Alani ni nini?(1Samweli 17:51)

by Admin | 29 August 2023 08:46 pm08

Alani ni kifuko cha kuhifadhia upanga ambacho huvaliwa kiunoni na askari hususani wakati wa vita. Tazama picha juu.

Neno hilo utalisoma katika vifungu hivi;

1Samweli 17: 51 “Ndipo Daudi akapiga mbio, akasimama juu ya Mfilisti, akautwaa upanga wake, akaufuta alani mwake, akamwua, akamkata kichwa kwa upanga huo. Nao Wafilisti walipoona ya kuwa shujaa wao amekufa, wakakimbia”

1Nyakati 21:27 “Bwana naye akamwamuru malaika; naye akaurudisha upanga wake alani mwake tena”.

Yohana 18:11  “Basi Yesu akamwambia Petro, Rudisha upanga alani mwake; je! Kikombe alichonipa Baba, mimi nisikinywee?”

Soma pia,  Ezekieli 21:3, 5

Je! Chombo hichi kinafunua nini rohoni?

Kama tujuavyo upanga na alani, ni kama pochi na pesa, havitengani. Na upanga, kibiblia ni Neno la Mungu (Waefeso 6:17, Waebrania 4:12). Hivyo Neno la Mungu halihifadhiwi penginepo zaidi ya kwenye moyo. Pale linapohitajika kutumika hutolewa moyoni na sio penginepo. Kwahiyo chombo hichi kijulikanacho kama Alani, kinauwakilisha moyo wa Mtu.

Na kama tunavyojua upanga hutumiwa na mtu yoyote, unaweza hata kumwangamiza  mwenye nao, ukitumiwa na adui. Ndivyo alivyojaribu kufanya shetani alipomjaribu Bwana na kumwambia ‘imeandikwa’, Lakini kwasababu Yesu alikuwa amejaa ‘Kweli yote’. Aliweza kumpokonya upanga huo huo na kummaliza nao.

Hivyo ni muhimu pia kujaa ‘Kweli yote’ sio Neno tu peke yake, yaani kuufahamu ukweli wa Neno la Mungu. Kwasababu ibilisi anaweza kulitumia kukuangusha ikiwa hutakamilishwa katika hilo, kwamfano anaweza kuja kukwambia kuoa wake wengi si dhambi, kwani Yakobo, alioa wake wengi, Daudi alioa wake wengi, Sulemani alioa wake wengi, na wote hawa walikubaliwa vizuri na Mungu, vivyo hivyo na wewe ukifanya hivyo utakubaliwa tu, hamna shida,. Lakini je! Hiyo ni kweli yote? Kweli yote inasema Mungu alimuumba mtu mke na mume, na hao wawili watakuwa mwili mmoja.(Mathayo 19:4-9), hakuumba Adamu mmoja, Hawa wengi. Hivyo usipojua kuligawanya vema Neno la Mungu kwa msaada wa Roho ni rahisi shetani kukupiga.

Na ndio maana maandiko yanatusihi tuivae ‘kweli’ kiunoni.

Waefeso 6:13  “Kwa sababu hiyo twaeni silaha zote za Mungu, mpate kuweza kushindana siku ya uovu, na mkiisha kuyatimiza yote, kusimama. 14  Basi simameni, hali mmejifunga kweli viunoni, na kuvaa dirii ya haki kifuani,”

Bwana akubariki.

Tafadhali shea na wengine ujumbe huu;

Pia Kwa maombezi/ Ushauri/ Maswali/ Whatsapp:
Tuandikie katika BOXI la Maoni hapo chini au
Piga namba hizi: +255693036618 au +255789001312

Mada Nyinginezo:

JE UPANGA UMEINGIA MOYONI MWAKO?

Silaha za Mkono wa kuume na za mkono wa kushoto ni zipi

Kwanini Bwana Yesu aliwaagiza wanafunzi wake wakanunue upanga?

Nini maana ya Dirii, Chapeo na Utayari?

Kwanini Mungu aseme “Alaaniwe azuiaye upanga wake usimwage damu” (Yeremia 48:10).

NA VIUNGO VYETU VISIVYO NA UZURI VINA UZURI ZAIDI SANA.

Rudi nyumbani

DOWNLOAD PDF
WhatsApp

Source URL: https://wingulamashahidi.org/2023/08/29/alani-ni-nini1samweli-1751/