JINSI YA KUISHINDA HALI YA MSONGO WA MAWAZO.

by Admin | 14 December 2023 08:46 pm12

Msongo wa mawazo ni nini? Ni shinikizo au mfadhaiko wa kiakili, unaomkumba mwanadamu, pale anapokutana  na  matatizo, au taabu, au dhiki au shida Fulani. Hivyo inapotokea mtu huyu anashindwa kuzitatua changamoto hizo, ndipo msongo huo huja.

Kwamfano labda mtu amegundulika, ana ugonjwa usiotubika, na kaambiwa na daktari hawezi kupona, mtu kama huyu ni rahisi kukumbwa na msongo wa mawazo,

Au labda mwingine  hana kazi na akiangalia familia inamtegemea, na bado hajafikia malengo yake kulinganisha na umri alionao, moja kwa moja mtu kama huyu ni rahisi kukumbwa pia na msongo wa mawazo. N.k.

Na kama tiba isipopatikana matokeo yake yanaweza kuwa mtu huyo, kupata matatizo ya kiafya, wengine kuchanganyikiwa, wengine kujitenga na watu, wengine kujifungia ndani kulia tu usiku kucha, wengine kutenda vitendo viovu,hata kujiua.

Je! Mkristo anaweza kuwa na msongo wa kimawazo? Jibu ni ndio anaweza kuwa nao. Lakini tiba imeshatolewa. Tutaona katika somo hili kwa namna gani, kwasababu yawezekana wewe ni mmoja wapo ambaye unakutana na hali hii na hujui cha kufanya.

Embu tuone kwanza baadhi ya watu katika maandiko ambao walipitia misongo ya mawazo

1) Eliya:

Eliya wakati amemaliza kuwaua manabii wa Baali, akatazama huku na huku na kujiona kama ni yeye peke yake ndiye nabii wa Mungu aliyebaki, hivyo ikampelekea ajitenge, na kukimbilia jangwani, akae huko mpaka afe.  Lakini Mungu alikuja kumtokea baada ya siku 40, akampa majibu ya faraja, kwamba asidhani yupo peke yake kuna wengine 7,000 amejisazia, rudi Israeli, kanitumikie.(1Wafalme 18-19)

2) Mfalme Daudi.

Alikumbwa mara nyingi na msongo wa mawazo katika maficho yake alipokuwa anawindwa na mfalme Sauli. Mara nyingi alifikia hatua ya kukata tamaa ya maisha. Embu tafakari haya maneno aliyoyasema Daudi.

Zaburi 69:1 Ee Mungu, uniokoe, Maana maji yamefika mpaka nafsini mwangu.  2 Ninazama katika matope mengi, Pasipowezekana kusimama. Nimefika penye maji ya vilindi, Mkondo wa maji unanigharikisha.  3 Nimechoka kwa kulia kwangu, Koo yangu imekauka. Macho yangu yamedhoofu Kwa kumngoja Mungu wangu.  4 Wanaonichukia bure ni wengi Kuliko nywele za kichwa changu. Watakao kunikatilia mbali wamekuwa hodari, Adui zangu kwa sababu isiyo kweli. Hata mimi nalilipishwa kwa nguvu Vitu nisivyovichukua.  5 Ee Mungu, unajua upumbavu wangu, Wala hukufichwa dhambi yangu

3) Ayubu

Baada ya kupotelewa na mali zake, na watoto wake, hadi mwili wake kubaki mifupa tu. Mkandamizo ulimjia. Ayubu anasema;

Ayubu6:2 Laiti uchungu wangu ungepimwa, Na msiba wangu kutiwa katika mizani pamoja!  3 Kwa kuwa sasa ungekuwa mzito kuliko mchanga wa bahari; Kwa hiyo maneno yangu yamekuwa ya haraka

 Mpaka akanza kusema maneno magumu, ya kulaana siku aliyozaliwa. Mtu kama huyu alikuwa katika hali mbaya sana kifikra na kiakili.

4) Petro

Petro na Yuda walipitia jambo moja, kukana na kusaliti, ni dhambi pacha. Isipokuwa Yuda alikwenda kujinyonga kwasababu msongo wa mawazo ulimshinda, lakini Petro hakujinyonga. Yeye alikwenda kujificha na kulia sana kwa “majonzi”.  Tengeneza picha ni wewe unamkana Mungu wako, tena kwa maneno ya dhihaka mbele za watu. Hali hiyo unadhani itakufanya ujionaje kama sio mateso ya kiakili baada ya hapo?. Wengine wanapitia hali kama hizi, wanapojiona wamemtenda Mungu dhambi kubwa sana, isiyosameheka, wakidhani kuwa Mungu hawajali tena, hawathamini.(Mathayo 26:75)

5) Mitume 11.

Baada ya Bwana Yesu kufa, hofu ya wayahudi ikawavaa mitume, wakiona kuwa wao ndio wanaofuata kuuliwa baada ya kiongozi wao kufa.. Hivyo hiyo ikawapelekea kujifungia ndani, wasitoke. Msongo mkubwa sana wa mawazo uliwavaa, kutoka kwa wayahudi.(Yohana 20:19-29)

Itoshe tu kutumia mifano hiyo michache, kwani wapo wengine wengi sana katika biblia waliopitia hali kama hizi, mfano ni Musa, Yusufu, Yeremia, Nebukadreza, Hana(mamaye Samweli),  Danieli, Mtume Paulo wote hawa ukisoma habari zao katika biblia utayathibitisha hayo.

Lakini Je! Waliwezaje kuzishinda hizo hali.

Utagundua, walipopotia taabu zao, walilikumbuka TUMANI la Mungu. Ndilo lililowapa nguvu ya kuweza kuvuka nyakati hizo mbaya walizozipitia.  Waliyazingatia haya maneno;

1Petro 5:6  Basi nyenyekeeni chini ya mkono wa Mungu ulio hodari, ili awakweze kwa wakati wake; 7  HUKU MKIMTWIKA YEYE FADHAA ZENU ZOTE, kwa maana yeye hujishughulisha sana kwa mambo yenu.

Na lile alolilisema Yesu..

Mathayo 11:28  Njoni kwangu, ninyi nyote msumbukao na wenye kulemewa na mizigo, nami nitawapumzisha

Pale akili zilipogoma, fikra kuzima, moyo kuwa baridi, walijifunza kumtwika Mungu, huzuni zao, mateso yao, shida zao. Hata pale ambapo hazikutatulika kwa wakati walioutarajia, lakini waliendelea na mwisho wa siku Bwana alikuja kuyaweka yote sawa. Kwasababu yeye mwenyewe alisema.

Yeremia 29:11 Maana nayajua mawazo ninayowawazia ninyi, asema Bwana, ni mawazo ya amani wala si ya mabaya, kuwapa ninyi TUMAINI siku zenu za mwisho

Hivyo ndugu, ikiwa na wewe upo katika hali hii ya msongo wa kimawazo, katika eneo lolote lile, iwe la kiroho, kihuduma, kifamilia, kikazi, kiafya, kimaendeleo. Umeshindwa kuendelea mbele, Usiogope. Kwa Mungu lipo TUMAINI, zaidi ya Matumaini yote ya kibinadamu.

Haijalishi msongo huo, umekupata kutokana na dhambi zako, au kutokana na hali zilizo nje ya uwezo wako. Usiogope. Mponyaji, mfajiri, mtatuaji wa matatizo yupo. Huyu si mwingine zaidi ya YESU KRISTO mwokozi.

Mungu akikupa tumaini, ujue ni lazima litokee, lakini mwanadamu akikupa tumaini, ni kusudi tu kukufariji, lakini tatizo linaweza kubaki palepale.  Yesu hayupo hivyo. Mtazame tu yeye. Wakati wa shida, ndio wakati wa kukimbilia chini ya mbawa zake, sio kuwakimbilia wanadamu.

JE! UFANYEJE?

  1. Katika hali hiyo, Usiache kuomba sana  & Kumsifu Mungu & Kushukuru, siku zote za maisha yako. Ongeza kiwango chako katika eneo hili.
  2. Soma sana Biblia: Utapata faraja ya Roho katika uwezo wa Mungu aliowatendea wengine.
  3. Usiwe mtu wa kutanga-tanga sana. Tuliza akili zako, si lazima utafute ushauri kwa kila mtu, jiachie kama vile huna tatizo lolote, ukimkabidhi Bwana yote, ukijua yeye yupo kazini.
  4. Kila wakati Jiambie, “Mungu wangu atayaweka yote sawa mwisho wa siku”.
  5. Mawazo ya kushindwa/kujihukumu yanapokuja yapinge.  Sema “Bwana ndiye boma langu na ngome yangu, na mwamba wangu sitatikisika”.

Na hakika, katika muda fulani, utaona Mungu anakuvusha, anakuponya, anakufariji, anakuondolea huo mzigo. Huo ni uhakika sio makisio. Usiache tu kuendelea na Bwana..

Bwana akubariki.

Tafadhali shea na wengine ujumbe huu;

Pia Kwa maombezi/ Ushauri/ Maswali/ Mafundisho Whatsapp:
Tuandikie katika BOXI la Maoni hapo chini au
Piga namba hizi: +255789001312 au +255693036618. Jiunge na magroup yetu ya whatsapp kwa kubofya hapa > WHATSAPP-Group

Mafundisho mengine:

TUMAINI NI NINI?

UKIOKOKA,HIZI FIKRA ZIKIJA NDANI YAKO, ZIKATAE.

VITA VYA KIFIKRA BAADA YA KUZALIWA MARA YA PILI

TUUTAFUTE UMOJA WA ROHO.

Je shetani ana uwezo wa kujua mawazo ya mtu?

Tofauti kati ya ndoto na Maono ni ipi?

Rudi nyumbani

DOWNLOAD PDF
WhatsApp

Source URL: https://wingulamashahidi.org/2023/12/14/jinsi-ya-kuishinda-hali-ya-msongo-wa-mawazo/