NIMEYATUNZA MANENO YA KINYWA CHAKE ZAIDI YA RIZIKI YANGU.

by Admin | 27 August 2022 08:46 pm08

Ayubu 23:12 “

[12]Sikurudi nyuma kuiacha amri ya midomo yake; Nimeyatunza maneno ya kinywa chake zaidi ya riziki yangu”,

Huyu ni Ayubu, …si ajabu kwanini Mungu alimwona ni mtu mkamilifu  aliyemcha Mungu, kuliko watu wote waliokuwa ulimwenguni wakati ule.

Kitendo cha kuyatunza maneno ya Mungu zaidi ya riziki..si jambo dogo, ni kumaanisha kwa hali ya juu sana.

Ni kawaida mtu akiamka asubuhi jambo la kwanza atakalowaza ni ale nini, anywe nini..haiwekezani mtu apitishe siku nzima bila kukumbuka kuna kitu kinapaswa kiwekwe tumboni, Au asifikirie miradi yake, au kazi zake zinakwendaje siku hiyo,. Labda awe na hitilafu katika neva za ubongo wake.

Lakini Ayubu, ilikuwa ni kinyume, chakula/rizki ilikuwa ni “B” …”A” alipoamka asubuhi alikuwa anatafakari atayatimiza vipi maagizo ya Mungu, alikuwa anawaza siku itapitaje pitaje bila kupiga hatua mpya ya ukamilifu.

Hicho ndicho kilichokuwa chakula chake, alionyesha tabia iliyokuwa kwa mkuu wake YESU KRISTO. Ambaye tunasoma wakati fulani alipofuatwa na wanafunzi wake  kuletewa chakula, aliwaambia maneno haya:

Yohana 4:30-34

[30]Basi wakatoka mjini, wakamwendea.

[31]Huko nyuma wanafunzi wakamsihi wakisema, Rabi, ule.

[32]Akawaambia, Mimi ninacho chakula msichokijua ninyi.

[33]Basi wanafunzi wake wakasemezana, Je! Mtu amemletea chakula?

[34]Yesu akawaambia, Chakula changu ndicho hiki, niyatende mapenzi yake aliyenipeleka, nikaimalize kazi yake.

Ayubu alipoamka asubuhi aliwaza toba,kwa ajili ya wengine.., (Soma Ayubu 1:5)

Alihakikisha Neno la Mungu halidondoki, alifanya agano na macho yake, asiwatazame wanawake akawatamani, (Ayubu 31:1). Aliwaza kuwafundisha wengine hekima na busara na kuwasaidia waliokuwa katika dhiki na uhitaji, (Ayubu 31:16-18), mtu wa namna hii Mungu hawezi acha kumwangalia na ndio maana tunasoma Habari zake mpaka leo.

Je na sisi tunaweza kufanana na watu kama hawa ambao walikuwa na tabia sawa na sisi. Kumbuka Ayubu hakuwa myahudi, wala nabii, wala kuhani..biblia inamwita MTU tu, fulani aliyetokea  katika nchi moja iliyoitwa USI.

Na sisi, hivi hivi tulivyo tuna wajibu wa kumaanisha kuyatunza maneno ya Mungu, katika wokovu wetu, tuhakikishe tunayafanya maneno yake ni sehemu ya maisha yetu ya kila siku, ili tusiwe wasahaulifu. 

Bwana Yesu alitupa amri tupendane..ni lazima tujifunze tabia hii, kila siku, alisema pia tusamehe, tusiposamehe Baba yetu naye hataweza kutusamehe makosa yetu.

Haijalishi umekosewa mara ngapi, umeibiwa mara ngapi, umedhulumiwa mali nyingi kiasi gani, kamwe usiyasahau maneno ya Bwana Yesu.. ‘samehe mara saba sabini…’

Bwana Yesu alisema, kesheni mwombe msije mkaingia majaribuni..ukilisahau hili neno ukawa ni mvivu wa kuomba walau saa moja kwa siku kama alivyosema, wewe sio mkamilifu.Ifikie hatua kama vile tukumbukavyo muda wa kula ndivyo tukumbuke muda wa maombi na ibada. Huko ndiko kuyatunza maneno yake zaidi ya riziki zetu.

Na kwa bidii hiyo Bwana atatuona na kujidhihirisha kwetu,kwasababu sikuzote anazunguka ulimwenguni kote kutafuta watu wenye kumaanisha huku kama Ayubu ajifunue kwao.

2 Mambo ya Nyakati 16:9

[9]Kwa maana macho ya BWANA hukimbia-kimbia duniani mwote, ili ajionyeshe mwenye nguvu kwa ajili ya hao, waliokamilika moyo kuelekea kwake…”

Bwana atutie nguvu.

Shalom.

Tafadhali shea na wengine ujumbe huu;

Pia Kwa maombezi/ Ushauri/ Maswali/ Whatsapp:
Tuandikie katika BOXI la Maoni hapo chini au
Piga namba hizi: +255693036618 au +255789001312

Mada Nyinginezo:

VITABU VYA BIBLIA: Sehemu ya 9 (Kitabu cha Ayubu).

HEKIMA NI NINI? NA UFAHAMU UNAPATIKANA WAPI?

JE UNA MATUMAINI YA KUPATA TENA KILE ULICHOPOTEZA?

Je Musa yupo anawashitaki watu..kulingana na Yohana 5:45?

Bwana alimaanisha nini kusema“maana mtenda kazi astahili posho lake”

MAOMBOLEZO YA HADADRIMONI.

Nini maana ya ugonjwa wa kufisha? (Yeremia 17:9)

Rudi nyumbani

DOWNLOAD PDF
WhatsApp

Source URL: https://wingulamashahidi.org/2022/08/27/nimeyatunza-maneno-ya-kinywa-chake-zaidi-ya-riziki-yangu/