NA WATU WOTE WALIKUWA WAKIAMKA MAPEMA, WAENDE HEKALUNI.

by Admin | 28 July 2022 08:46 am07

Jina la Bwana wetu Yesu Kristo libarikiwe karibu tujifunze biblia,

Luka 21:37 “Basi, kila mchana alikuwa akifundisha hekaluni, na usiku huenda kulala katika mlima uitwao wa Mizeituni

38 NA WATU WOTE WALIKUWA WAKIAMKA MAPEMA WAENDE HEKALUNI ILI KUMSIKILIZA”.

Je unaijua sababu ya Bwana Yesu kulala juu ya mlima wa mizeituni?

Si kwasababu hakuwa na watu wa kumkaribisha kwake awe analala kwao? La! alikuwa nao tele!!, na wengine wenye uwezo mkubwa tu!.. mfano wa hao ni Yule Yusufu mwanafunzi wake ambaye alikwenda kumwomba Pilato auondoe mwili wake pale msalabani, maandiko yanasema alikuwa ni mtu tajiri.

Mathayo 27:57 “Hata ilipokuwa jioni akafika MTU TAJIRI wa Arimathaya, jina lake Yusufu, naye mwenyewe alikuwa mwanafunzi wa Yesu;

58 mtu huyu alimwendea Pilato akauomba mwili wa Yesu. Ndipo Pilato akaamuru apewe”.

Mwingine ni Yule aliyempa chumba Bwana Yesu wakati wa Pasaka, (maandiko yanasema mtu huyu alikuwa ni mtu anayemiliki ghorofa, na kuna chumba maalumu, juu ya ghorofa ambacho alikuwa amempa Bwana Yesu na wanafunzi wake).

Marko 14:13 “Akatuma wawili katika wanafunzi wake, akawaambia, Nendeni zenu mjini; atakutana nanyi mwanamume amechukua mtungi wa maji; mfuateni;

14 na po pote atakapoingia, mwambieni mwenye nyumba, Mwalimu asema, Ki wapi chumba changu cha wageni, niile pasaka humo, pamoja na wanafunzi wangu?

15 Naye mwenyewe atawaonyesha orofa kubwa, imeandikwa tayari; humo tuandalieni”.

Umeona?..watu hawa wote walikuwa wanaishi pale pale Yerusalemu, ambao wangeweza kumhifadhi Bwana kipindi yupo Yerusalemu…na sio hao tu, bali pia walikuwepo  na wengine wengi,

Lakini jiulize kwanini Bwana kipindi anakaribia kuteswa hakuwa anakwenda kulala katika nyumba zao?.. Sababu zipo mbili. 1) KUOMBA. na  2) KUWAHI IBADANI.

KUOMBA.

  Bwana Yesu alikuwa ni mtu wa kuomba sana..na alijua mazingira bora ya kuomba ni yapi?, si ghorofani wala nyumbani. Bali ni sehemu iliyo na utulivu. Alijua Nyumbani kunakuwa na usumbufu mwingi ambao ungeweza kumwondoa katika uwepo,(usumbufu wa watu na kimazingira), Ndio maana utaona mara kadhaa akipanda mlimani pamoja na wanafunzi wake kuomba.. Hiyo ikitufundisha na sisi tuwe watu wa kuchagua mazingira sahihi ya kuomba.

KUWAHI IBADANI.

Sababu ya pili ya Bwana Yesu kulala katika mlima wa Mizeituni, ni ili AWAHI IBADANI. Alijua mazingira ya nyumbani si mazingira ambayo si rafiki kwa yeye kuwahi hekaluni.. kwasababu ya maandalizi kuwa mengi..

 Utaona kipindi tu yupo kwa akina Miriamu na Martha, ni jinsi gani, Martha alivyokuwa anamhangaikia kumwandalia vyakula, mara  chai, mara maji ya kunawa na kadhalika…mahangaiko yale, yakachukua mpaka muda wa kuanza kujifunza, mwisho Bwana Yesu ikabidi aanze kufundisha kabla hata ya Martha kumaliza kupika.. na kilichofuata utaona Martha!, alikwazika!..

Sasa mambo kama hayo hayo Bwana Yesu aliyajua ndio maana akatafuta mlima uliopo na hekalu awe analala huko kipindi anaendesha semina ya Masomo pale Hekaluni.

Kwasababu kukisha pambazuka tu, kazi aliyo nayo ni yeye pengine ni kunawa tu uso na kuteremka hekaluni kufundisha, pengine ingemchukua tu robo saa, kufanya maandalizi, tofauti na angekuwa nyumbani kwa watu..kwasababu Mlima wa Mizeituni na hekaluni ni mita kadhaa tu, si mbali..!

Hivyo Bwana Yesu akawa anawahi hekaluni mapema sana, wa kwanza kabla ya wote!..na kuwafundisha wale waliowahi kama yeye (akawa kielelezo). Na wengine wote walipoona kuwa anawahi, na kumkuta akifundisha wachache waliowahi kama yeye, na wenyewe wakawa wanaamka asubuhi na mapema kwenda kumsikiliza, wasikose madarasa hayo ya asubuhi..

Luka 21:37 “Basi, kila mchana alikuwa akifundisha hekaluni, na usiku huenda kulala katika mlima uitwao wa Mizeituni. 38 NA WATU WOTE WALIKUWA WAKIAMKA MAPEMA WAENDE HEKALUNI ILI KUMSIKILIZA”.

Kristo hata leo anawahi asubuhi na mapema Nyumbani kwake!.. na wote walio wake kweli kweli, wanawahi nyumbani kwake kumsikiliza! Na wanapokea Baraka!.

Katika siku hizi za mwisho, shetani anawaharibu wengi katika eneo la USINGIZI, na KUTOKUJALI. Asilimia kubwa ya watu wanaochelewa ibadani, au wasiofika kabisa ibadani ni kwasababu ya Usingizi!, au Kutokujali.

Kama kweli unamjali Bwana Yesu na maneno yake, huna sababu yoyote ya KUCHELEWA IBADANI, hata kama unakaa mbali na kanisa!, Amka mapema wahi kanisani!, KATISHA USINGIZI!!..Tabia ya kupenda usingizi kimwili, inafunua tabia ya kupenda usingizi katika roho, ambayo ni mbaya sana.

Na kama ukiona mahali ulipo ni mbali sana, basi siku moja kabla ya ibada, hamia karibu na maeneo ya kanisa, au kisha kanisani omba, asubuhi yake uamkie nyumbani kwa Bwana, utakuwa umejizolea Baraka nyingi zaidi.

Lakini kama utafika  nyumbani kwa Bwana kwa kuchelewa kwasababu ya usingizi!.. basi ni heri usingefika kabisa kanisani hiyo siku, kwasababu hakuna chochote unachokwenda kupokea hiyo siku!!, ni heri urudi nyumbani ukamalizie usingizi wako tu!!. Tabia ya KUPENDA USINGIZI na ya KUTOKUJALI ni tabia zinazomchukiza Bwana kuliko zote (soma Luka 22:46, Marko 13:35-37).

Na kumbuka hakuna maombi ya kuondoa KUONDOA USINGIZI!!..Dawa ya kuushinda usingizi ni kuamua kubadilisha tabia tu!, na wala si kuombewa!!.. Bwana Yesu alipowakuta akina Petro wamelala muda wa kuomba, hakwenda kukemea mapepo ndani yao!.. alichofanya aliwaambia WAAMKE WAOMBE!.. Roho zao zi radhi, lakini miili ndio midhaifu, hivyo wajilazimishe waamke!.

Na wewe leo hii, Amka mapema nenda Ibadani, amka mapema nenda kwenye maombi, amka mapema nenda shambani kwa Bwana, Ukatae usingizi, na pia Acha kuwa mtu wa KUTOKUJALI.

Bwana atubariki.

Maran atha!

Tafadhali shea na wengine ujumbe huu;

Pia Kwa maombezi/ Ushauri/ Maswali/ Whatsapp:
Tuandikie katika BOXI la Maoni hapo chini au
Piga namba hizi: +255693036618 au +255789001312

Mada Nyinginezo:

NAWAAMBIA MAPEMA!

WALA MSIUANGALIE MWILI, HATA KUWASHA TAMAA ZAKE.

SABATO ILIFANYIKA KWAAJILI YA MWANADAMU NA SI MWANADAMU KWAAJILI YA SABATO!

Mlima wa Mizeituni  unaumuhimu gani kwetu?

Rudi nyumbani

DOWNLOAD PDF
WhatsApp

Source URL: https://wingulamashahidi.org/2022/07/28/na-watu-wote-walikuwa-wakiamka-mapema-waende-hekaluni/