Kwanini Tomaso atake kwenda kufa pamoja na Lazaro? (Yohana 11:14-16).

by Admin | 17 February 2023 08:46 am02

Jibu: Tusome,

Yohana 11:14  “Basi hapo Yesu akawaambia waziwazi, Lazaro amekufa.

15  Nami nafurahi kwa ajili yenu kwamba sikuwako huko, ili mpate kuamini; lakini na twendeni kwake.

16  Basi Tomaso, aitwaye Pacha, akawaambia wanafunzi wenziwe, Twendeni na sisi, ili tufe pamoja naye”

Kwa haraka ni rahisi kutafsiri kuwa Tomaso alitaka na yeye kwenda kufa pamoja na Lazaro, lakini kiuhalisia sio hivyo!.

Tomaso hakutaka kwenda kufa pamoja na Lazaro, bali hapo alimaanisha “kwenda kufa pamoja na Bwana Yesu”.

Ili tuelewe vizuri tuanze kusoma kisa hicho kuanzia juu mstari ule wa tano..(Zingatia vipengele vilivyoainishwa kwa herufi kubwa).

Yohana 11:5  “ Naye Yesu alimpenda Martha na umbu lake na Lazaro.

6  Basi aliposikia ya kwamba hawezi, alikaa bado siku mbili pale pale alipokuwapo.

7  Kisha, baada ya hayo, akawaambia wanafunzi wake, TWENDENI UYAHUDI TENA.

8  Wale wanafunzi wakamwambia, Rabi, JUZIJUZI TU WAYAHUDI WALIKUWA WAKITAFUTA KUKUPIGA KWA MAWE, NAWE UNAKWENDA HUKO TENA?

9  Yesu akajibu, Je! Saa za mchana si kumi na mbili? Mtu akienda mchana hajikwai; kwa sababu aiona nuru ya ulimwengu huu.

10  Bali akienda usiku hujikwaa; kwa sababu nuru haimo ndani yake.

11  Aliyasema hayo; kisha, baada ya hayo, akawaambia, Rafiki yetu, Lazaro, amelala; lakini ninakwenda nipate kumwamsha.

12  Basi wale wanafunzi wakamwambia, Bwana, ikiwa amelala, atapona.

13  Lakini Yesu alikuwa amenena habari ya mauti yake; nao walidhania ya kuwa ananena habari ya kulala usingizi.

14  Basi hapo Yesu akawaambia waziwazi, Lazaro amekufa.

15  Nami nafurahi kwa ajili yenu kwamba sikuwako huko, ili mpate kuamini; lakini na twendeni kwake. 16  Basi Tomaso, aitwaye Pacha, akawaambia wanafunzi wenziwe, TWENDENI NA SISI, ILI TUFE PAMOJA NAYE”

Katika kisa hiki tunaona Bwana Yesu anawapa taarifa wanafunzi wake ya kurejea tena kule Uyahudi ambapo walitaka kumpiga mawe mpaka afe!.. na taarifa hiyo ikawashitusha wanafunzi inakuwaje anataka kurudi tena huko kwenye hatari! (Maana yake si ndo anaenda kufa sasa!)

Lakini  Tomaso aliposikia wanafunzi wenzake wakimhoji hivyo, ndipo na yeye akawashauri kwamba wasimwache aende pake yake huko uyahudi, bali nao pia waende pamoja naye, ili kama ikitokea kauawa basi na wao wafe pamoja naye!.

Ni moyo mzuri aliokuwa nao Tomaso, lakini hakujua kuwa kufa kwaajili ya Kristo ni Neema na si jambo la kujiamulia tu au kujivunia kwamba linaweza kutendeka kwa uwezo wa mtu.

Mtume Petro alijaribu hilo zoezi kama la Tomaso likamshinda, kwasababu alidhani anaweza kufa ajili ya Kristo kwa nguvu zake..

Luka 22:31 “Akasema, Simoni, Simoni, tazama, Shetani amewataka ninyi apate kuwapepeta kama vile ngano;

32  lakini nimekuombea wewe ili imani yako isitindike; nawe utakapoongoka waimarishe ndugu zako.

33  Akamwambia, Bwana, niwapo pamoja nawe, mimi ni tayari kwenda gerezani AU HATA KIFONI.

34  Akasema, Nakuambia, Petro, jogoo hatawika leo, kabla wewe hujanikana mara tatu ya kuwa hunijui”.

Zaidi sana huyu Tomaso ambaye alitaka kwenda kufa pamoja na Bwana, siku Bwana anakamatwa alimkimbia, hakuonekana!..(huenda ndo alikuwa Yule kijana aliyekimbia uchi, Marko 14:52)…na zaidi sana hata baada ya kufufuka kwake bado ilikuwa ni ngumu kuamini mpaka alipotokewa na Bwana Yesu..(huyo ndio mtu aliyetaka kwenda kufa na Yesu Yerusalemu)

Kwahiyo kwa hitimisho ni kwamba Tomaso hakutaka kwenda kufa na Lazaro, vinginevyo ingekuwa haina maana… lakini kinyume chake alitamani kwenda kufa pamoja na Bwana kwasababu aliamini huo ni ushujaa mkuu wa Imani.

Jambo tunaloweza kujifunza ni kuwa, hatupaswi kuzitumainia nguvu zetu, hatuwezi kusema tutamtumikia Mungu kwa nguvu zetu, hatuwezi kujivuna kuwa tutafanya hiki au kile kwa nguvu zetu, bali siku zote hatuna budi kuwa katika hali ya unyenyekevu, na kujishusha mbele za Bwana, kama tunatamani kufa kwaajili ya Bwana kifo cha kishujaa, basi tumalizie kwa kusema, BWANA TUSAIDIE

Na chochote kile tukifanyacho au tukikusudiacho ni lazima kumalizia kwa kusema “KWA MSAADA WA BWANA KITAFANIKIWA”.. Lakini tukijivuna kuwa tunaweza hiki au kile, tutaishia kumkana na hata kumsaliti.

Bwana akubariki.

Maran atha!

Tafadhali shea na wengine ujumbe huu;

Pia Kwa maombezi/ Ushauri/ Maswali/ Whatsapp:
Tuandikie katika BOXI la Maoni hapo chini au
Piga namba hizi: +255693036618 au +255789001312

Mada Nyinginezo:

Kwa kuwa ni shida mtu kufa kwa ajili ya mtu mwenye haki;

TUKIO LA MUSA NA ELIYA KUMTOKEA BWANA, LIMEBEBA UJUMBE GANI?

MPENDEZE MUNGU ZAIDI.

Je ni kweli kila nafsi itaonja mauti kulingana na (Zaburi 89:48)?

Nini maana ya “mtakayoyafunga duniani, yatakuwa yamefungwa mbinguni”?

Rudi nyumbani

DOWNLOAD PDF
WhatsApp

Source URL: https://wingulamashahidi.org/2023/02/17/kwanini-tomaso-atake-kwenda-kufa-pamoja-na-lazaro-yohana-1114-16/