika juu yake; lakini haikuwamo pumzi ndani yake.

9 Ndipo akaniambia, Tabiri, utabirie upepo, mwanadamu, ukauambie upepo, Bwana MUNGU asema hivi; Njoo, kutoka pande za pepo nne, Ee pumzi, ukawapuzie hawa waliouawa, wapate kuishi.

10 Basi nikatabiri kama alivyoniamuru; pumzi ikawaingia, wakaishi, wakasimama kwa miguu yao, jeshi kubwa mno.

11 Kisha akaniambia, Mwanadamu, mifupa hii ni nyumba yote ya Israeli; tazama, wao husema, Mifupa yetu imekauka, matumaini yetu yametupotea; tumekatiliwa mbali kabisa.

12 Basi tabiri, uwaambie, Bwana MUNGU asema hivi; Tazama, nitafunua makaburi yenu, na kuwapandisha kutoka katika makaburi yenu, enyi watu wangu, nami nitawaingizeni katika nchi ya Israeli.

13 Nanyi mtajua ya kuwa mimi ndimi Bwana, nitakapoyafunua makaburi yenu, na kuwatoa ninyi katika makaburi yenu, enyi watu wangu.

14 Nami nitatia roho yangu ndani yenu, nanyi mtaishi, nami nitawawekeni katika nchi yenu, nanyi mtajua ya kuwa mimi, Bwana, nimesema hayo, na kuyatimiza, asema Bwana.

Hii ni mistari ya Faraja, kwasababu inaeleza ukuu wa Mungu, kwenye matumaini ambayo yalishakwisha potea. wana wa Israeli walipopelekewa unabii huu walipata nguvu mpya,kwasababu wakiwa Babeli walikuwa wameshapoteza matumaini ya kurudi katika taifa lao tena, kuishi na kumwabudu Mungu. Lakini Mungu akawaambia japokuwa mmekuwa kama mifupa mikavu iliyokauka, mimi nitawafufua tena na kuwarudisha katika nchi yenu, na kupanda na kujenga na kunitumikia tena.

Na kweli jambo hilo lilikuja kutokea vilevile, Bwana aliwarejesha tena katika taifa lao.

Hata sasa, unaweza ukawa umekufa, kwa namna nyingi, mpaka umekata tamaa ya kuishi au ya kuendelea mbele katika Imani, pengine afya yako imepoteza matumaini kabisa, labda unaugonjwa wa kiharusi huwezi kutembea umelala tu kitandani miaka mingi au una kansa hatua ya nne, umeambiwa na daktari una wiki chache tu za kuishi, au umeishi na virusi vya ukimwi kwa muda mrefu sasa, na kinga yako imeshuka sana, siku yoyote umeambiwa unaondoka, usiogope, Bwana anaweza kukurejesha ukawa mzima tena, kama zamani.

Ibrahimu alikuwa na matumaini hayo, na ndio maana hakuona shida kumtoa mwanaye kafara kwa ajili ya Bwana, mpaka Mungu akamuita baba wa Imani,

Waebrania 11:17 “Kwa imani Ibrahimu alipojaribiwa, akamtoa Isaka awe dhabihu; na yeye aliyezipokea hizo ahadi alikuwa akimtoa mwanawe, mzaliwa pekee;

18 naam, yeye aliyeambiwa, Katika Isaka uzao wako utaitwa,

19 akihesabu ya kuwa Mungu aweza kumfufua hata kutoka kuzimu; akampata tena toka huko kwa mfano”.

hivyo na wewe kuwa na Imani na Mungu wako, hakuna linalomshinda yeye.

Mwingine, unaweza ukawa hata chakula ni shida, hujui kesho utaamkaje, familia inakutegemea, kazi huna, umekuwa mifupa mikavu kwelikweli, kumbuka uwezo wa Mungu ni mkubwa sana. Anaweza kukufufua kutoka huko tena, na kukutajirisha.

Unachopaswa kufanya ni kutulia katika mapenzi yake. Yaani, kama hujaokoka basi OKOKA leo, na kama umeshaokoka, basi zidi kumwamini yeye, na hakika atakutengenezea njia pasipo na njia.

Ikiwa wewe ni mmojawapo wa mifupa hii mikavu, ningependa tusali Pamoja sala hii;

Basi magoti mahali ulipo  kisha nyanyua mkono wako mmoja juu kisha sema sala hii kwa Imani na Bwana atakusaidi.

Baba yangu, Nimejua hakika wewe ni Mungu, wala hapana mwingine mwenye ishara kuu na za ajabu kama wewe. Nimesoma maneno yako, nami nimeamini, kuwa wewe MUNGU unaweza kurejesha uhai tena kwa watu waliokwisha kufa na kuoza na kubakia mifupa tu. Naomba Bwana wangu, unisamehe makosa yangu yote, niliyokukosea kwa kujua na kutokujua. Naomba Damu ya mwanao Yesu Kristo initakase kuanzia sasa, nami nakiri kuwa nitatembea katika maisha ya utakatifu, sikuzote za Maisha yangu.

Naomba unisaidie tatizo langu hili (Taja tatizo lako, kama ni ugonjwa, shida, n.k. mwambie ), Unifufue upya, nisimame, nikutukuze, nikutumikie, nikuabudu Mungu wangu. Asante kwa kunisamehe, Asante kwa kunisaidia, asante kwa kuniweka huru.

Amen.

Irudie sala hiyo kwa mara nyingine tena, hadi usikie amani ndani ya moyo yako.

Na amini kuwa Bwana ameshaanza kutenda jambo katika Maisha yako,.

Ubarikiwe sana.

Tafadhali washirikishe na wengine habari hizi njema,

Kwa maombezi/Ratiba za ibada/ Ushauri/ Maswali./Ubatizo
Piga namba hizi: +255693036618 au +255789001312

pia kama utapenda uyapate mafundisho haya kwa njia ya Whatsapp au email basi tutumie ujumbe kwenye namba hizo hizo.

Mada Nyinginezo:

Kama wakitenda mambo haya katika mti mbichi, itakuwaje katika mkavu?

FAHAMU JINSI MUNGU NA SHETANI WANAVYOZUNGUMZA NA WATU.

HEKIMA YA KIMUNGU, INAINGIAJE MIOYONI MWETU?

FAHAMU JINSI MUNGU NA SHETANI WANAVYOZUNGUMZA NA WATU.

Rudi nyumbani

DOWNLOAD PDF
WhatsApp

Source URL: https://wingulamashahidi.org/2021/12/22/ezekieli-itabirie-mifupa-mikavu/