WAANDAA MEZA MBELE YANGU, MACHONI PA WATESI WANGU

by Admin | 26 December 2022 08:46 am12

Mungu kamwe hajatuweka hapa duniani tutafute “dunia njema”, Dunia ambayo tutaishi mbali na hatari, mbali na majanga, mbali ni watu wabaya au waovu, hapana, hili ni jambo ambalo kila mtu aliyempokea Kristo au aliyeokoka anapaswa alijue, hata tujitahidi vipi kutafuta mahali ambapo patakuwa pazuri kwetu bado hatutapaona…

Kwasababu duniani hii ilishaharibika tangu Adamu alipoasi, na iliendelea kuwa hivyo hivyo, na hata sasa itakuwa hivyo hivyo ya hatari hadi mwisho wake, hakuna  mahali utaenda au utakaa na kusema hapa hakuna ukinzani, hakuna masumbufu.., ni kitendo cha muda tu, ukiyashazoelea hayo mazingira mapya utavumbua shida nyingine nyingi na hatari zilizopo hapo,ambazo kule hukuziona, nenda kote ulimwenguni ndio uhalisia ulivyo..

Kitu Mungu anachokifanya ni kutufanya tuwe salama katika mazingira haya mabaya, lakini sio kubadili mazingira yawe mbingu kwetu. Anachofanya ni kutuandalia meza, tule tunywe, katikati ya watu waovu, katikati ya wachawi, katikati ya waganga, katikati ya wauaji, katikati ya wapagani.. Lakini tusidhuriwe na wao..Na anafanya hivyo ili tumaini letu liwe kwake tu.

Daudi alilijua hilo akasema maneno haya katika Zaburi..

ZABURI 23

1 Bwana ndiye mchungaji wangu, Sitapungukiwa na kitu.

2 Katika malisho ya majani mabichi hunilaza, Kando ya maji ya utulivu huniongoza.

3 Hunihuisha nafsi yangu; na kuniongoza Katika njia za haki kwa ajili ya jina lake.

4 Naam, nijapopita kati ya bonde la uvuli wa mauti, Sitaogopa mabaya; Kwa maana Wewe upo pamoja nami, Gongo lako na fimbo yako vyanifariji

5 WAANDAA MEZA MBELE YANGU, MACHONI PA WATESI WANGU. Umenipaka mafuta kichwani pangu, Na kikombe changu kinafurika.

Umeona, anasema waandaa meza mbele yangu machoni pa watesi wangu.. Machoni pa wafanyakazi wenzangu wanaonionea wivu, machoni pa wafanya-biashara wenzangu wanaoniendea kwa waganga, machoni pa majirani zangu wanaoniundia visa kila kukicha..Hapo ndipo Mungu anapokuletea chakula chako, anapokuchunga, anapokupa faraja..Kamwe usitazamie atakupeleka mbinguni, kukupa rizki, au Baraka zako.

Usihangaike kumwomba Mungu akubadilishie mazingira akupe mengine, au akubadilishie watu akupe wengine, au akubadilishie majirani, au wafanyakazi, au akuhamishe mahali ulipo akusogeze kwingine kwasababu hapo ulipo ni pabaya sana.. Mungu atakusogeza wakati wake ukifika, lakini fahamu kuwa hata huko uendako, hata hao watu wengine uwakutao, matatizo yanaweza kuzuka hata makubwa kuliko ya kwanza.. Lakini mwombe Bwana katika mazingira yoyote akusaidie,, Hilo linatosha yeye awe mchungaji wako, awe mwamba wako, awe jemedari wako wa vita, ndio maombi anayotaka kuyasikia, na huwa anayajibu upesi, maombi ya namna hii. Mwombe akufanikishe hapo hapo ulipo, akupe amani na faraja hapo hapo ulipo..

Bwana Yesu alimwomba Mungu maneno haya..

Yohana 17:15 “Mimi siombi kwamba uwatoe katika ulimwengu; bali uwalinde na yule mwovu”.

Si mapenzi ya Bwana, wewe ukae mbali na walimwengu, bali katikati yao, mpaka wakati wa Bwana utakapofika ndio akuondoe na kukupeleka pengine.  Wakristo wengi wameathiriwa na mazingira yanayowazunguka, wanapoona hatari nyingi mbele yao au  nyuma yao. Badala waweke tegemeo lao kwa Bwana awasaidie watimize mapenzi ya Mungu, wanabakia kuyalaumu mazingira, wakisema, ni kwasababu ya hiki, ni kwasababu ya kile..Yule ananipiga vita ndio maana sina muda na Mungu..Laiti ningeondoka hapa na kwenda kule ningetumika vizuri zaidi  n.k…

Ndugu, Dunia hii iliyoanguka haina mahali utakuta pana unafuu, zaidi ya pengine, hapatakuwa na wachawi lakini patakuwa na magonjwa, hapatakuwa na magonjwa lakini patakuwa na uzito kiroho, au mwitikio wa watu kwa Mungu ni mdogo, hapatakuwa na maskini lakini patakuwa na majanga,..Hivyo hatari zipo na zitaendelea kuwepo kwasababu mkuu wa ulimwengu huu yupo kote.

Lakini tukiegemea kwa Bwana, na kumlilia yeye atembee nasi, atulinde, atuokoe, atupe amani, atupe faraja,atupiganie, na sio kuyalaumu mazingira, tutakuwa salama.

Wakati Fulani Mungu alinionyesha usiku katika ndoto, nilijikuta nimeingia katika jumba Fulani, lakini sikufahamu kama ni milki ya adui..Hivyo nikiwa kule nikawa kuzungumza na mama mmoja ambayr alikuwa kama kafungwa, lakini ghafla, mahali pale palibadilika,nikaanza kuwaona watu wanaotumiwa na ibilisi ndani ya mazingira yale, nikagundua uwepo wa pale sio wa ki-Mungu, bali ni milki ya ibilisi, basi nikawa natafuta mlango wa kutoka niondoke, lakini milango yote ilikuwa imepotea, basi nikawa nazunguka zunguka kwenye lile jumba lenye mazingira ya kutisha, kutafuta mlango wa kutokea sioni, kila nikiingia kwenye mlango mmoja, nakutana na chumba kingine, nikifungua kile huku nikitazamia ndio mlango wa kutoka nje, ndio kwanza nazama katika vyumba vya ndani zaidi..

Lakini nikiwa huko ndotoni, nikajikuta Napata hisia nyingine, nikasema Bwana ndiye ngome yangu ninahofu ya nini..Nikasema sitahangaika tena kutafuta mlango wa kutokea, nitatulia tuli, niendelee kumwangalia Bwana wangu, nikasema hapa nitatoka tu nisiwe na hofu..Na muda huo huo ghafla , nikawaona wenzangu wakiwa katika chumba kimoja wapo ndani ya hilo jumba, tukakutana wote tukiwa na amani sana kana kwamba pale sio ndani ya jumba la shetani, tukawa tunakula na kunywa, halafu tukaanza kuimba nyimbo nzuri za kumsifu Mungu, nakumbuka mahali pale niliona uwepo mzuri wa Bwana kana kwamba tulikuwa kanisani,

Na ghafla nikashutuka, ndipo Mungu akanifundisha neno hili..

Zaburi 23:5 Waandaa meza mbele yangu, Machoni pa watesi wangu. Umenipaka mafuta kichwani pangu, Na kikombe changu kinafurika.

6 Hakika wema na fadhili zitanifuata Siku zote za maisha yangu; Nami nitakaa nyumbani mwa Bwana milele.

Hivyo tuondoe hofu ya watu, tumtazame Bwana. Na yeye atatuokoa.

Shalom.

Tafadhali shea na wengine ujumbe huu;

Pia Kwa maombezi/ Ushauri/ Maswali/ Whatsapp:
Tuandikie katika BOXI la Maoni hapo chini au
Piga namba hizi: +255693036618 au +255789001312

Au jiunge na makundi yetu ya mafundisho ya kila siku kwa kwa njia ya Whatsapp kwa kubofya hapa >>>> WHATSAPP GROUP

Mada Nyinginezo:

Njia zote za mtu ni safi machoni pake mwenyewe;(Mithali 16:2)

Je ni lazima kushiriki Meza ya Bwana?

YESU ANAKWENDA KUIBADILISHA OFISI YAKE.

SALA YA BWANA. (Namna ya kuiomba)

MEZA YA BWANA, NA KUTAWADHANA MIGUU.

Mahali pa juu palikuwa ni wapi kama tunavyosoma katika biblia?

Ni miaka mingapi ya njaa Daudi aliyoambiwa achague? Ni miaka 7 au miaka 3?

Rudi nyumbani

DOWNLOAD PDF
WhatsApp

Source URL: https://wingulamashahidi.org/2022/12/26/waandaa-meza-mbele-yangu-machoni-pa-watesi-wangu/