HUJAPEWA MBAWA ZA KUKIMBIA MATATIZO

by Admin | 10 March 2022 08:46 pm03

Ni kawaida mwanadamu anapopitia matatizo mengi au shida nyingi, huwa anatamani hata  afanane na mnyama asiyejua shida, anatamani angekuwa kama ndege apae zake aende mbali na makao ya watu akaishi humo.

Ndivyo Daudi alivyosema..kipindi ambacho anafukuzwa na Sauli huko majangwani, alisema..

Zaburi 55:5-8
[5]Hofu na tetemeko limenijia,
Na hofu kubwa imenifunikiza.
[6]Nikasema, Ningekuwa na mbawa kama njiwa,
Ningerukia mbali na kustarehe.
[7]Ningekwenda zangu mbali, 
Ningetua jangwani.
[8]Ningefanya haraka kuzikimbia
Dhoruba na tufani.

Lakini jinsi Mungu alivyotuumba, kamwe hatuwezi kuzitoroka dhoruba na tufani za maisha…fahamu kuwa watu wanaokuudhi ndio hao hao utaendelea kuishi nao, na kama hutaishi nao nyumba moja, basi kuna kipindi mtakutana tu katika nukta fulani ya maisha..

Maadui zako, watesi wako, pamoja na wachawi hakuna siku Mungu atakutenga nao akupeleke katika dunia yako mwenyewe uishi huko kwa starehe, hicho kipindi hutakaa ukifikie haijalishi wewe ni mtakatifu kiasi gani.

Mungu anachokifanya kwetu ni kutulinda na kutuepusha tu na madhara yao, yasitufikie. Lakini kuishi katikati yao ni jambo endelevu mpaka mwisho.
Bwana Yesu alisema;

Yohana 17:15
[15]Mimi siombi kwamba uwatoe katika ulimwengu; bali uwalinde na yule mwovu.


Wakati mwingine, Mungu anapotaka kukupa rizki, anatumia hata njia ya hao hao, unakula katikati yao wakikuona..


Zaburi 23:5
[5]Waandaa meza mbele yangu,
Machoni pa watesi wangu.
Umenipaka mafuta kichwani pangu,
Na kikombe changu kinafurika.

Hivyo ndugu uliyeokoka, acha kutaabika kwa ajili ya wanadamu, wala usipeleke akili zako mbali sana, ukidhania kuwa hao watu walio na wewe kama mwiba kuna siku watatoweshwa milele, uishi peke yako kwa starehe..Kanuni hiyo Mungu hajaichagua japo tunaitamani.


Zaidi sana jifunze kuyatimiza mapenzi ya Mungu katikati yao. Utakuwa na furaha katika maisha.
Kumbuka Mbawa kama za njiwa hatujapewa wanadamu.


Shalom.

Tafadhali washirikishe na wengine habari hizi njema,

Kwa maombezi/Ratiba za ibada/ Ushauri/ Maswali.
Piga namba hizi: +255693036618 au +255789001312

pia kama utapenda uyapate mafundisho haya kwa njia ya Whatsapp au email basi tutumie ujumbe kwenye namba hizo hizo.

Mada Nyinginezo:

Kwanini wakristo wengi ni maskini?.

ALAMA KATIKA VIPAJI VYA NYUSO.

KWANINI MTINI KATIKATI YA MIZABIBU?

Swali: Kurushwa upesi kunakozungumziwa katika Danieli 9:21 ndio kupi?

Rudi nyumbani

DOWNLOAD PDF
WhatsApp

Source URL: https://wingulamashahidi.org/2022/03/10/hujapewa-mbawa-za-kukimbia-matatizo/