Nijapokuwa sipo kwa mwili, lakini nipo pamoja nanyi kwa roho,

by Admin | 1 December 2022 08:46 am12

SWALI: Mtume Paulo alikuwa na maana gani kusema..

Wakolosai 2:5  “Maana nijapokuwa sipo kwa mwili, lakini nipo pamoja nanyi kwa roho, nikifurahi na kuuona utaratibu wenu na uthabiti wa imani yenu katika Kristo”

Je! Kwasasa kauli hii inasimama katika mazingira gani?

JIBU: Katika mazingira ya kibinadamu kuna wakati inatokea, hutakuwa karibu na watakatifu wenzako kimwili, pengine kwasababu kadha wa kadha, lakini biblia bado inatoa tumaini kuwa hali hiyo ni kweli inaweza kuathiri mwili , lakini roho bado ikawa pale pale inashiriki neema na Baraka kana kwamba hukuondoka, lakini hiyo yote mpaka ifikiwe zipo taratibu zake..

Inahuzunisha kuona Neno hili linachukuliwa juu juu.. Utaona watu wanatoa udhuru zao, halafu mwishoni wanamalizia na hili Neno “Kimwili sipo nanyi, lakini nitakuwa nanyi kiroho” Wakidhani kuwa ni rahisi kiivyo.

Embu tuangalie Paulo aliyesema haya maneno kwa Wakolosai alichochewa na nini mpaka akapata ujasiri wa kusema vile..

1) Ni kwasababu ya vifungo vyake ndio maana alishindwa kuwa karibu na kanisa la wakolosai:

Alilisisitiza hilo mwishoni kabisa mwa waraka wake akasema..

Wakolosai 4:18  Salamu yangu mimi Paulo, kwa mkono wangu mwenyewe. Kumbukeni kufungwa kwangu. Neema na iwe pamoja nanyi

Maana yake ni kuwa kama isingekuwa ni vifungo vile, kulikuwa hakuna udhuru wowote wa yeye kutokuwepo katika mwili na watakatifu. Lakini leo, watakatifu hawapo magerezani, wapo bize na kazi wanasema nimetingwa siwezi kuja kanisani, Hawapo nje ya mikoa au nchi, wapo mtaa wa pili lakini wanasema, kanisani ni mbali, nitakuwa nanyi kiroho. Hapo usijidanganye ndugu, hakuna muunganiko wowote ulio nao wa watakatifu wenzako..Upo nje ya kundi.

2) Alikuwa anawaombea sana kwa dua na sala:

Anasema..

Wakolosai 1:9  Kwa sababu hiyo sisi nasi, tangu siku ile tuliposikia, hatuachi kufanya maombi na dua kwa ajili yenu, ili mjazwe maarifa ya mapenzi yake katika hekima yote na ufahamu wa rohoni.

Japokuwa alikuwa vifungoni, lakini hakupotelea moja kwa moja huko, lakini alifanya bidii kila siku usiku na mchana, kuwaombea ndugu zake aliombali nao. Akiwaombea waimarike, wajazwe maarifa na hekima. Lakini ni mara ngapi, mpendwa mmoja akihama mkoa, au akisafiri nje ya kanisa, ndio anasahau kabisa kuliombea kanisa lake, Hapo Paulo aliliombea kwa Dua..Dua ni maombi ya kuzama ambayo yanaambatana na kufunga na kuomboleza kwa kipindi kirefu. Je na sisi tunafanya hivyo tuwapo mbali?

Na kwa kawaida mtu wa namna hii, atampenda Mungu hata na kwa matoleo yake, na dhabihu, kwa ajili ya kanisa lake. Kwasababu maandiko yanasema, hazina yako ilipo ndipo utakapokuwepo na moyo wako (Mathayo 6:21).

3) Alikuwa akiwaulizia mienendo yao, na kuwapelekea ndugu wa kuwaimarisha

Wakolosai 4:7  Tikiko, ndugu mpendwa, mtumishi mwaminifu, mjoli wangu katika Bwana, atawaarifu mambo yangu yote; 8  ambaye nimemtuma kwenu kwa sababu iyo hiyo, ili mjue mambo yetu, naye akawafariji mioyo yenu; 9  pamoja na Onesimo, ndugu mwaminifu, mpendwa, aliye mtu wa kwenu. Hao watawaarifu mambo yote ya hapa petu.

Zaidi sana alikuwa anawaandikia nyaraka kama hizi, pamoja na kuwatumia za makanisa mengine wazisome, ili waimarike,(Wakolosai 4:16). Je! Na sisi tunaweza kuwa wafuatiliaji wa wapendwa wetu tuliowaacha nyuma? Au tutaliachia kanisa la kule lihusike lenyewe. Kwani wewe si haupo, ya nini tena, kuwaandikia waraka? Lakini Paulo hakuwa hivyo, alijitahidi kutumia karama yake hata kwa kuandika waraka, akiwa huko huko mbali lengo lake likiwa ni karama yake iifaidie kanisa.

.

4) Alikuwa tayari kutoa ripoti na changamoto zake na maendeleo yake katika huduma:

Wakolosai 4:10-13,14 

“Aristarko, aliyefungwa pamoja nami, awasalimu; na Marko, mjomba wake Barnaba, ambaye mmepokea maagizo kwa habari yake; akifika kwenu mkaribisheni. 11  Na Yesu aitwaye Yusto; hao ni watu wa tohara. Tena hao peke yao ni watendaji wa kazi pamoja nami kwa ajili ya ufalme wa Mungu; nao walikuwa faraja kwangu. 12  Epafra, aliye mtu wa kwenu, mtumwa wa Yesu Kristo, awasalimu, akifanya bidii siku zote kwa ajili yenu katika maombi yake, ili kwamba msimame wakamilifu na kuthibitika sana katika mapenzi yote ya Mungu……

14  Luka, yule tabibu mpendwa, na Dema, wanawasalimu.”

Hakujificha, wala hakufanya mambo yake kwa siri, kanisa la Kolosai lilikuwa linafahamu kwa kina maendeleo ya kiroho ya Paulo, kwasababu Paulo mwenyewe alikuwa tayari kueleza wazi. Hakusubiri kufuatiliwa, lakini sasa kigezo cha watu kuwa mbali, ndio sababu ya kutokueleza maendeleo yao, wanapotea kabisa. Hapo hakuna muunganiko wowote.

Hivyo baadaya ya yeye kuyatimiza hayo ndipo sasa Roho Mtakatifu akamshuhudia aandike waraka ule kwamba japokuwa yupo nao mbali kimwili lakini kiroho yupo nao.

Hata sasa, mtu yeyote aliyembali na kanisa anayekidhi vigezo hivyo vyote, rohoni anakuwa hana tofauti na kama tu yupo pale. Hivyo wakibarikiwa wenzake na yeye atabarikiwa, wakipata neema na yeye atapata, Lakini kama atapoteza sifa hizo, haijalishi atatamka kwa maneno mazuri namna gani, hayupo kiroho na wenzake. Na hivyo hawezi shiriki chochote kitokacho kwa Mungu.

Shalom.

Tafadhali shea na wengine ujumbe huu;

Pia Kwa maombezi/ Ushauri/ Maswali/ Whatsapp:
Tuandikie katika BOXI la Maoni hapo chini au
Piga namba hizi: +255693036618 au +255789001312

Mada Nyinginezo:

AMEFANYIKA BORA KUPITA MALAIKA!

Nini maana ya kuabudu malaika? (Wakolosai 2:18)

Maongeo ni nini?(Wakolosai 2:19)

Uasherati wa Kiroho ni nini?

EPUKA MAKUNDI ILI UTAKATIFU WAKO UDUMU!.

KUMJUA YESU SI KUPATA UZIMA WA MILELE.

KUTII NI BORA KULIKO DHABIHU.

Rudi nyumbani

DOWNLOAD PDF
WhatsApp

Source URL: https://wingulamashahidi.org/2022/12/01/nijapokuwa-sipo-kwa-mwili-lakini-nipo-pamoja-nanyi-kwa-roho/